ANGALIA LIVE NEWS

Sunday, December 14, 2014

TANZANIA YAISHAURI ICC KUBORESHA UHUSIANO WAKE NA AFRIKA

Balozi Irene Kasyanju, Mkurugenzi wa Idara ya Masuala ya Sheria, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, akizungumza wakati wa Mkutano wa Kumi na Tatu wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai ( ICC). Mkutano huo wa wiki mbili unafanyika hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa.
Sehemu ya wajumbe wa nchi wanachama wa Mkataba wa Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai wakimsikiliza Mwakilishi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mkutano huo, Balozi Irene Kasyanju ambaye katika hotuba yake pamoja na mambo mengine ameishauri Mahakama hiyo kuimarisha uhusiano wake na Afrika.

.
Na Mwandishi Maalum, New York
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  imesema, mafanikio ya  Mahakama ya Kimataifa ya  Makosa ya  Jinai (ICC) yatategemea  uimarishishwaji wa ushirikiano kati ya  Makahama hiyo na Afrika.
Na kwa sababu hiyo, Tanzania imeshauri kuwa Rais Mpya wa Mkutano wa Nchi wanachama wa Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai hana budi kuhakikisha kuwa moja ya vipaumbele vyake vijielekeze katika kuimarisha uhusiano wa  Makahama hiyo na Afrika.
Ushauri huo umetolewa na Balozi Irene Kasyanju,  Mkurugenzi wa Idara ya Masuala ya Sheria, Wizara ya  Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wakati akizungumza katika  mkutano wa kumi na tatu wa  Nchi  wanachama wa Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai.
Amesema Tanzania ina imani kubwa na Rais mpya wa Mkutano wa Nchi wanachama wa Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai, Bw. Sidiki Kaba, kutoka Senegal, kuwa afanye kila awezalo katika kuimarisha uhusiano huo ambao kwa sasa  umezorota.

Vile vile Balozi Kasyanju amesema Rais huyo anashika uongozi katika kipindi ambacho, Mahakama inakabiliwa na  changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na  mwenendo mzima  wa mahakama  na hasa uhusiano wake na  Afrika.
Amebainisha kuwa, changamoto hiyo ya mahusiano na nyinginezo zinahitaji majadiliano ya uwazi yatakayowashirikisha wadau  wote, na kwamba Tanzania inaamini kuwa anao uwezo huo.
Akizungumzia zaidi kuhusu   ushirikiano kati ya Mahakama na Afrika, Tanzania imeeleza kuwa namna ICC ilivyoshughulia shauri la Kenya   hakutafanya mambo yawe shwari, kutokana na ukweli kuwa ICC ilishindwa kulifanyia kazi ombi la awali lililowasilishwa na Afrika mbele ya chombo hicho la kutaka kuahirishwa kwa  shauri hilo kumechangia katika kuongeza malumbano kati ya  ICC na Afrika.
Kwa mantiki hiyo Tanzania imesema uamuzi wa hivi karibuni wa kumwondolea mashtaka Rais  Uhuru Kenyata unapaswa kutoa fursa kwa  mahakama hiyo kujitazama upya.
Vile vile Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetumia fursa hiyo kumpongeza Rais Kenyatta kwa kuonyesha  ushirikiano na  ICC.
Katika hatua nyingine Tanzania pia imeishauri ICC kuangalia namna  itakavyoweza  kufanya kazi kwa karibu na  Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa hasa katika kushughulikia makosa  ya  jinai yanayofanywa na  Nchi ambazo  si wanachama wa  Mkataba wa Mahakama hiyo ili kuondoa dhana ya undumilakuwili katika utendaji wa ICC.
Tanzania imeujulisha mkutano huu kwamba ipo  katika hatua yake ya awali ya kuziingiza sheria zitokanazo na Mkataba wa ICC katika mfumo wa Kisheria wa Nchi.

Balozi Kasyanju anaongoza Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huo wa wiki mbili unaohusisha pia uchaguzi wa majaji  sita wa mahakama hiyo. 

No comments: