Advertisements

Friday, December 19, 2014

ANAKUPENDA, UNAMPENDA KWA NINI MAPENZI YENU YAWE YA SIRI?


Uhali gani mpenzi msomaji wangu! Ni matumaini yangu kwamba kwa kudra za Mwenyezi Mungu uko poa na unaendelea vyema na majukumu yako ya kila siku.Bila shaka msomaji wangu utakuwa unaelewa vizuri nikizungumzia mapenzi ya siri. Inawezekana umewahi kuwa katika aina hii ya uhusiano, umewahi kusikia au kushuhudia watu wawili wanaopendana, wakiendesha uhusiano wao kwa siri kubwa.

e, kwa nini kuna baadhi ya watu hupenda kuishi kwenye uhusiano wa siri? Hiyo ndiyo mada ambayo ningependa tuijadili leo hapa kwenye busati letu la mahaba.
Najua wapo wengi ambao wapo kwenye uhusiano wa siri na wanazo sababu zinazowafanya waishi kwenye aina hiyo ya uhusiano, lakini je, kama unampenda, na yeye anakupenda kwa dhati, kuna haja gani ya kuishi kwenye uhusiano wa siri?

MAPENZI YA SIRI YANAVYOKUWA
Katika aina hii ya mapenzi, kila kitu wanachokifanya wahusika, kinakuwa kimetawaliwa na usiri wa hali ya juu. Uko naye, siku zinazidi kuyoyoma lakini humfahamu rafiki yake hata mmoja na yeye hamfahamu rafiki yako au ndugu yako hata mmoja.

Hata watu wenu wa karibu wanaowazunguka, hakuna hata mmoja anayejua kwamba nyie ni wapenzi. Mazungumzo yenu mnayafanya kwa siri sana, kukutana kwenu pia kunakuwa ni kwa kuibia sana, tena kwenye maeneo ya vificho.

Hata kama mnafanya kazi ofisi moja, hamuoneshi dalili yoyote ya kuwa wapenzi, hakuna ukaribu kati yenu na kila kitu kinatawaliwa na usiri. Muda pekee mnaokuwa huru, ni pale mnapokuwa peke yenu, yaani wewe na yeye tu.
Hata kama mnataka kutoana ‘out’, mpo radhi msafiri kwa umbali mrefu kwenda sehemu ambayo hakuna anayewafahamu.

DALILI MBAYA
Yawezekana umejikuta tu katika mkumbo wa mapenzi ya siri! Yaani mwenzi wako ndiye anayekulazimisha muishi aina hiyo ya maisha lakini ndani ya moyo wako unaona kama unaidhulumu nafsi yako.

Unatamani kila mtu ajue kwamba ninyi ni wapenzi lakini mwenzi wako anakukataza kufanya hivyo. Pengine hata anakupa vitisho kwamba utakapotoa siri ya uhusiano wenu, huo ndiyo utakuwa mwisho wa mapenzi yenu.

Shtuka! Chunguza kwa kina kwa nini mwenzi wako anataka muishi maisha ya mapenzi ya siri wakati kila siku anakwambia kwamba anakupenda na yupo tayari kufanya chochote kwa ajili yako. Mara nyingi, uhusiano wa siri huwa ni dalili mbaya kwa wahusika! Kwamba lipo jambo ambalo analificha na ndiyo maana anataka muwe wapenzi kwa siri.

Zifuatazo ni baadhi ya sababu zinazofanya mtu apende kuwa na uhusiano wa siri na mwenzi wake.

1. AMEOA/ AMEOLEWA
Sababu kubwa ya kwanza inayowafanya wengi wapende kuwa na uhusiano wa siri na wenzi wao ni kwa sababu wanakuwa wapo kwenye ndoa halali lakini kwa sababu ya tamaa zao, wanaamua kuchepuka. Katika kuchepuka huko, hawawaambii wenzi wapya ukweli kwamba tayari wanao wake au waume zao halali.

Wanawadanganya kwamba wapo singo ili wawatumie kimapenzi na watakapomaliza haja zao ndiyo wawaeleze ukweli na kuvunja mapenzi yao. Upo ushahidi wa wanawake wengi ambao walitongozwa, wakakubali kuanzisha uhusiano wa siri na wanaume na kukaa nao kwa kipindi kirefu lakini baadaye wakaja kugundua kumbe wao ni ‘spea tairi’.

Vilevile wapo wanaume ambao wameingizwa mkenge kwa kuingia kwenye uhusiano wa siri na wanawake, wakiwahudumia na kuwatimizia kila kitu lakini kumbe nyuma ya pazia ni wake za watu.

2. ANA MICHEPUKO MINGI
Sababu nyingine inayosababisha wengi wapende kuishi na wenzi wao kwa usiri, ni tabia ya umalaya au uhuni anayokuwa nayo mtu. Kwamba katika sehemu hiyohiyo moja, wewe unadhani uko peke yako lakini kumbe kuna wenzako kadhaa unapanga nao foleni. Kwa kuwa kila mmoja anatunza siri, inakuwa vigumu kujuana.

Itaendelea wiki ijayo. Kwa maoni, ushauri nicheki kwa namba za hapo juu.

No comments: