Advertisements

Tuesday, May 31, 2011

Mauaji Tarime: Daktari atishiwa kuuawa

Anthony Mayunga, Tarime
DAKTARI aliyesimamia uchunguzi wa miili ya watu wanne kati ya watano waliouawa na Polisi Mei 16, mwaka huu akiziwakilisha familia za wafiwa amedai kwamba ametumiwa ujumbe wa maandishi kwa simu kwamba atauawa.

Daktari huyo, Grayson Nyakarungu wa Mwanza alisimamia uchunguzi wa miili ya Chacha Ngoka, Emmanuel Magige, Bhoke Chawali na Mwikwabe Mwita katyika uchunguzi uliofanyika Mei 23, mwaka huu.

Alisema kwamba alipokea ujumbe wa simu mara mbili kwa nyakati tofauti Mei 26, mwaka huu akiwa safarini kuelekea Dar es Salaam uliojaa vitisho.
 

Alidai kwamba moja wa ujumbe huo unaosomeka, “Hizo ripoti siyo za kisiasa, acha kujiingiza kichwa kichwa utajutia, Tundu Lissu ndiye anakutumia ili yeye apate umaarufu, usipokoma kwa onyo hili, tutakushughulikia, subiri mahakamani ukatoe ushahidi, usidanganywe...”

Dk Nyakarungu alisema mara baada ya kupokea ujumbe huo, alipiga simu katika namba hiyo na kupokewa na mwanamke aliyedai kuwa yuko Mwanza ambaye hakutaka kujitambulisha. Alidai kwamba mara baada ya kukata simu hiyo, alipokea ujumbe mwingine uliosema:

“Hata ukitutambua utafanya nini, narudia mara ya mwisho, hizo ripoti haziwahusu wanahabari, funga domo lako.”Dk Nyakarungu alisema kwamba ametoa taarifa juu ya matukio hayo katika Kituo cha Polisi, Oystebay, Dar es Salaam na kufunguliwa jalada namba OB/RB/9214/11.

Hata hivyo, alisema licha ya vitisho hivyo hataogopa kwa kuwa alitumwa na familia na amelazimika kuwapa taarifa zote zilizojitokeza.Alisema inaelekea kuwa aliyetuma ujumbe huo amekuwa akimfuatilia kwa kuwa ametuma ujumbe huo katika namba zake mbili tofauti za simu.


CHANZO:MWANANCHI

No comments: