ANGALIA LIVE NEWS

Sunday, July 14, 2013

VITUO VYA WATOTO YATIMA KUNUFAIKA MSIMU WA RAMADHAN

Rais Mstaafu Mhe. Ali Hassan Mwinyi, akikabidhi sabuni, mafuta na vitabu kwa watoto yatima kati ya 700 wa madrasa Kisarawe, wakati wa futari ya pamoja na wafanyakazi wa Vodacom Tanzania, walioambatana na Mwenyekiti wa bodi ya Vodacom Foundation Hassan Saleh (kulia) kupitia kampeni ya Pamoja na Vodacom ambayo imetenga kiasi cha shilingi milion 50 kwa ajili ya kipindi hiki cha Ramadhan.
Rais Mstaafu Mhe. Ali Hassan Mwinyi, akikabidhi mbuzi kwa mmoja wa watoto yatima kati ya 700 wa madrasa Kisarawe, wakati wa futari ya pamoja na wafanyakazi wa Vodacom Tanzania, kupitia kampeni ya Pamoja na Vodacom ambayo imetenga kiasi cha shilingi milioni 50 kwa ajili ya kipindi hiki cha Ramadhan.
Rais Mstaafu Mhe. Ali Hassan Mwinyi, akimsikiliza Mwenyekiti wa bodi wa Vodacom Foundation Hassan Saleh, akimfafanulia jambo wakati wa futari na baadhi ya watoto yatima kati ya 700 wa madrasa Kisarawe, iliyoandaliwa na Vodacom Foundation kupitia kampeni yake ya Pamoja na Vodacom ambayo imetenga kiasi cha shilingi milion 50 kwa ajili ya kipindi hiki cha Ramadhan.
Baadhi ya wafanyakazi wa Vodacom Tanzania wakiwapa vyakula baadhi ya watoto wa madrasa wanaoishi katika mazingira magumu Kisarawe Pwani wakati wa futari iliyaoandaliwa na Vodacom Foundation kupitia kampeni yake ya Pamoja na Vodacom iliyotenga kiasi cha shilingi milioni 50 kwa ajili ya kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani na kuudhuriwa na Mgeni rasmi Rais Mstaafu Mhe. Ali Hassan Mwinyi hayupo pichani.
KISARAWE-PWANI Katika kipindi hiki cha msimu wa mwezi mtukufu wa Ramadhani vituo mbalimbali vya watoto yatima hupata misaada kutoka taasisi mbalimbali ikiwa ni sehemu ya kuwa pamoja na kuwafarij wagonjwa na watoto waishio katika mazingira magumu.

Vituo vingi vimekuwa vikikabiliwa na changamoto kubwa ya miundombinu na maradhi kwa watoto wanaokaa au kulelewa katika vituo hivyo, na katika msimu huu wa ramadhani ambao mara nyingi uhitaji wa chakula kinachokidhi haja ya watoto wanaoishi katika vituo hivyo huwa ni mkubwa kutokana na aina ya vyakula vinavyo hitajika kufuturu.

Kutokana na kukabiliana na changamoto zinazovikabili vituo hivyo kampuni ya Vodacom kupitia mfuko wa huduma za jamii wamezindua mpango wa Pamoja na Vodacom ambao utawezesha vituo mbalimbali vya kulelea watoto yatima na wengine waishio katika mazingiza magumu wakipata msaada wa chakula na maradhi katika kipindi hiki cha msimu wa Ramadhan.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo Kisarawe, Mkoa wa Pwani, Mwenyekiti wa kitengo cha huduma za jamii “Vodacom Foundation”, Hassan Saleh alisema kuwa mpango huu ambao umedumu kwa miaka sita hadi sasa utashuhudia vituo kadhaa nchini vikipata msaada wa chakula, nguo, madawa pamoja na vifaa vya kujifunzia.

“Hiki ni kipindi muhimu kwa ndugu zetu waislam kwa kuwa karibu zaidi na Mungu, lakini pia kipindi hiki kinatoa fursa kwa watu mbalimbali kujumuika na wagonjwa pamoja na watu wengine waishio katika mazingira magumu na kuwa pamoja nao, kuwafariji na kuwasaidia mahitaji yao mbalimbali,” alisema Saleh, na kuongeza kuwa.

“Kwetu sisi kupitia mfuko wetu wa huduma za jamii tumejiwekea mpango huu wa kuhakikisha tunawaunga mkono wale wote wanaojumuika na makundi haya kuhakikisha tunawafariji na kuwapatia mahitaji yote muhimu katika kipindi hiki cha msimu wa Ramadhani.”

“Kwa kuanzia katika mpango huu, tutashuhudia zaidi ya watoto 700 kutoka katika vituo mbalimbali vya mkoa wa pwani wakipata misaada hii na baada ya hapo tutaenda katika mikoa mingine ya bara na visiwani,” alisema Saleh.

Rais wa Zamani wa Tanzania, Alhaj Ali Hassan Mwinyi, ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi, aliipongeza kampuni ya Vodacom kwa juhudi zake za kuwasaidia Watanzania kwa njia mbalimbali.

“Ni furaha yetu kuona jinsi ambavyo mnaendela kuwasaidia wananchi wa Tanzania. Tunawatakia kila la kheri katika majukumu yenu ya kila siku,” alisema rais huyo wa zamani.

No comments: