Advertisements

Thursday, November 27, 2014

Nchi yatikiswa

Dodoma. Hatimaye mtikisiko wa tano umetimia na nchi kutikiswa; ripoti ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) imependekeza kuwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, Mwanasheria Mkuu, Waziri wa Nishati na Madini, naibu wake na katibu mkuu wa wizara hiyo wawajibishwe kutokana na kuhusika kwao kwenye sakata la uchotwaji wa Sh306 bilioni kutoka kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow.
Akaunti hiyo ilifunguliwa kwa ajili ya kutunza fedha za gharama za uwekezaji (capacity charge) baada ya kuibuka mzozo wa kimkataba baina ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na kampuni binafsi ya IPTL ambayo iliingia mkataba wa kufua umeme na kuliuzia nishati hiyo shirika hilo la umma.
Ripoti hiyo ilisomwa jana bungeni kwa kupokezana kati ya Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe na Makamu mwenyekiti, Deo Filikunjombe baada ya majadiliano marefu kwenye vikao vya ndani vya CCM na Kamati ya Uongozi wa Bunge na jitihada kubwa za kutaka isisomwe na kujadiliwa.
Ripoti hiyo ilitokana na ukaguzi uliofanywa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ambayo ilianika ukiukwaji mkubwa wa taratibu wakati wa uchotaji wa fedha hizo pia mahojiano na mkurugenzi mkuu wa Takukuru na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Waziri Pinda ametiwa hatiani na kamati hiyo kutokana na kujua kuwapo kwa ufisadi huo na kauli zake kuwa fedha hizo hazikuwa mali ya umma, wakati Mwanasheria Mkuu Jaji Frederick Werema ameonekana kutoishauri vizuri Serikali na pia kuagiza fedha hizo zitolewe kwenye akaunti hiyo, wakati Waziri Sospeter Muhongo hakuchukua hatua wakati akijua kuwapo kwa sakata hilo, huku naibu wake, Stephen Masele akitiwa hatiani kwa kulidanganya Bunge.
Kamati pia imependekeza uteuzi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakimu Maswi utenguliwe kutokana na kuingia makubaliano ya kutoa fedha bila ya kujiridhisha kikamilifu kuhusu uamuzi wa hukumu ya mahakama ya Kituo cha Kimataifa cha Utatuzi wa Migogoro ya Kiuwekezaji (ICSID).
Iwapo mjadala huo, unaotazamiwa kuendelea leo, utaafiki hatua hizo zichukuliwe, Rais atalazimika kuunda Serikali upya kwa mara ya pili tangu alipofanya hivyo mwaka 2008 wakati wa sakata la Richmond, ambalo lilihusu umeme. Pia atakuwa akifanya mabadiliko ya mawaziri kwa mara ya tano kutokana na wasaidizi hao kujikuta kwenye kashfa.

Kuhusu Pinda
Akiwasilisha ripoti ya kamati hiyo, Makamu Mwenyekiti wa PAC, Filikunjombe alisema katika suala hilo, Pinda anahusika kwa kuwa katika Katiba Ibara ya 52(1) inaeleza kuwa waziri mkuu atakuwa na madaraka ya juu ya udhibiti, usimamiaji, utekelezaji wa siku hata siku wa kazi na shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
Pia ibara ya 52(2) inasema waziri mkuu atakuwa kiongozi wa shughuli za Serikali bungeni. Kutokana na ibara hizo, Filikunjombe alisema baada ya kupitia vielelezo vilivyomo kwenye ripoti ya CAG, kamati imejiridhisha pasipo shaka kwamba Waziri Mkuu alikuwa ana taarifa zote kuhusiana na mchakato mzima wa kuchotwa fedha katika Akaunti ya Escrow.
“Ushahidi uliotolewa na CAG kwenye kamati unaonyesha kuwa waziri mkuu alikuwa akipata taarifa za jambo hili na kamati imesikitishwa kuona kuwa Waziri Mkuu hakuchukua hatua zozote kuzuia muamala huu usifanyike,” alisema Filikunjombe
Alisema: “Kamati inathibitisha bila shaka kwamba waziri mkuu alikuwa analijua jambo hilo vizuri na kwamba aliridhia muamala huo ufanyike na ndiyo maana kauli zake bungeni mara kadhaa alithibitisha kuwa fedha za escrow si mali ya umma.
“Kwa uzito na unyeti wa jambo hili, kwa vyovyote vile Waziri Mkuu anapaswa kuwajibika kwa kauli zake na kwa kutokutekeleza wajibu wake wa kikatiba ipasavyo, ili kurejesha imani ya wananchi kwa Serikali yao na viongozi wao kisiasa,” alisema mbunge huyo wa Ludewa.
Maswi kikaangoni
Kuhusu Maswi, kamati ya PAC imethibitisha kuwa katibu mkuu huyo aliingia makubaliano ya kutoa fedha katika Akaunti ya Tegeta Escrow bila kijiridhisha kikamilifu kuwa maamuzi ya hukumu ya ICSID yalikuwa bado kutolewa na hivyo kusababisha fedha kutolewa bila kukokotoa upya gharama za ‘capacity charges’ jambo ambalo limesababisha kupotea kwa fedha za umma.
“Pia kamati imethibitisha uzembe wa hali ya juu uliofanywa na katibu mkuu huyo, kushindwa kujiridhisha kama masharti ya sheria ya kodi ya mapato sura ya 333 kifungu cha 90(2) yalitekelezwa. Kifungu hicho kimsingi kinaitaka mamlaka ya ‘approval’ ya uhamishaji wa kampuni kutotambua kampuni mpaka kwanza kodi za uhamishaji ziwe zimelipwa na hati za malipo ya kodi zimetolewa na mamlaka ya kodi,” alisema Filikunjombe.
Alisema kutokana na hilo kamati inapendekeza kuwa uteuzi wa katibu mkuu huyo utenguliwe na Takukuru wamfikishe mahakamani mara moja, kwa kukosesha serikali mapato, matumizi mabaya ya ofisi na kusaidia utakatishaji wa fedha haramu.
Kauli zamponza Masele
Kwa upande wa Masele, Filikunjombe alisema kuwa kamati imethibitisha kuwa naibu waziri huyo alisema uongo bungeni kwa kutamka kauli ambazo zilikuwa na lengo la kupotosha umma kuhusu akaunti hiyo ikiwamo kutoa kauli ambazo zingeweza kusababisha nchi kuingia kwenye mgogoro wa kidiplomasia na nchi ya Uingereza.
“Kamati inapendekeza naibu waziri huyo achukuliwe hatua kali za kinidhamu ikiwemo kutenguliwa uteuzi wake. Pia inapendekeza kuwa naibu waziri huyo afikishwe mbele ya kamati ya Bunge ya Maadili ili aadhibiwe kama mbunge kwa kusema uongo bungeni ili iwe fundisho kwa wabunge wengine kuhusiana na kauli wanazotoa ndani ya Bunge,” alisema Filikunjombe.
Muhongo matatani
Akizungumzia kuhusu Muhongo, alisema kamati imethibitisha kuwa waziri huyo amekuwa mara kwa mara akipotosha Bunge na Taifa kwa ujumla kuhusu fedha za akaunti hiyo kwamba ndani ya fedha hizo hakukuwa na fedha za umma.
Alisema kuwa kamati imebaini kuwa waziri huyo, ambaye wakati wote alikuwa akitingisha kichwa kuonyesha kutokubaliana na taarifa ya kamati, ndiye alikuwa dalali mkuu aliyewakutanisha Harbinder Singh Sethi na James Rugemalira tena katika ofisi ya umma na pengine hilo ndilo lilikuwa sababu ya upotoshaji huo.
“Iwapo waziri huyo angetimiza wajibu wake ipasavyo, fedha za Tegeta Escrow zisingelipwa kwa kwa watu wasiohusika na nchi ingeweza kuokoa mabilioni yaliyopotea kama kodi za VAT, Capital Gain Tax na ushuru wa stempu ambazo ni sawa na takribani Sh30 bilioni,” alisema Filikunjombe.
Kutokana na hilo, Filikunjombe alisema kamati inapendekeza kuwa mamlaka yake ya uteuzi itengue uteuzi wake kutokana na sababu hizo.
Werema naye yumo
Kuhusu AG, Filikunjombe alisema kuwa kamati imethibitisha kuwa Jaji Werema alitoa ushauri ulioipotosha Benki Kuu ya Tanzania kuhusu hukumu ya Jaji Utamwa kwa kutumia madaraka yake vibaya, AG aliagiza kodi ya serikali yenye thamani ya Sh21 bilioni isilipwe na hivyo kuikosesha serikali mapato adhimu.
“Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kujua au kwa makusudi alipotosha Bunge na Taifa kwamba mgogoro uliopelekea kufunguliwa kwa Akaunti ya Escrow ulikuwa ni mgogoro wa wanahisa wa IPTL badala ya mgogoro kati ya Tanesco na IPTL,” alisema Filikunjombe.
Alisema kutokana na hilo kamati inapendekeza kuwa uteuzi wa manasheria mkuu wa serikali utenguliwe mara moja na kisha afikishwe mahakamani kwa maumizi mabaya ya ofisi yaliyopelekea serikali kupoteza mabilioni ya fedha.

Baada ya kumaliza kusoma mapendekezo hayo, Spika wa Bunge, Anne Makinda alisema Serikali itatoa majibu leo kabla ya mjadala kuendelea.
MWANANCHI

1 comment:

Anonymous said...

Hawa wote warudishe pesa zetu.na waende jela.