Advertisements

Thursday, July 3, 2014

USILIE, ACHA KUJIUMIZA, MAPENZI HAYATAKIWI KUKUTESA!-3


NINA furaha kukutana nanyi tena hapa katika ukurasa huu ambapo tunajifunza mambo mbalimbali kuhusu maisha ya uhusiano na mapenzi. Bila shaka unapata elimu nzuri inayokusaidia kukuza uhusiano wako.

Uwanja huu ni wa marafiki ambao hata lugha inayotumika hapa ni ya kirafiki zaidi ili kufikisha ujumbe kama ilivyokusudiwa. Kama ni mara yako ya kwanza kufungua ukurasa huu, amini kuwa umeingia kwenye chama sahihi.

Utajifunza kila siku na utavuna mengi uliyoyakosa kwa muda mrefu kabla ya kujiunga nasi. Sasa turejee kwenye somo letu ambalo leo linafikia ukingoni.

Tunajifunza kuhusu mateso katika mapenzi. Nimeshafafanua mengi katika matoleo mawili yaliyotangulia lakini kubwa zaidi ambalo nimesisitiza ni kwamba, mapenzi hayatakiwi kukutesa hata kidogo.

MATESO YA KUJITAKIA

Inaweza kukushangaza kidogo, lakini nakuambia rafiki yangu, wakati mwingine unaweza kusababisha mateso katika maisha yako mwenyewe. Mateso hayo, utayasababisha kwa kufanya mambo ambayo ni kinyume na utaratibu kwa mpenzi wako.

Wapo baadhi ya watu huamua kufanya makosa kwa makusudi wakiamini kwamba hawawezi kuachwa kwa sababu wapenzi wao wanawapenda sana! Huko nakuita ni uvivu wa kufikiri.
Kamwe usiwe mvivu wa kufikiri mambo, unaweza kumfanyia visa leo, ukamtesa na kumnyanyasa, lakini ipo siku moyo wake utachoshwa na mambo yako, utachoshwa na mateso na mwishowe unaweza kuachwa kwenye mataa.

Kama upo katika uhusiano na mpenzi wako ni vyema ukaonesha mapenzi yako, uoneshe jinsi unavyompenda. Jinsi unavyojali ili penzi lenu lizidi kukua siku hadi siku.

Upo mfano wa wazi kabisa wa kijana mmoja ambaye alikuwa na mpenzi wake aliyempenda kwa miaka kumi kwenye mapenzi. Kila wakati mwanamke huyo alikuwa akimfanyia jamaa visa, kila siku visa vinazidi. Leo akifanya hivi, kesho anafanya vile.

Lakini kwa sababu jamaa alikuwa akimpenda sana mpenzi wake alikuwa akimvumilia. Hakuthubutu kumuacha, lakini ilifika wakati akaona hana sababu ya kuendelea kubaki na maumivu, akafanya uamuzi ambao ulimuumiza sana yule mchumba wake. Ulimuumiza kwa sababu haukuwa mzuri.

Ulikuwa uamuzi wa kumuacha. Leo hii analia na kuomba msamaha kila kukicha, lakini jamaa ameendelea kushikilia msimamo wake. Anafanya hivyo si kwa sababu hampendi, bali amechoshwa na maumivu!
Kama ni kweli unahitaji furaha katika maisha yako ya kimapenzi, badilika. Chunguza mapito yako, angalia wapi unapokosea kisha anza upya ili furaha iwe sehemu ya maisha yako.

JIFUNZE KUTOKA KWA MWENZAKO

Si vibaya kuwa mwanafunzi kila siku. Usikubali kuwa mtu wa kulia kila wakati. Ni vyema pia kujifunza kutoka kwa mwenzako.

Angalia anapenda nini na anachukizwa na jambo gani? Kuyajua kutakusaidia sana kukwepa yale mabaya ambayo hayafurahii kisha utafanya mazuri ambayo yatasaidia zaidi kukuza uhusiano wenu.
Mapenzi ni furaha ndugu zangu, hakuna tatizo kuwa mjinga kwa muda ili utengeneze kitu kizuri na kikubwa kwenye uhusiano wako. Kuna sababu gani ya kuishi bila amani?

Kwa nini uumizwe na amani ya wengine? Maana inawezekana wewe na mwenzi wako kila siku ugomvi lakini nyumba ya pili wanaishi kwa amani na upendo.

Unawaona wanapita wakiwa wenye nyuso za furaha siku zote. Hakuna jipya, ni kutengeneza uhusiano wenye nguvu, ushirikiano, kusikilizana na upendo wa dhati.

Huna sababu ya kutoa machozi yako tena kwa ajili ya mapenzi. Mada imeisha, tukutane wiki ijayo kwa mada nyingine, USIKOSE!

Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Saikolojia ya Uhusiano anayeandikia Magazeti ya Global Publishers. Kwa sasa anaandaa kitabu chake kipya cha Maisha ya Ndoa.

GPL

3 comments:

Anonymous said...

Luke Ramadhan hii kaka ::-)))

Anonymous said...

ramadhan kwa wanaofunga si wote na luke yeye pamoja na wengine hawafungi dini yao hajawaamuruu wafunge mwezi huu wa ramadhan.
so jamani nyiyeee tujaribu kuwa wafahamu na wawelewefu.

Na wewe uliyefunga unaugopa ramadhan tu mbona humuogopi Allah aliye fardhisha ramadhan?Tunatakiwa kila siku ya maisha yetu tujitahidi kwa kufanya mema na yenye kumridhia Allah si mwezi wa ramadhan tu pekee.

na kimekupata nini kusoma habari hii kama umefungwa kweli wewe?

funga si kujizuiwa kula na kunywa ni kujizuiya yote maovi na kuyasoma yasiyo mazuri kwa wakati wa fungu ili usibatilishe funga yako.

na hata ukiftari pia saumu bado unayo usidhani kama ndo usiku unaruhusiwa kuyafanya yako na pia ukisherehekea eid siku ya mwanzo siyo ujirushe kwa maovu.Funga ni kheir yetu si wajaa kwa kutaka radhi za Allah.

Tumnyenyeke rahman kwa mema ili atupe fadhila na rehma za mwenzi huu mtukufu na atukubaliye ramadhan zetu.Ameen.

Anonymous said...

mimi mapenzi yananitesa sana nampenda fulani na nadhani anajua ndo maana ananidengulia kwa kweli mpenzi wangu huyu ananitesa sana namuomba mungu sana katika mwezi huu wa ramadhani tuelewana na mpenzi wangu na asinitese.amin