Advertisements

Wednesday, March 4, 2015

Wananchi wamsaidia Nape ujumbe kwa Nyerere


Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye (wa pili kulia) akishirikiana na wanamuziki wa nyimbo za dansi kuimba wimbo maalumu wa kumuaga marehemu John Komba katika Viwanja vya Karimjee juzi. Picha na Venance Nestory

Dar/Mikoani. Wakati wa kumuaga John Komba, ambaye alikuwa mpiga kampeni mashuhuri wa CCM, kada wa chama hicho, Nape Nnauye aliimba “Neenda baba… msalimie Mwalimu (Julius Nyerere), mweleze hali ya Watanzania ilivyo hivi sasa, mweleze hali ya nchi yetu ilivyo wakati huu,” bila ya kutaja ikoje, lakini wananchi walioongea na gazeti hili wamemalizia wimbo huo; wanaona hali ya nchi ni mbaya.
Nape, katibu wa itikadi na uenezi na mtoto wa kada maarufu wa CCM, Marehemu Moses Nnauye aliyetunga nyimbo nyingi za uhamasishaji, aliungana na wasanii wa muziki wa dansi kuimba wimbo huo uliotungwa na Komba wakati wa kifo cha Julius Nyerere, ambaye ni mwasisi wa Taifa la Tanzania kwenye Viwanja vya Karimjee juzi.
Katibu huyo wa Itikadi na Uenezi wa CCM aliongoza kuimba sehemu ya wimbo huo yenye maishairi yasemayo “Kapteni Komba, familia yako umeiacha na nani, chama chako umekiacha na nani. Nenda baba, msalimie Mwalimu, mweleze hali ya Watanzania ilivyo hivi sasa, mweleze hali ya nchi yetu ilivyo hivi sasa hasa wakati huu, msalimie Mzee Kawawa Simba wa Vita”.
Baada ya kuimba sehemu hiyo ya wimbo huo uliotungwa na Komba mwaka 1999 wakati kifo cha Mwalimu Nyerere na ambao umebadilishwa maneno na kupewa jina la “Nani Yule”, waombolezaji mbalimbali walionekana kuguswa hisia zao.
Wakati Nape akiwa amerudi nyuma na kuinamisha kichwa chini, Rais Jakaya Kikwete, Rais wa Serikali ya Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi, Spika Anne Makinda, wabunge na viongozi wengine walionekana kububujikwa na machozi.
 Wengi waliohojiwa walielezea kuwa nchi imejaa maovu yanayofanywa na watu wenye dhamana, mamlaka na nyadhifa katika taifa, wakitaja ufisadi, rushwa, ubinafsi, ubadhirifu na hata hali ya kisiasa kuwa mbaya na hivyo hayo ndiyo angeelezwa Mwalimu Nyerere, ambaye aliongoza harakati za uhuru wa Tanganyika na anasifika kwa kupinga maovu hayo kwenye jamii.
“Kwa mtazamo wangu, kama Komba akikutana na Nyerere ningependa amwambie kwamba, Tanzania ya leo inanuka rushwa viongozi wa Serikali hawana maadili, bora angekuwepo yeye,” alisema Gervas Mbaya, mkazi wa Nyegezi wilayani Nyamagana, Mwanza.
Imani Hezron, Mkazi wa Nyakato alisema: “Amwambie Mzee Nyerere kwamba alipoondoka aliacha kilimo kama uti wa mgongo wa taifa, leo si hivyo tena, na taifa halipigani vita kuondoa umasikini ujinga wala maradhi.”
Mkazi mwingine anayeishi Chuo Kikuu cha St Augustine cha Mwanza, Sarah Onesimo, alisema: “Ningependa amwambie Mwalimu Nyerere kuwa Tanzania imechafuka kwa mauaji ya albino... mauaji yanazidi kuongezeka, huku jitihada ya kudhibiti hazionekani na kama angejaliwa kuwepo, pengine yote haya yasingetokea.”
MWANANCHI

No comments: