Advertisements

Wednesday, September 17, 2014

UMOJA WA MATAIFA KUJADILI UGONJWA WA EBOLA-BAN KI MOON

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban ki Moon akizungumza na waandishi wa habari ( hawapo pichani) siku ya jumanne ambapo alitumia fursa hiyo kuainisha masuala mbalimbali yatakayopewa kipaumbele wakati wa Mkutano wa 69 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa unaoanza wiki ijayo hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, jijini New York, Marekani. Mlipuko wa Ugonjwa wa Ebola ni moja ya suala litakalopewa kipaumbele cha pekee wakati wa mkutano huo utakaohudhuriwa na wa viongozi zaidi ya 140 wakuu wa nchi na serikali, viongozi wa asasi za kiraia, na wakuu wa mashirika mbalimbaliya Kimataifa.
Na Mwandishi Maalum, New New York.
Viongozi Wakuu wa Nchi na Serikali zaidi ya 140 kutoka mataifa mbalimbali duniani wamethibitisha kuhudhuria na kushiriki majadiliano ya jumla wakati wa Mkutano wa 69 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa unaoanza wiki ijayo

Akizungumza na waandishi wa habari hapo siku ya Jumanne, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, amesema, viongozi hao pamoja na kujadili changamoto mbalimbali zinazoikabili dunia hivi sasa, watautumia mkutano huu kujadiliana kwa kina kuhusu mchango na ushiriki wa jumuiya ya kimataifa katika kuukabili mlipuko wa ugonjwa hatari wa Ebola.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete ni miongoni wa viongozi hao 140 na anaongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huu.

Akizungumzia zaidi kuhusu mlipuko wa ugonjwa hatari wa Ebola na athari zake kwa uhai wa mwanadamu na kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii, Ban ki Moon amewaeleza waandishi hao, kuwa Jumuiya ya kimataifa haiwezi kuendelea kuufumbia macho na kwamba kadiri inavyochelewa kuutafutia ufumbuzi ndivyo hatari yake inavyozidi kuongezeka.

“Tutatoa kipaumbele cha peke kuhusu ugonjwa wa Ebola ambao umeleta athari kubwa kwa baadhi ya nchi za Afrika ya Magharibi na maeneo mengine. Siku mbili zijazo ( Alhamisi) Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa litakutana kwa dharura kuzungumzia mlipuko wa Ebola. Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani Margaret Chan na Mimi tutazungumza katika mkutano huo” akasema Ban Ki Moon

Akaongeza kwa kusema wiki ijayo Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa litakuwa na mkutano wa kilele kuhusu mahitaji ya watu na nchi zilizokabiliwa na ugonjwa wa Ebola.

Pamoja na kujadili na kutafuta mkakati wa pamoja wa kukabiliana na Ebola, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema viongonzi hao wakuu wa nchi na serikali pia wanatarajiwa kujadili na kubadilishana mawazo kuhusu changamoto za mabadiliko ya tabia nchi katika mkutano utakaofanyika septemba 23.

Mhe. Rais Jakaya Kikwete ni kati ya Viongozi walioalikwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhudhuria na kuzungumza katika mkutano huu muhimu kuhusu suala zima la mabadiliko ya tabia nchi na athari zake.

Akielezea zaidi kuhusu mkutano huo wa mabadiliko ya tabianchi, Ban Ki Moon anasema mkutano huo utakuwa na malengo mawili, kwanza ni kukusanya utashi wa kisiasa ili kufikia makubaliano ya pamoja hapo mwakani katika mkutano utakaofanyika huko Paris , Ufaransa. Na pili kuchukua hatua madhubuti za kupunguza uzalishaji wa gesi chafu.

Akiainisha zaidi kuhusu ajenda mbalimbali zitakazojadiliwa wakati wa Mkutano wa Baraza kuu la Umoja wa Mataifa, Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa, amesema, majadiliano ya Baraza Kuu ( General Debate) yatakayoanza septemba 24 yatatumika kukusanya nguvu za pamoja za kuushinda umaskini, na kupitisha ajenda za malengo mapya ya maendeleo endelevu .

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete atalihutubia Baraza Kuu Septemba 25.

Masuala mengine ambayo pia yanatarajiwa kutawala mkutano huo wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwa mujibu wa Ban Ki Moon, ni pamoja na migogoro na machafuko yanayoendelea katika nchi za Syria, Iraq, Libya, Mali, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Ukraine, Sudan ya Kusini ukiwamo pia mgogoro kati ya Palestina na Israel.

No comments: