Wednesday, June 5, 2013

Somo la dini kuendelea kufundishwa shuleni

Dk Shukuru Kawambwa
Baraza Kuu la Waislam Tanzania (Bakwata) limesema masomo ya dini yataendelea kufundishwa shuleni na mitihani ya taifa ya somo hilo kutahiniwa na Baraza la Mitihani la Taifa(Necta) kama ilivyo kawaida.

Kauli hiyo imetolewa baada ya hivi karibuni Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kuliandikia barua Baraza hilo na kujulisha kuwa somo hilo sasa litasimamiwa na viongozi wa dini wenyewe na halitakuwa katika mfumo wa Necta.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, jijini Dar es Salaam Kaimu Mufti wa Tanzania, Sheikh Ali Muhidin Mkoyogore kwa niaba ya Mufti, alisema wanaipongeza serikali kwa usikivu katika hoja iliyotolewa na baraza hilo na kufikia uamuzi huo. "Tunapenda kuipongeza serikali pamoja na kuwashukuru Waislamu wote nchini kwa ujumla kwa mchango wao katika kuunga mkono hoja za Bakwata hadi kufikia muafaka huu na serikali, hivyo Waislamu tujitahidi kuwahamasisha vijana wetu wasome zaidi masomo ya dini kwa faida ya hapa duniani na akhera," alisema Sheikh Mkoyogore
Bakwata ilipeleka barua Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kuilalamikia hatua ya kuondoa somo la dini na kujibiwa Juni 3, mwaka huu, kuwa wizara imefuta barua yake ya awali, hivyo masomo ya dini yataendelea kufundishwa na kutahiniwa na Necta kama kawaida.
CHANZO: NIPASHE

No comments: