ANGALIA LIVE NEWS

Tuesday, December 27, 2011

Takwimu za wizara, mkoa kuhusu waliofutiwa matokeo zatofautiana

Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA)



Wakati Afisa  Usalama  wa Mkoa wa Mwanza, Meja  Joson Mutashongerwa, akikusudia kuwashtaki walimu wote  ambao  wamesababisha udanganyifu na hatimaye wanafunzi 42 wakafutiwa matokeo ya mitihani ya kuhitimu elimu ya msingi mkoani hapa,  imebainika kwamba takwimu zilizotolewa  na Afisa Elimu wa mkoa zinatofautiana na zilizotolewa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.
Mkoa  wa Mwanza umetangaza kuwa wanafunzi 42 pekee ndio wamefutiwa matokeo, tofauti na wanafunzi 333 ambao walitangazwa na  Naibu Waziri, wa Elimu na Mafunzo ya ufundi, Philipo Mulugo.
Waziri Mulugo  alitangaza kuwa  Mkoa  wa Mwanza  una jumla ya  wanafunzi 333  ambao  wamefutiwa matokeo  mwaka huu  kutokana na vitendo vya  udanganyifu.


Mkoani Mwanza, matokeo  hayo yalitangazwa Desemba 14  mwaka huu na Afisa Elimu wa mkoa, Hamis  Maulidi, siku ambayo Mulugo  alitangaza matokeo hayo  ngazi ya taifa.
Wakati  akitangaza matokeo hayo, Maulidi  alisema wanafunzi 42 wamefutiwa matokeo mkoani hapa  kutokana na uchunguzi  uliofanywa na ofisi  yake uambao pia uliwasilishwa katika Baraza  la Mitihani la Taifa (Necta)  kwa ajili ya kupitiwa.
“Awali ni shule 20 ndizo  zilituhumiwa kufanya udanganyifu. Na ndipo Baraza la Mitihani  lilipotuagiza kufanya uchunguzi na tulifanya hivyo, tukawatumia na baadaye wakabaini kuwa ni shule 4 tu zenye  wanafunzi 42 ambazo  zilikumbwa na udanganyifu huo,” alisema.
Alisema kuwa awali kabla ya uchunguzi,  wanafunzi 500 wangelifutiwa matokeo katika  mkoa wa Mwanza pekee.
 Maulidi alisema idadi hiyo ni kubwa  huku akishauri hatua kali za kinidhamu zichukuliwe dhidi ya  walimu (wasimamizi  wa mitihani) waliosababisha  udanganyifu huo.
Alipoulizwa  kuhusiana na tofauti hiyo, Maulidi  alistuka na kudai  kwamba yeye hana taarifa za kuwepo kwa tofauti hiyo.
“Kwa kweli mimi sina taarifa za kuwepo kwa tofauti  kati ya matokeo ya mkoa na matokeo yaliyotangazwa na Wizara. Hata  hivyo, siwezi kusema lolote kwa vile sina nakala ya  taarifa  iliyowasilishwa na  Waziri,” alisema Maulidi  wakati  alipoulizwa na NIPASHE ofisini kwake.
Alisema takwimu alizozitoa wakati akitangaza matokeo ndizo ambazo amepokea kutoka Baraza la Mitihani na kwamba hata Waziri  ametumia takwimu za matokeo  kutoka Necta.
Maulidi alitangaza matokeo hayo katika ukumbi wa shule ye sekondari Mwanza jijini hapa mbele  ya Katibu Tawala wa Mkoa  wa Mwanza, Doroth Mwanyika ambaye alikuwa amefuatana na walimu wakuu shule za sekondari, wataalamu pamoja na viongozi  wengine kutoka sekretarieti ya mkoa, maafisa  elimu, Wakurugenzi  wa Halmashauri pamoja na wenyeviti wa Halmashauri zote saba za mkoa wa Mwanza.
 Baada  ya kupokea  taaria ya kufutwa kwa matokeo ya wanafunzi 42,  Afisa Usalama wa Taifa  mkoani hapa, Mutashongerwa, alisema atahakikisha kuwa walimu waliohusika katika udanganyifu wanafikishwa mahakamani.


Alisema ni vyema walimu hao na waliokuwa wasimamizi wa mitihani wakafikishwa mahakamni ili liwe fundisho kwa walimu wengine wenye tabia kama hiyo
CHANZO: NIPASHE

No comments: