Advertisements

Friday, April 13, 2012

IJUE DUNIA YA WANAWAKE WAKOROFI!-2

NI wakati mwingine tunakutana tena katika safu yetu nzuri kabisa ya kuelimishana juu ya mapenzi. Nina imani upo tayari kupata kitu kipya kama ilivyo kawaida ya ukurasa huu kila wiki.
Ndugu zangu, tuendelee na mada yetu. Nazungumza juu ya namna ya kuishi na mwanamke ambaye kiasili ni mkorofi. Wiki iliyopita nilianza na utanguzi tu, sasa hebu tuingie katika eneo muhimu.

JIONE MWENYE JUKUMU
Nilitangulia kusema, ikiwa umeshamchunguza mwanamke wako vya kutosha na kufikia hatua ya kuingia naye katika ndoa, yupo moyoni mwako. Bila shaka utakuwa umeridhishwa na tabia yake.
Inawezekana huo ujeuri au ukorofi mwanzoni hakuwa nao na sasa unaona ni tabia mpya usiyoipenda na unatamani kuachana naye au kutoka kwenye ndoa (kwa wenye ndoa).
Kikubwa hapa unatakiwa kutambua kuwa mwanamke wako ana tabia hiyo, halafu pili ujue kuwa jukumu la kukabiliana na tabia hiyo lipo mikononi mwako. Hii itakuwa hatua nzuri ya kuelekea kwenye mafanikio.
KUWA MSIKILIZAJI
Ukishatambua jukumu lako la kuhakikisha unakomesha tabia yake, anza na hatua ya kuwa msikilizaji zaidi wakati unapozungumza naye. Mara nyingi ukorofi wa mwanamke huanzia pale utakapotoa hoja, akatakiwa kujibu.
Wakati mwingine, inawezekana alitoa hoja, ukamjibu lakini akaingilia kati. Hapo sasa unatakiwa kuwa msikilizaji zaidi. Usijali amekudharau, mwache azungumze mpaka achoke.
Usikivu wako kupitiliza, utamgongea alamu kichwani mwake na huenda akaelewa kwamba ‘kelele’ zake hazikufurahishi. Vichwa ngumu wanaweza wasielewe hilo, hatua inayofuata itakusaidia sana.
MPE MIFANO
Jenga hoja zako kwa mifano, mweleze hisia zako lakini fananisha na tukio lingine la watu wengine. Zungumza kwa staha na uoneshe umakini na uhakika wa kila kinachotoka kinywani mwako.
Kama ni wa kuelewa atakuelewa tu lakini kama ni wale ambao ujeuri na ubishi upo kwenye damu yake, mpe dawa nyingine hapa chini.
USIMBISHIE SANA
Hata kama unaona anakushushia heshima kiasi gani, anakujibu jeuri kwa kiwango gani, usibishane naye sana. Mweleze msimamo wako halafu mwache aendelee kujibishia mwenyewe.
Siku zote wewe utabaki kwenye heshima, maana kunyamaza kwako kutaonesha umedharau ‘pumba’ zake.
KUBALIANA NA KILA KITU
Hatua hii ni muhimu sana na yenye nguvu kuliko zote. Kama umeshagundua tabia yake ni kubisha na kupinga kila kitu akiamini yeye yupo sahihi zaidi, usiumize kichwa, kubaliana naye kwa kila kitu.
Hata kama anazungumza ‘utumbo’ muunge mkono na umweleze kuwa ana busara sana ya kufikiria. Faida katika hatua hii ni kwamba, kama alitoa mawazo yake katika mambo ambayo baadaye yanatoa matokeo mabaya.
Matokeo mabaya ndiyo yatakayomshtua na kumfanya ajione fikra zake hazikuwa sahihi. Endelea kumuunga mkono kwa kila unachoona hakifai na mwisho kabisa, matokeo yasiyotarajiwa yakijirudia mara kwa mara, atajirudi na kuanza kukusikiliza.
MRUDISHE KWENYE MSTARI
Huu ni wakati wako sasa wa kuonesha kuwa kwa muda wote huo ulikubaliana naye kwenye mambo yake yote ili muweze kufikia hapa, kumrudisha kwenye mstari. Mweleze madhara yote yaliyopatikana na umfundishe njia sahihi ya kuwasilisha hisia zake.
Mfundishe namna ya kuzungumza na wewe, umweleze wazi kuwa hupendi ‘kupigiwa kelele’ na yeye kwa kuwa unampenda na anapaswa kukuheshimu wewe kama kiongozi wake (mpe nukuu za maandiko matakatifu).
Tumia fursa hii vizuri sana kumwelewesha juu ya wajibu na haki zake kama mpenzi wako. Kwa kutumia kauli nzuri, atakuelewa na hata kama tabia hii ni sugu na ya muda mrefu itakoma.
JENGA MASIKILIZANO
Hii ni hatua muhimu zaidi, unapatakiwa kujenga masikizano ya pande zote mbili. Pamoja na kwamba ametambua kuwa unapaswa kuheshimiwa na kusikilizwa, usimfanye akaamini kwamba wewe ni mbabe na unataka kumburuza!
Mpe nafasi ya kutoa hisia zake na umsikilize vizuri. Mpe thamani na heshima ya mawazo yake. Kama unapingana naye uwe na hoja. Hapo sasa rafiki yangu utakuwa umejenga uhusiano mzuri ambao hauna migogoro. Suala la ujeuri, kiburi na ubishi litakuwa limefikia ukingoni!
Kwa leo naweka kituo kikubwa hapa, wiki ijayo nitakuja na mada nyingine kali zaidi, USIKOSE!

Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Mambo ya Mapenzi anayeandikia magazeti ya Global Publishers, ameandika vitabu vya True Love, Let’s Talk About Love na Who is Your Valentine? vilivyopo mitaani.

No comments: