Advertisements

Wednesday, February 27, 2013

YANGA YAZIDI KUJIKITA KILELENI , YAICHAPA KAGERA SUGAR 1-0


Haruna Niyonzima (wa pili kutoka kushoto) mfungaji wa bao la ushindi katika mchezo wa leo dhidi ya Kagera Suagr

Bao lililofungwa na kiungo wa kimataifa raia wa Rwanda Haruna Niyonzima dakika ya 66 ya mchezo, limeifanya timu ya Young Africans kuendelea kujikita kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom nchini Tanzania bada ya kuichapa timu ya Kagera Sugar kwa bao 1-0 katika mchezo uliofanyika leo katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Young Africans imeendelea kujiweka katika nafasi nzuri ya msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom baada kufikisha point 42 na mabao 35 ya kufunga, pointi 6 mbele ya timu inayoshika nafasi ya pili Azam Fc yenye pointi 36 huku timu zote zikiwa zimecheza michezo sawa. 
Kikosi cha mholanzi Ernest Brandts kiliuanza mchezo kwa kasi na katika dakika 15 za kwanza washambuliaji wake Didier Kavumbagu na Said Bahanuzi walikosa nafasi za wazi za kuweza kuipatia timu ya Yanga bao la mapema kutokana na kupoteza nafasi za wazi.

Kagera Sugar ilicheza soka la kushambulia kwa kushitukiza na kupitia washambuliaji wake Shija Mkina na Darlington Enyima lakini umakini wa walinzi wa Yanga Kelvin Yondani na Nadir Haroub 'Cannavaro' ulikuwa kikwazo kwao kuweza kulifikia lango la watoto wa Jangwani.

Dakika ya 45 ya mchezo, mwamuzi Simon Mberwa alitoa penati kwa Yanga kufuatia mlinda mlango wa Kagera Sugar Hannington Kalyesubula kumchezea madhambi mshambuliji Dider Kavumbagu, penati hiyo ilipigwa na Kavumbagu mwenyewe ambaye alikosa na mpira kuwa wa kutoka.

Mpaka dakika 45 za kpindi cha kwanza zinamalizika, Young Africans 0 - 0 Kagera Sugar.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi na Yanga kuutawala mchezo na kuhakikisha wanasaka bao la mapema lakini umakini wa walinzi wa Kagera Sugar na kuwachezea faulo nyingi washambuliaji wa Yanga ilipunguza radha ya mchezo kutokana na mwamuzi kupuliza filimbi mara nyingi na kuharibu mipango ya kupata bao.

Haruna Niyonzima aliwainua washabiki wa Young Africans dakika ya 66 baada ya kuifungia timu yake bao la kwanza na la ushindi baada ya kufanya jitihada binafsi za kuwahadaa walinzi wa Kagera Sugar na kupiga shuti kali ililokwenda moja kwa moja wavuni na kumuacha mlinda mlango wa Kagera Sugara akiruka kuuokoa mpira huo bila mafanikiko.

Kocha Brandts alifanya mabadiliko ya kuwaingiza Jerson Tegete na Hamis Kiiza kuchukua nafasi za Said Bahanuzi na Didier Kavumbagu mabadiliko yaliyoifanya Yanga kuendelea kuumiliki mpira na kucheza pasi za kuonana kwa umakini zaidi, kwani kiungo FranK Domayo alipiga shuti kali lililogonga mtambaa wa panya na kurudi ndani kabla ya kuokolewa na walinzi wa Kagera Sugar.
Mpaka mwisho wa mchezo Young Africans 1 - 0 Kagera Sugar
Kocha mkuu wa Yanga Ernest Brndts amesema anashukuru timu yake  kupata kwa ushindi katika mchezo wa leo, kipindi cha kwanza washambuliaji hawakuwa makini lakini kipindi cha pili timu ilibadilika sana hali iliyopelekea kuutawala mchezo kwa kipindi chote na kupata bao hilo la ushindi
Kikubwa tulikuwa tunahitaji ushindi wa pointi 3 amabzo tumefanikiwa kuzipata, kila mchezo kwetu ni fainali ili kujiweka katika mazingira mazuri ya kutwaa Ubingw, inabidi tushinde kila mchezo na ninashukru tumeshinda, tunajiandaa na mchezo dhidi  ya Toto Africans siku ya jumamos ya tarehe 09.03.2013 'alisema Brandts'
Baada ya mchezo huu wa leo kikosi cha Young Africans kitaendelea na mazoezi yake kesho asubuhi katika uwanja wa mabatini Kijitonyama ikiwa ni maandalizi ya mchezo unaofuata dhidi ya timu ya Toto African mwishoni mwa wiki ijayo katika dimba la uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
 Young Africans: 1.Ally Mustapha 'Barthez', 2.Mbuyu Twitel, 3.Oscar Joshua, 4.Nadir Haroub'Cannavaro', 5.Kelvin Yondani, 6.Athuman Idd 'Chuji', 7.Saimon Msuva, 8.Frank Domayo, 9.Said Bahanuzi/Jerson Tegete 10.Didier Kavumbagu/Hamis Kiiza, 11.Haruna Niyonzima 
Kagera Sugar: 1.Hannington Kalyesubula, 2.Benjamin Asukulie, 3.Muganyizi Martin, 4.Malegesi Mwanga, 5.Amandus Nesta, 6.Geroge Kavila, 7.Julius Mrope, 8.Juma Nade, 9.Darlington Enyima/Themi Felix, 10.Shija Mkina, 11.Daud Jumanne/Paul Ngwai

No comments: