Advertisements

Saturday, August 29, 2015

MKATABA KUHUSU MAHITAJI NA MATARAJIO YA WAZEE TANZANIA KUTOKA KATIKA SERIKALI YA AWAMU YA TANO 2015

UTANGULIZI

KWAMBA, sisi wazee wa Tanzania ambao tumewakilisha wazee wenzetu, kutoka mikoa yote nchini, tuliokutana kuanzia tarehe 24 hadi 26 Juni 2015, hapa Dar es Salaam tumechangia mawazo yetu katika kuandaa Mkataba huu na kuuridhia. Lengo la Mkataba huu ni kutambulisha umma wa Watanzania haki zetu, mahitaji yetu na changamoto tunazokumbana nazo ili ziweze kupatiwa ufumbuzi.
KWAMBA, Mkataba huu ni nyenzo ya kuhakikisha kuwa wagombea wote katika nafasi mbalimbali za uongozi na Serikali kwa ujumla wanatambua mahitaji yetu na hivyo kuchukua hatua stahiki.
NA KWAMBA, sisi wazee tumetumikia Taifa hili katika sekta mbalimbali zilizo rasmi na zisizo rasmi. Na tumekuwa chimbuko na mhimili wa Taifa letu. Aidha, tumetoka jasho jingi katika kulifikisha Taifa letu hapa lilipo na bado tunaendelea kutoa mchango wetu. Tulijinyima sana ili kuhakikisha kuwa vijana wetu wanapata elimu na afya bora ili kujenga kizazi kitakachoweza kuliendeleza Taifa hili; na  sasa tumekuwa wazee.
NA KWAMBA, pamoja na hayo, sasa tumekuwa waathirika wakubwa. Wenzetu wanauawa kikatili kwa imani potofu za kishirikina. Tunaathirika kwa maradhi na kufa kutokana na kukosa matibabu ya uhakika, vipato vya kumudu gharama za maisha. Hatuna uwakilishi katika vyombo vya maamuzi na hivyo kilio chetu hakisikiki. Haki na mahitaji ya wazee  hayapewi kipaumbele kutokana na kutokuwepo mfumo wowote wa kutoa Pensheni jamii kwa wazee wote na pia  kukosekana kwa sheria ya wazee.
NA KWA KUZINGATIA HAYO,
sasa wazee tunahitaji kulindwa na kuheshimiwa. Tunahitaji kuwekewa mazingira bora yatakayotufanya tuishi katika utu, usawa na haki na kupata mahitaji ya msingi kutoka jamii na mamlaka za serikali.Kupitia Mkataba huu, tunahitaji viongozi watambue umuhimu wa wazee na hivyo kutoa matamko na kuchukua hatua za kulinda haki za wazee kama zilivyotamkwa katika Mkataba huu ambazo pia zinatambulika katika Tamko la Umoja wa Mataifa Kuhusu Haki za Wazee (Na. 46 ya 1991) na mikataba mingine ya Kimataifa na Kikanda.



SEHEMU YA KWANZA:
HAKI ZA WAZEE
A.   Haki za Wazee
1.   Haki ya Usawa
·         Haki ya kutobaguliwa.
·         Haki ya usalama.
·         Haki ya kuishi maisha bora yenye utu.
·         Haki ya kupata taarifa zote muhimu, zikiwemo zile zinazohusu wazee na kuelimishwa.
·         Uhuru wa mtu kwenda atakapo.
2.   Haki ya Kuheshimiwa
·         Haki ya kupata heshima na kuthaminiwa na watumishi wa umma pamoja na watu wanaohudumia wazee.
·         Haki ya kushiriki katika shughuli za kijamii kwa hiari.

B.   Haki Kuhusu Huduma, Usalama na Uwakilishi wa Wazee
1.   Huduma Muhimu kwa Wazee
·         Haki ya kupata pensheni.
·         Haki ya kupata huduma za afya na matibabu bila malipo.
·         Haki ya kuhudumiwa na wahudumu wa afya ambao wamepata mafunzo maalum kuhusu afya ya wazee.
·         Haki ya kupata huduma na usaidizi kutokana na mahitaji maalum.
·         Haki ya kupata mikopo nafuu.
·         Haki ya kupata usafiri wa umma bila malipo.
·         Haki ya kufanya kazi na hivyo kupata kipato.
·         Haki ya kupata uangalizi na matunzo nyumbani ikiwa mzee hana uwezo wa kufuata huduma.
·         Haki ya kupata huduma za kisheria bila kulipa au kwa gharama ya Serikali.
2.   Ulinzi na Usalama
·         Haki ya ulinzi dhidi ya vitendo vya kubaguliwa, kupuuzwa, kunyanyaswa, kuumizwa au kuuawa.
·         Haki ya kulindwa dhidi ya  kunyang’anywa mali kama ardhi, nyumba na mali nyingine isipokuwa tu kwa mujibu wa sheria.
·         Haki ya kuishi katika mazingira ambayo ni salama.


3.   Uwakilishi na ushiriki
·         Haki ya kushiriki katika vyombo vya maamuzi katika ngazi zote kupitia uwakilishi wa wazee.
·         Haki ya kushirikishwa na kutoa maoni kuhusiana na utengenezaji na mabadiliko ya sera na sheria zinazogusa wazee.
·         Haki ya kuanzisha mabaraza maalum ya wazee.


SEHEMU YA PILI:
MASUALA MUHIMU NA HATUA ZA KUCHUKUA

Kama ishara ya kuheshimu na kulinda haki za wazee na kuhakikisha kuwa haki hizo zinatekelezwa, sisi Wazee tunahitaji vyama vya siasa na wagombea wa nafasi za kisiasa katika ngazi zote kuweka katika ilani zao za uchaguzi masuala yaliyotajwa katika Mkataba huu na kuchukua hatua stahiki kutegemeana na nafasi wanazogombea na pindi watakapochaguliwa kuhakikisha kuwa masuala haya yanatekelezwa.

1.   Pensheni Jamii kwa wazee
·         Kutoa tamko kwamba Serikali ina wajibu wa kutunza na kulinda wazee ikiwa ni pamoja na wajibu wa kuwapa Pensheni Jamii (Social Pension) kutambua mchango wao katika Taifa.
·         Kwamba wazee wote kuanzia miaka 60+ wataandikishwa ili kupanga mikakati ya kuwahudumia.
·         Kupanga bajeti ambayo inajumuisha pensheni jamii kwa wazee wote.
·         Kutoa tamko kuhusu kuanza pensheni jamii kwa wazee kuanzia Novemba 2015.


2.   Huduma ya Afya
·         Ziwepo takwimu sahihi za wazee za kiafya zilizochambuliwa.
·         Itengwe fedha ya kutosha katika bajeti kitaifa na katika halmashauri kwa ajili ya kutoa huduma kwa wazee.
·         Kuwe na kasma ya masuala ya wazee.
·         Kuwe na Bima ya Afya kwa wazee na kupata dawa na tiba zote bila malipo.
·         Halmashauri zote kuhakikisha fedha za kuwalipia wazee kwenye CHF zinatengwa.
·         Kuwepo na dawa kwa ajili ya kutibu magonjwa yanayoathiri wazee na kuingiza dawa hizo katika orodha ya dawa muhimu.
·         Ihakikishwe kuwa wazee wote nchini watapata huduma za afya kupitia vyumba maalum katika vituo vyote vya afya na hospitali za umma na uwepo wa kitengo maalum cha wazee na wodi za wazee katika vituo vya afya. 
·         Ihakikishwe kuwa hospitali zinazopata ruzuku ya Serikali zinatoa matibabu bila malipo kwa wazee kulingana na makubaliano na Serikali.
·         Ihakikishwe kuwepo vifaa tiba vya kupima magonjwa yanayoathiri wazee.
·         Kuwepo kwa huduma za mikoba (outreach services) kwa wazee walioko mbali na taasisi za kiafya ili kupata huduma.
·         Itolewe elimu kwa wazee kuhusu Ukimwi na magonjwa mengine mtambuka na namna ya kuwahudumia walioathirika.
·         Yatolewe mafunzo kwa watumishi wote wa afya kuhusu haki za wazee na jinsi ya kuhudumia wazee.
·         Kuwepo wataalam wa afya wenye ujuzi katika kutoa huduma kwa wazee.
·         Kuwepo uwakilishi wa wazee katika kamati za kata na bodi za afya za wilaya na mikoa.
·         Kusimamia matumizi bora ya rasilimali na ukusanyaji wa mapato na kuweka utaratibu wa kupata dawa katika maduka ya dawa binafsi ikiwa hakuna dawa katika hospitali za umma.


3.   Sheria ya Wazee
·         Ihakikishwe  kwamba  Sheria ya Wazee (Bara na Zanzibar)  inaandaliwa na kufikishwa Bungeni/Baraza la Wawakilishi.
·         Serikali ya Tanzania ishiriki kikamilifu katika jitihada za kimataifa za kuwa na Mkataba wa Haki za wazee.



4.   Mauaji ya Wazee
·         Mada kuhusu uzee na kuzeeka na haki za wazee ziingizwe katika mitaala ya shule.
·         Jeshi la Polisi lisimamiwe kikamilifu kutimiza wajibu wake katika kulinda wazee dhidi ya vitendo vya unyanyasaji, ukatili na mauaji ya wazee kwa kisingizio cha ushirikina.
·         Halmashauri zote zielekezwe kutimiza wajibu wao kwa mujibu wa Sera ya wazee na miongozo mingine ya serikali juu ya usalama wa raia na makundi maalumu na waagizwe kutunga sheria ndogondogo za utekelezaji wa maagizo hayo.
·         Idara ya Ustawi wa Jamii iaigizwe kuelimisha jamii juu ya athari za imani potofu za ushirikina na suala zima la matunzo ya wazee.
·         Itungwe sheria mahususi ya kulinda haki za wazee.
·         Vijana wawezeshwe kujikwamua kiuchumi ili kuepuka kuwaua wazee kwa nia ya kupata mali.

5.   Uwakilishi na Ushiriki wa wazee
·         Kuwepo na ushiriki wa wazee katika ngazi zote za maamuzi (WDC, Halmashauri na Bunge).
·         Kuhakikisha kwamba mabaraza ya wazee yanaanzishwa au kuimarishwa kuanzia ngazi ya kijiji/mtaa hadi Taifa na kuyatambua kisheria ili kuwapa wazee sauti na fursa ya kuchangia mawazo katika ujenzi wa Taifa.
·         Serikali katika ngazi zote ishirikiane na wazee na kusilikiza mawazo yao kupitia mabaraza ya wazee. Mfano, viongozi wakitaka kukutana na wazee wafanye hivyo kupitia mabaraza haya.
·         Kuwepo na wizara/idara maalum itakayokuwa na wajibu wa kushughulikia masuala ya wazee.


6.   Kipato duni
·         Halmashauri zote ziagizwe kuwa na takwimu sahihi zinazohusu mahitaji mbalimbali ya wazee. Mfano, kutambua wazee wanaotunza yatima na watu walioathirika na VVU/UKIMWI.
·         Kuanzisha mfuko wa wazee kwa ajili ya kugharamia huduma mbalimbali za wazee.
·         Huduma za usafiri wa umma zitolewe bila malipo.
·         kutoa mafunzo kwa wafanyakazi wanaokaribia kustaafu kuhusu njia za kukabiliana na matokeo ya kustaafu.
·         kutoa mafunzo ya ujasiriamali kwa wazee na kutoa mikopo nafuu kwa wazee wanazoweza kufanya kazi.
·         Taasisi za fedha ziagizwe kutoa mikopo yenye  masharti nafuu kwa wazee.
·         Kukomesha utaratibu wa baadhi halmashauri kuendelea kutoza kodi ya majengo  ya makazi kinyume cha Waraka wa Serikali.
·         Wazee wasamehewe kulipa tozo na michango mbalimbali kama vile ya shule, mwenge, maabara n.k.

7.   Msaada wa Kisheria
·         Wazee wapatiwe msaada wa kisheria kwa gharama za Serikali ili kulinda haki zao.

8.   Vitambulisho kwa wazee
·         Ihakikishwe kuwa halmashauri zote zinatambua wazee na kuwapatia vitambulisho ambavyo vitatumika kupata huduma mbalimbali kama vile matibabu bila malipo, usafiri wa umma bila malipo na pensheni jamii mahali popote nchini.



Imepitishwa na wawakilishi wa wazee kutoka mikoa yote nchini walioshiriki katika Mkutano uliofanyika kuanzia tarehe 24 hadi 26 Juni, 2015 Blue Pearl Hotel, Dar es Salaam






2 comments:

mandenda said...

wewe ccm nini mbona huna coverage ya ukawa yakutosha

mandenda said...

wewe ccm nini mbona huna coverage ya ukawa yakutosha