Advertisements

Monday, December 3, 2012

Fahamu madhara ya kuongeza makalio

NEW YORK, Marekani
VIDEO iliyoonyweshwa mwishoni mwa wiki katika mitandao mbalimbali ya kijamii, ambayo ilielezea madhara ya taratibu anayoyapata mwanamke aliyeongeza ukubwa wa makalio, kwa dawa za silkoni imewashtua wanawake wengi waliowahi kutumia aina yoyote ya madawa hayo.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa madawa hayo badala ya kumfanya mwanamke awe laini, video hiyo inaelezea namna ukuaji wa haraka wa makalio pamoja na kuathirika huku yakiachwa katika sura mbaya sehemu za nyuma (chini) baada ya muda mfupi.
Imebainika kuwa pamoja na dawa za kuongeza ukubwa wa makalio ya akina dada kupendwa, dawa hizo pia zina madhara kwa afya ya binadamu.
Wataalamu wa mambo wanadai kwamba pamoja na kuongeza ukubwa wa makalio pia dawa huleta matatizo ya kuvimba kwa ngozi ya makalio katika mpangilio usio sahihi.
Dawa hizo pia zimetajwa kuwa husababisha kwa uwepo mkubwa wa ugonjwa wa  saratani.
Video hiyo ya sekunde 20, inamwonyesha mwanamke aliyeongeza makalio yake kwa dawa za silicone akionyesha namna alivyoathirika kutokana na matumizi ya madawa hayo huku akisema : "Hivi ndivyo nilivyoongeza ukubwa wa makalio yangu".
Anaongeza: "Sidhani kama ni sahihi kufanya hivi. Nadhani kuna ulazima wa kuyaondoa haya makalio yangu yote kwa sasa." alisikika akisema.
Mpaka kufikia jana video hiyo ambayo pia iliwekwa katika mtandao wa kijamii wa Facebook tayari ulikuwa umependezwa na watu 278,000 wanaotembelea huku ikiwa imehamishwa na watu zaidi ya 430,000 wakipeleka katika kurasa zao.
Mtumiaji mmoja wa mtandao huo kutoka nchini Marekani Donna Wright-Levy, alichangia akisema: "Mimi hupendelea kwenda maeneo kadhaa ambako hutengenezwa shepu yangu kwa madawa haya sasa nina ulazima wa kwenda kupima saratani".
Ni vigumu kuthibitisha mwanamke huyu alitumia kliniki gani wakati alipofanyiwa uongezwaji wa ukubwa wa makalio yake miaka miwili iliyopita.
Lakini mmoja wa madaktari kutoka kliniki ya upasuaji ya BAAPS Aurora nchini Uingereza Adrian Richards, ambaye pia ni mshauri wa upasuaji anaamini kuwa mwanamke huyo alifanyiwa marekebisho ya makalio yake kwa dawa za silicone.
Alisema tatizo hutokea wakati nyama ya makalio inaposhindwa kuulinda vema mwili na kuwa imara katika nyama na mifupa na hivyo madhara huanza kutokea juu ya ngozi na kusambaa mpaka ndani ya nyama na baadaye mfupa.
Ni matatizo ambayo ni ya kawaida kumfika mtumiaji ya dawa za kuongeza ukubwa wa maumbile iwe ni matiti ay makalio. Ni lazima itokee baada ya muda maana kama kitu kilipulizwa na upepo ina maana wakati wake ukiisha kitarudi kama awali.
"Huyu mwanamke aliyaongeza makalio yake kwa nyuma na kwa juu zaidi hivyo tayari madhara yake yamekuwa ni makubwa kwa maana hakufanya upasuaji bali alitumia njia za mkato za silicone, " alisema Richards.
Alisema ni lazima anapata maumivu makali, lakini alipendekeza kuwa ni vema kama makalio hayo yangeondolewa kabisa ili kuzuia maambukizi  kuendelea.
Uongezwaji wa makalio ni jambo lililoshamiri mno Amerika ya Kusini ambapo ukubwa wa makalio unapimwa kama kigezo kimojawapo katika ngono.
Katika miaka ya karibuni, upasuaji na uongezwaji wa makalio ni kati ya mambo yaliyopigwa vita huku wanawake wengi wakionywa sana ambapo idadi kubwa ya watu maarufu pamoja na wengine wamekufa kufuatia huduma hii.
Mwezi Aprili mwaka jana, mama wa watoto watatu mwenye umri wa miaka 42 alifariki wakati akifanyiwa upasuaji wa kuongeza ukubwa wa makalio yake katika kliniki moja huko Las Vegas.
Desemba 2009, aliyekuwa Miss Argentina alifariki dunia wakati akijitahidi kufanyiwa upasuaji wa kuongeza ukubwa wa makalio yake.
Solange Magnano, 38, aliwahishwa hospitalini kwa ajili ya kufanyiwa matibabu baada ya kuzidiwa katika kliniki ya oparesheni ya vipodozi kwa kushindwa kupumua.
Habari iliyosambaa duniani mwaka 2011 ni kuhusiana na April Brown, raia wa Marekani ambaye alikuwa mwanamitindo, kutokana na tamaa yake ya kuwa na makalio makubwa, alijikuta akikatwa miguu na mikono baada ya kuchoma sindano zenye dawa za kumuwezesha kuwa na umbile hilo.
Akizungumza kwa masikitio na mtandao mmoja wa habari za kijamii, mrembo huyo alisema: “Ni tukio lililoyateteresha maisha yangu. Nilikuwa na umbile la kawaida tu lakini nikaingiwa na tamaa na kusaka makalio makubwa.
“Wapo walionishauri nitumie vidonge lakini baadaye nikaambiwa naweza kupata shepu hiyo kwa kuchoma sindano.
“Nilichoma sindano hizo kwenye zahanati bubu na mwanzoni niliona mabadiliko kwa kuongezeka lakini baadaye nikaanza kujisikia hali ya tofauti, nilipokwenda hospitali wakaniambia nimepata infections (maambukizi).
“Kadiri siku zilivyozidi kwenda, hali yangu nayo ilizidi kuwa mbaya na nilivyokwenda kwa daktari aliniambia kwa maambukizi niliyopata kutokana na kuchomwa sindano yenye silkoni inayotumika viwandani, ilikuwa lazima nikatwe miguu na mikono.
“Sikuwa na jinsi, ilibidi nikubaliane na ushauri wao na ndipo nilipopata kilema hiki,” anasema April ambaye sasa anaendesha kampeni ya kuwaelimisha wanawake wenzake juu ya madhara ya kutumia madawa ya kuongeza makalio.
Hali ikoje nchini?
Kwa hapa nchini baadhi ya mastaa na wengineo wanadaiwa kutumia dawa  hizo maarufu kama za Kichina kwa lengo la kuongeza makalio na matiti yao.
Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) ilishawahi kuteketeza dawa nyingi za kuongeza ukubwa wa maumbile ya kiume, dawa za Kichina za kuongeza makalio, kurudisha bikira, kukuza matiti, kuongeza hips, kukuza uume na kahawa ambayo hutumika kuongeza hamasa kwa wanawake.
Wafanyabiashara wengi  wamekuwa hawatumii misingi ya utaratibu na kanuni za vyakula dawa na vipodozi. Dawa za Kichina zinazouzwa kila kona zimekuwa na athari kubwa kwa maisha ya binadamu na baadhi zimekuwa zikiongeza shinikizo la damu.
Licha ya njia hiyo, pia kuna aina nyingine ya kukuza ukubwa wa makalio inayotumiwa kwa sasa na wanawake wengi hasa wa mjini si ya kumeza wala kupaka dawa bali ni ya kuvaa taiti zilizojaladiwa vifaa maalum vilivyotuna mithili ya makalio.
Mmoja wa wafanyabiashara wa ‘makalio’ hayo aliyejitambulisha kwa jina la Mama Sanura, alisema ubunifu huo umekuja kufuatia utafiti kuonesha kuwa baadhi ya wanawake wanatamani kuwa na makalio makubwa ila wanaogopa kutumia dawa za Kichina.
“Wanawake wengi wanatamani kuwa na makalio makubwa lakini hawakujaaliwa kuwa nayo, wapo ambao wamefikia hatua ya kutumia zile dawa za Kichina na ilipobainika zina madhara wameacha.
“Watu wakakaa na kuumiza vichwa, ndipo walipogundua njia hii ambayo ni salama kwani anachotakiwa kufanya mwanamke ni kununua taiti hizo ambazo ndani yake kuna kitu chenye shepu ya kalio na hips, akivaa na suruali au sketi, huonekana amejaaliwa kumbe hamna kitu,” alisema mama huyo mwenye duka lake la nguo maeneo ya Kariakoo, jijini.
Herieth Makwetta kwa msaada wa mtandao wa gazeti la Mwananchi

1 comment:

Anonymous said...

Wanawake yajulieni maumbile yenu,namna ya kuvaa, na mtapendeza,kuliko walio na makalio makubwa.usiige uvaaji wa mwenzio.Ijue kwanza shepu yako mama mtoto.Poleni saana!!!!!!!!!!