Advertisements

Thursday, July 24, 2014

Kikwete aagiza ulinzi uimarishwe mpakani Tanzania, Msumbiji

Rais Jakaya Kikwete ameiagiza kamati ya ulinzi na usalama mkoani Ruvuma kuchukua hatua za haraka kuweka ulinzi wa kutosha eneo la Kijiji cha Dar pori, wilayani Nyasa, ambacho kipo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji.

Alitoa agizo hilo jana wakati akizungumza na viongozi mbalimbali kwenye majumuisho ya ziara yake ya siku saba mkoani Ruvuma.

Alisema kijiji hicho chenye wakazi zaidi ya 4,000, ambao wengi wao ni wachimbaji wadogo wa madini aina ya dhahabu hakina ulinzi wa aina yoyote kwenye mpaka wa Tanzania, hali inayosababisha watu kuingia na kutoka nchini kiholela.

Awali, Rais Kikwete alimtaka Brigedia John Chacha wa Kanda ya Kusini kutoa maelezo juu ya mpaka ulivyo wa Tanzania na Msumbiji katika eneo la Dar Pori.

Chacha alikiri kuwa kijiji hicho hakina usalama kwa kuwa watu wamekuwa wakiingia na kutoka bila kuwapo ulinzi mpakani, jambo linalonaweza kuchangia uingiaji wa silaha kiholela.

Rais Kikwete alisema atafanya mazungumzo na Rais wa Msumbiji ili waone namna watakavyoweza kuweka ulinzi, ambao hautaathiri pande zote mbili na kudumisha uhusiano uliopo.
CHANZO: NIPASHE

No comments: