Sunday, December 6, 2015

MWASHIUYA ACHACHAMAA KUPELEKWA YANGA B, ASEMA WAKIMWAGA MBOGA, ANAMWAGA UGALI

Winga wa Yanga Geofrey Mwashiuya ameibuka na kuzungumzia suala ya yeye kushushwa hadi kikosi B cha mabingwa hao watetezi wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara (VPL).
Siku chache zilizopita baadhi ya vyombo vya habari pamoja na mitando ya kijamii viliripoti kuwa kinda huyo ametupwa kikosi B kutokana na uwezo wake kushuka hivyo amepelekwa huko ili akatengeneze makali yake upya.
Mtandao huu haukusita kumtafuta kijana huyo wa Mbeya aliyesajiliwa kutoka klabu ya Kimondo FC inayoshiriki ligi daraja la kwanza na kupiga nae story kutaka kujua ‘mbivu na mbichi’ juu ya sakata hilo.

Mwashiuya amesema ameshangazwa na taarifa hizo ambazo amesema si za kweli kwasababu hajapewa taarifa yoyote na mwalimu wala uongozi wa timu yake kama ameshushwa hadi Yanga B.

“Hata mwalimu amekasirishwa na kushangazwa na taarifa hizo, kilichotokea ni kwamba, wachezaji wengi walikuwa kwenye timu za taifa na wachezaji wa kikosi cha kwanza tuliobaki tulikuwa wachache alichokifanya mwalimu ni kuwachukua baadhi ya wachezaji wa kikosi B ili kuongeza idadi ya wachezaji tujumuike pamoja kufanya mazoezi”, alisema winga huyo ambaye alipewa jina la Lunyamila Jr.

“Wakati wa mazoezi mimi nikawa upande wa wachezaji wa kikosi B nadhani watu wakajua kwamba yale mazoezi yalikuwa ni kati ya kikosi cha kwanza dhidi ya kikosi B, na kwa vile mimi nilikuwa upande wa kikosi B basi nimeshushwa kutoka kikosi cha kwanza”.

“Ni bora niende hata kwenye timu yangu ya Kimondo nikapikwe tena upya kuliko kushuhwa hadi kikosi B, wote wanaonibeza ipo siku wataniheshimu”.

No comments: