Advertisements

Wednesday, May 27, 2015

RAIS KIKWETE ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWA MSIBA WA MTANGAZAJI WA ZAMANI WA RADIO TANZANIA MSHINDO MKEYENGE

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ametuma salamu za rambirambi kuomboleza kifo cha aliyekuwa mtangazaji mashuhuri na maarufu wa iliyokuwa Redio Tanzania (sasa TBC Taifa), Ndugu Mshindo Mukeyenge ambaye alifariki dunia mwishoni mwa wiki na kuzikwa jana, Jumatatu, Mei 25, 2015.

Katika salamu alizomtumia Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Mkoa wa Dar Es Salaam, Mheshimiwa Sofia Mjema jana, Jumanne, Mei 26, 2015, Rais Kikwete amesema kuwa kifo cha Mzee Mukeyenge kimelinyang’anya “taifa letu hakina kubwa ya uzoefu wa utangazaji katika kipindi ambapo vijana wanaochipukia katika tasnia ya habari, na hasa utangazaji, walikuwa wanahitaji sana malezi, ushauri na uongozi wake.”

Rais Kikwete amemwelezea Mzee Mukeyenge kama Mtanzania aliyetoa mchango mkubwa katika ujenzi wa taifa letu kupitia kipaji chake cha utangazaji na kuwa mchango wake utaendelea kukumbukwa kwa miaka mingi ijayo.

“Aidha, tutaendelea kumkumbuka Ndugu Mshindo Mukeyenge kwa mchango wake mkubwa katika maendeleo ya michezo hapa nchini, na hasa mchezo wa soka, ambako alichangia kwa kulihabarisha taifa letu kupitia utangazaji wa mechi nyingi za soka za kitaifa ama kimataifa,” amesema Rais Kikwete.

Amemwambia Mkuu huyo wa Wilaya, “Kwa hakika nimepokea kwa huzuni taarifa za kifo cha Ndugu Mshindo Mukeyenge. Napenda kuungana nawe na wana-Temeke wote katika kuomboleza kifo cha mwenzetu. Aidha, napenda kukuomba unifikishie salamu zangu za rambirambi kwa wanafamilia na wote ambao wamepotelewa na mhimili wao. Wajulishe kuwa naungana nao katika machungu yao na katika kumwomba Mwenyezi Mungu aiweke pema peponi roho ya Marehemu Mshindo Mukeyenge. Amina”.

Imetolewa na;

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.
26 Mei, 2015

No comments: