Sunday, January 17, 2016

SERIKALI YALIFUTA GAZETI LA MAWIO

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, leo wakati akitangaza kufutwa kwa gazeti la Mawio. (Picha na Habari Mseto Blog)

DAR ES SALAAM, TANZANIA
 Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeamua kulifuta kutoka katika Daftari la usajili wa magazeti, gazeti lijulikanalo kama “MAWIO”. Amri ya kulifuta Gazeti hilo imetolewa kwa Tangazo la Serikali Na. 55 lililotolewa tarehe 15 Januari, 2016. Uamuzi huo umetolewa kwa mjibu wa Sheria ya Magazeti Sura ya 229, kifungu 25(1).
Hatua hii pia inazuia gazeti la Mawio kuchapishwa katika njia nyingine yoyote ikiwa ni pamoja na mitandao (Online publication) kwa mujibu wa Sheria ya Mawasiliano ya Kieletroniki na Posta Sura ya 306.
Serikali kwa masikitiko makubwa, imechukua uamuzi huu kutokana na mwenendo wa uandishi wa gazeti hilo usioridhisha wa kuandika na kuchapisha habari zenye mwelekeo wa uchochezi na kuhatarisha amani, utulivu na usalama wa nchi yetu.
Aidha, hatua hii ya kulifuta gazeti hilo imechukuliwa baada ya Msajili wa Magazeti kufanya juhudi kubwa za muda mrefu kuanzia Juni, 2013 hadi Januari,  2016  kumtaka Mhariri wa gazeti hilo kubadili aina ya uandishi wa habari na makala katika gazeti lake, bila mafanikio.
Msajili wa magazeti kwa juhudi zake alifanya mawasiliano na mhariri wa gazeti hilo mara nane kwa lengo la kutaka afanye marekebisho ya  mtindo wa kutoa habari zake lakini mhariri wa gazeti hilo hakuzingatia ushauri mzuri aliopewa na Msajili wa Magazeti.
Ninatoa wito kwa wamiliki, wahariri, waandishi na watangazaji wa habari kuzingatia sheria, Kanuni na taratibu za taaluma ya uandishi wa habari ambazo zikizingatiwa hakutakuwa na migogoro yoyote. Aidha Serikali inasisitiza kwamba inaheshimu uhuru wa vyombo vya habari unaozingatia maadili, weledi na Sheria za nchi na kwamba Serikali itaendelea kushirikiana navyo.
Kwa upande mwingine ninatoa pongezi kwa vyombo vyote vya habari nchini vinavyozingatia maadili, weledi na Sheria zinazosimamia taaluma ya habari na sheria nyingine za nchi.  Kwa namna ya pekee Serikali inawapongeza wamiliki na wahariri wa vyombo vya habari ambavyo vinapofanya makosa vikielekezwa hujirekebisha na kutoa ushirikiano kwa Serikali na pia kubadili mwenendo wao; hawa ni pamoja  na wahariri wa magazeti ya; 

·        Mwananchi Tanzania
·        Mtanzania
·        The East African
·        Magazeti ya Daily News na Habari Leo
·        Uhuru na mengineyo

Ninapenda  kusisitiza kwamba Serikali inapenda kujenga uhusiano mzuri na wa kirafiki kati yake na wadau wa sekta ya habari. Aidha ninasisitiza tena wadau wa sekta hii kuzingatia Sheria ili kujenga heshima ya tasnia ya habari na kulinda amani ya nchi yetu.


Imetolewa na Nape M. Nnauye(Mb,)
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Dar es Salaam, leo tarehe 17 Januari, 2016

1 comment:

Anonymous said...

Yaani wakiandija habari inayogusa mambo wanayoyafanya. Gazeti linafungiwa! Jifunzeni kujirejebisha mnapoambiwa mmekisea na sio kufungua magazeti hilo sio suruhisho la tatizo. Mungu ibariki Tanzania.