Saturday, December 5, 2015

Wafanyakazi Tanesco, Wachina kizimbani kwa tuhuma za ufisadi

By Phinias Bashaya,Mwananchi

Bukoba.Wafanyakazi wawili wa Tanesco na raia wawili wa China wamefikishwa katika mahakama ya hakimu mkazi mkoa wa Kagera kwa tuhuma za kutenda makosa kumi na sita na kusababisha hasara ya zaidi ya shilingi bilioni moja.

Watuhumiwa kutoka Tanesco Isaack Tibita na Olver Mushumbusi kwa nyakati tofauti walikuwa mameneja Wilayani Karagwe wanadaiwa kushirikiana na wafanyakazi wa kampuni ya ujenzi wa barabara ya Chico kufanya udanganyifu na kujipatia fedha hizo.

Raia wa China katika kesi hiyo ni Wang Lei na Zhang Shuaitong ambao kwa pamoja wanadaiwa kutenda makosa 16 wakati wa kuhamisha miundombinu ya umeme zikiwemo nguzo ili kupisha ujenzi wa barabara ya lami ya Kyaka,Bugene.

Katika kesi hiyo namba 65 ya mwaka 2015 Wakili Mfawidhi kutoka ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Hashimu Ngole alisema watuhumiwa kati ya mwaka 2011 na 2014 kwa nyakati tofauti walitenda makosa hayo na kusababisha hasara ya kiasi hicho cha fedha.

Miongoni mwa makosa waliyosomewa washitakiwa ni kughushi nyaraka zikiwemo hundi za malipo zinazonyesha kuwa kampuni ya Chico imelipwa fedha kupitia mradi wa ujenzi wa barabara ya lami ya Kyaka Bugene.

Mtuhumiwa wa tatu ambaye ni raia wa China Wang Lei alikuwa meneja wa mradi huo na alisomewa mashitaka mawili peke yake huku mtuhumiwa wa nne Zhang Shuaitong akifanya tafsili kutokana na raia mwenzake kufahamu lugha ya Kichina pekee.

Pia wafanyakazi hao wa Tanesco miongoni mwa mashitaka mengine yanayowakabili ni kughushi nyaraka zilizoonyesha kuwa shirika hilo lilikuwa linadai kulipwa na kampuni ya Chico na kuwa kwa nyakati tofauti walipokea fedha kutokana na nyadhifa zao.

Watuhumiwa wote walikosa dhamana baada ya hakimu Charles Uiso kusema kuwa hakimu anayehusika na kesi hiyo alikuwa na majukumu mengine na itatajwa tena Desemba 7,na kupewa masharti ya dhamana.

No comments: