Advertisements

Friday, October 2, 2015

Polisi wakanusha karatasi za kura kukamatwa Masasi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, Henry Mwaibambe.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara limekanusha taarifa zinazodaiwa kuandikwa katika mtandao mmoja wa kijamii, zikidai kukamatwa kwa baadhi ya watu katika kituo cha polisi wilaya ya Masasi mkoani hapa wakiwa na masanduku na fomu za kupigia kura zipatazo 2000 zikiwa tayari zimetumika.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, Henry Mwaibambe, alisema taarifa hizo zilidai kuwa, fomu hizo zilimpa alama ya vema mgombea urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli na mgombea ubunge wa jimbo la Masasi kupitia chama hicho.

Alisema taarifa hiyo iliendelea kudai kuwa, mkuu wa wilaya ya Masasi aliingilia kati na watuhumiwa hao ambao hawakutajwa majina waliachiwa huru kwa dhamana kwa amri ya mkuu huyo wa wilaya ambaye ndiye aliewadhamini na kwamba masanduku hayo na karatasi yamehifadhiwa katika kituo cha polisi wilayani humo.
Kamanda Mwaibambe alisema taarifa hiyo ni uzushi na upotoshaji mkubwa na kwamba hakuna mtuhumiwa wala masanduku yaliyokamatwa mkoani hapa wala katika wilaya hiyo.

“Tunachofahamu kupitia kwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (Nec), vifaa vya kupigia kura bado havijawasili nchini na alituahidi vitaanza kuwasili mwishoni mwa mwezi huu kutoka nchini Afrika Kusini.” alisema.

Alisema Jeshi la Polisi linamsaka mhalifu huyo wa mtandaoni na akitiwa mbaroni atafikishwa katika vyombo vya sheria.
CHANZO: NIPASHE

No comments: