Wednesday, February 6, 2013

Mke wa bosi wa benki auawa kinyama Dar

WATU wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wame muua kinyama mke wa Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki M. Meera Sanjeev Kumar kwa kumfunga plasta mdomoni wakiwa katika harakati za kufanya uhalifu nyumbani kwa ofisa huyo.


Taarifa za mauaji hayo zilitolewa polisi na Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono ambaye aliwaambia waandishi wa habari kuwa alifika Kituo Kikuu cha Polisi Oysterbay kutoa taarifa za mauaji hayo.

Akizungumza jana Kama nda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo ambayo aliyaita ni ya kinyama na kueleza kuwa maja mbazi hao watashughulikiwa ipasavyo.
“Ni kweli kuna mauaji hayo yametokea eneo la Masaki ambako mama mmoja Meera Sanjeev Kumar (52) ameuawa majira ya saa tano usiku juzi akiwa nyumbani kwake,” alisema Kamanda Kenyela.

Alisema watu hao wanaodhaniwa ni majambazi walifika katika nyumba hiyo iliyoko kiwanja namba 1500 na ku mfunga kamba mikononi na miguuni na halafu plasta mdomoni na puani na kusababisha kifo chake.
“Wakati wa tukio, mume wake aitwaye Sanjeev Kumar(56) hakuwepo nyumbani na aliporudi alimkuta mkewe akiwa kwenye kochi na tayari amekwishafariki,” alisema Kamanda Kenyela na kuongeza;

“Baada ya kukuta hali hiyo, alipatwa na mshtuko na kupiga simu polisi ambao walifika katika nyumba hiyo na kukuta mauaji hayo.”

Alisema baada ya polisi kufika walielezwa kuwa nyumba hiyo ina walinzi watatu, lakini walikutwa wawili wakiwa wamelala huku mmoja wao akiwa hayupo eneo hilo.

“Tulifuatilia na kubaini kuwa wale walinzi walikuwa wako hoi baada ya kula chakula kilichokuwa kimewekwa dawa ya kulevya ambayo yalisababisha walewe na kushindwa kujitambua,” alisema Kamanda Kenyela na kuongeza;

“Mlinzi mwenzao wa tatu ambaye inadaiwa ndiye aliyewapelekea chakula hicho na kuhusika na njama za kufanyika kwa uhalifu huo alitokomea na majambazi hayo na hajulikani aliko hadi sasa.”

Kamanda Kenyela alisema hadi sasa haijulikani kama kuna kitu kilichoibwa kwa kuwa mume wa marehemu huyo bado hajatulia kuweza kueleza kama kuna fedha au kitu chochote kilichoibwa.

Alisema walinzi waliokuwa wanalinda nyumba hiyo wote ni wa Kampuni ya Securex na kitendo kilichofanywa na mmoja wao ni kusaliti lindo lao na kujihusisha na ujambazi jambo ambalo ni hatari.

“Tunamsaka mlinzi huyo kwani amesababisha mauaji na kwamba tabia ya walinzi kujihusisha na uhalifu inatisha kwa kuwa kama wenyewe wanajihusisha na ujambazi basi ni hatari,” alionya Kenyela.

Alisema ni muhimu kampuni za ulinzi zikawa makini na watu zinaowaajiri kwa kuweka takwimu zao vizuri ili wanapofanya uhalifu kama huo wajulikane mapema.
Kamanda Kenyela alisema hivi sasa Kinondoni kuna tishio la baadhi ya walinzi kujihusisha na ujambazi kitu ambacho kinafanya kazi ya polisi kuwa ngumu.
Alisema tishio jingine ni la madereva wa bodaboda ambao nao wamekuwa wakijihusisha kwenye ujambazi.
Katika hatua nyingine, mwili wa mfanyakazi wa mkazi wa jijini Dar es Salaam, Issack Banda, raia wa Malawi aliyeteswa hadi kufariki Jumatano iliyopita, umezikwa leo katika makaburi ya Mwananyamala kwa Kopa.

Marehemu, aliteswa kwa kufungwa kamba na baadaye kuchomwa moto kutokana na kutuhumiwa kumwibia tajiri yake, kiasi cha mali zenye thamani ya zaidi ya Sh 80 milioni zilizokuwa katika nyumba ili yopo Kinondoni.

Marehemu ambaye alikuwa akifanya kazi ya kutunza na kulinda nyumba ya mwanamke huyo ambaye pia anaishi nchini Marekani, alifariki dunia juzi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kutokana na majeraha aliyoyapata baada vipigo na moto aliochomwa na tajiri yake.

Kauli ya Polisi
Kamanda wa Polisi Kino ndoni, Charles Kenyela alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba wanamshikilia mwanamke huyo ili kuisaidia polisi katika uchunguzi wa shauri hilo.
Kenyela alisema polisi wanachunguza tukio hilo na hasa madai kuwa mama huyo alimtesa marehemu kwa kumfunga kamba miguuni na mikononi tangu awasili kutoka Marekani mwezi Januari 22, mwaka huu hadi Jumamosi iliyopita baada ya kubaini kuwa mali zake zenye thamani ya Sh80 milioni zimetoweka.

Ndugu wa marehemu Mjomba wa marehemu aliyejitambulisha kwa jina la Samson Tindwa alisema kuwa yeye ndiye ambaye alimpeleka marehemu kufanya kazi kwa mama huyo zaidi ya miaka miwili iliyopita na kilichotokea kinamsikitisha kwani hakutegemea kama nduguye angefanyiwa unyama wa namna hiyo na mtu ambaye anamuamini.

“Mimi ndiye ambaye nilimpeleka marehemu kufanya kazi kwa mama huyo na nyumbani kwao hapo kulikuwa na watu wengine ambao wanaishi ikiwa ni pamoja na mfanyabiashara wa mwanamume mmoja mwenye asili ya Kiasia ambaye alikuwa mshirika wa biashara wa mama huyo,” alisema.

Alisema jamaa za mama huyo ambao walikuwa wanaishi katika nyumba hiyo wametoweka baada ya upotevu huo na hali hiyo ndio ambayo imefanya mama huyo kumng’ang’ania marehemu ambaye licha ya kujitetea kuwa hakuchukua, lakini hakumsikiliza.
Mwananchi

No comments: