ANGALIA LIVE NEWS

Tuesday, January 14, 2014

Shukuruni Katika Kila Jambo Maana Hayo Ni Mapenzi Ya Mungu Kwenu katika Kristo Yesu.

1 Wathesalonike 5:18
Tuna kila sababu ya kumshukuru Mungu wetu, kama Mtume Paulo anavyotukusha katika barua yake kwa 1 Wathe 5: 18.  Kwanza, hatuna budi ya kumshukuru Mungu  kwa kutusaidia kuumaliza Mwaka 2013.  Pili, tuna sababu nyingi za kumshukuru Mungu kwa kutuingiza katika Mwaka Mpya, 2014.  Haya yote ni mapenzi ya Mungu kwetu.  Katika Mwaka 2013, tuliweza kuuona Mkono wa Bwana katika mambo mengi; kwa mfano, Mungu alitusadia kutimiza umri wa miaka minne katika Ibada ya Kiswahili Columbus. Pili, 2013 tuliweza kuuona Wema wa Mungu pale Ibada  ya  Kiswahili Columbus ilipofanikiwa  kupata utambulisho rasmi ndani ya KANISA la Kiinjili la Kilutheri hapa Marekani, kuanzia ngazi ya Sinodi mpaka makao makuu yake pale Chicago.  Kwa hakika, tuna kila sababu ya kumshukuru Mungu wetu kwa mafanikio makubwa ndani ya Umoja wetu.
Vilevile,  katika Mwaka 2013 tuliweza kupata baraka ya ushirikiano mkubwa kutoka kwa wadhamini wetu,  ambao ni kanisa la Gethsemane na kanisa la Ascension.  Kupitia kwa watumishi wa Mungu,  Mchungaji June Wilknis  na Mchungaji Tim Miller, tulifanikiwa kupata huduma  mbalimahali; kwa mfano mahali pa kuabudia, huduma ya mpiga kinanda, na huduma nyingine muhimu  bila ya matatizo yoyote.  Vilevile, tulifanikiwa kupata huduma za kiroho, kimwili na kijamii pale tulipokuwa na mahitaji ndani ya Ibada ya Kiswahili na ndani ya jumuiya yetu kwa ujumla.  Kwa hakika, tuliweza kuuona Mkono wa Mungu ukiwa katikati yetu.   Mwaka 2013, ulizidi kuwa ni mwaka wa baraka kwetu pale Mungu alipotupatia huduma za kiuchungaji  kwa karibu zaidi kupitia mtushi wake, Mchungaji Ipyana Mwakabonga.  Tuliipotazama NEEMA ya BWANA katika mambo haya yote, tuliweza kufungua vinywa vyetu na kumshukuru Mungu wetu, “Pamoja na Kwa Umoja”  tulisema Mungu wetu ndiye EBENEZA ndani ya Umoja wetu.
Wapendwa katika Kristo, Mkono wa Bwana umetusaidia kuuona Mwaka Mpya, 2014.  Pamoja na kuendelea kutoa shukrani zetu kwa Mungu wetu aliyetutoa mbali na kutufikisha katika Mwaka 2014, tunamuomba kila mmoja wetu aendelee kuumbea UMOJA wetu pamoja na huduma ya Ibada Ya Kiswahili Columbus.  Karibuni tuitangaze Habari hii Njema ,“Pamoja na kwa Umoja,”  Habari Njema ambayo Mungu ametutendea ndani ya JUMUIYA yetu.  Habari Njema  iletayo furaha pale penye huzuni.  Pamoja na kwa Umoja tuwe NURU ndani na nje ya jumuiya yetu .  Nuru iletayo Mwanga. Mwanga wenye kuleta matumaini mema kwa watoto wa Mungu. Haya yote yatawezekana kwa IMANI , kama tunavyokumbushwa na nabii Jeremia, “ … nitakuonyesha mambo makubwa, magumu usiyoyajua.” Yer.33:3.
Mwisho, tunamuomba kila mmoja wetu awe huru kutoa maoni au ushauri utakaoiboresha  huduma ya “Ibada Ya Kiswahili Columbus” katika Mwaka 2014.  Karibuni sana ili tuweze kuujenga Mwili Kristo, “Pamoja na kwa Umoja” kwa njia ya vipawa vyetu au karama zetu ambazo Mungu amembariki kila mmoja wetu. Mtunzi wa Zaburi ya 133, anatukumbusha ujumbe ufuatao: …..Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, Ndugu wakae pamoja, na kwa umoja.  Wapendwa katika Kristo Yesu, Mungu wetu anatupa mwaliko wa kuuanza Mwaka 2014 tukiwa “Pamoja na kwa Umoja” na  Mungu wetu. Mwaka 2014 na uwe mwaka wetu “PAMOJA NA KWA UMOJA.”   AMEN.  

Mch. Ipiana Mwakabonga

No comments: