Advertisements

Monday, May 4, 2015

CUF wawapania CCM Ruangwa.

Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa CUF, Abdul Kambaya.

Wananchi wa Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi, wamechoshwa na uongo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wamedai kuwa miaka 53 ya uhuru wameshindwa kuwajengea barabara kuu ya wilaya hiyo kwa kiwango cha lami na fimbo watakayotumia ni kukiadhibu ni kukinyima kura Oktoba, mwaka huu.

Wakizungumza katika mikutao ya hadhara ya Chama cha Wananchi (CUF) katika maeneo mbalimbali ikiwamo Kata ya Nandagala, kuhamasisha wanachama na wananchi kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapigakura wananchi wa kata hiyo walisema wamechoshwa na uongo wa CCM na hivi sasa propaganda za chama hicho hazina nafasi tena.

Walisema kwa miaka 53 barabara kuu inayounganisha wilaya ya Ruangwa na wilaya zingine imeshindikana kujengwa na kila uchaguzi unapokaribia wanadanganywa kuwa itajengwa kwa kiwango cha lami, lakini baada ya hapo hakuna kinachofanyika.

Mambo mengine ambayo ni kero ni kata ya Nandagala kukosa hospitali ya kata, shule ya kata, maji safi, huku zao la korosho kila mwaka likiendelea kunufaisha wachahe na wao wakiendelea kuwa masikini.

Mkazi wa kata hiyo, Asia Mohamed, alisema kila uchaguzi mkuu unapofika CCM wanatoa ahadi za uongo na kwamba mwaka huu wasipoteze muda kwa kuwa hakuna mtu wa kuwasikiliza bali ni kutowachagua.

Saidi Mkopwa wa kata ya Nandagala A, alisema kata hiyo haina kituo cha afya na wananchi wanalazimika kutembea umbali mrefu kufuata kutafuta huduma, hali inayowawia vigumu wajawazito kupata huduma ya kujifungua na wengi huzalia majumbani.

Alina Issa alisema wameamua kubadilika baada ya kuona serikali ya CCM imeshindwa kuwajengea shule ya kata hali inayochangia watoto wao kusoma mbali na wengine kuacha shule kutokana na umbali mrefu.

Pia alisema serikali ya CCM imekuwa ikiwaahidi kuwapelekea maji safi na salama, lakini hakuna kilichofanyika.

Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa CUF aliyeongoza ujumbe wa viongozi wa chama hicho Taifa katika ziara hiyo, Abdul Kambaya (pichani), akizungumza katika mkutano huo wa hadhara, alisema CCM wataadhibiwa kwa mambo mawili ambayo ni wananchi kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapigakura pamoja na kujitokeza kwa wingi kupiga kura ya kuchagua rais, mbunge na diwani muda utakapofika.

Aliwataka wananchi wa wilaya ya Ruangwa kutambua kuwa siasa ndiyo inayopanga maisha yao na kuwashauri kutumia haki yao ya kikatiba kuiadhibu CCM na kuongeza kuwa haiwezekani miaka 53 ya uhuru wilaya ya hiyo haina hata kilomita tano ya barabara iliyojengwa kwa kiwango cha lami.

Mwenyekiti wa Vijana wa chama hicho Taifa, Abuu Bobali na Katibu wa Jumuiya ya Wanawake wa chama hicho, Fatuma Kalembo walisisitiza kwamba watoto wadogo kunyiwa elimu ni kutegeneza Taifa la watu maskini na tegemezi, hivyo ni wakati mwafaka kufanya maamuzi kwa kujiandikisha kwa wingi katika daftari la kudumu la wapigakura na muda ukifika wafanye maamuzi.
CHANZO: NIPASHE

No comments: