Monday, January 4, 2016

WAAMUZI WANUSURIKA KUCHEZEA KICHAPO MAPINDUZI CUP


Waam,uzi wa mchezo wa Azam FC vs Mibwa Sugar wakitolewa uwanjani chini ya ulinzi mkali wa jeshi la Polisi

Zanzibar
Goli lililokataliwa na mwamuzi aliyechezesha mchezo wa pili wa Azam FC vs Mtibwa Sugar lilizua kizazaa kwa waamuzi hao ambapo walilazimika kutolewa chini ya ulinzi mkali wa polisi ili kuzuia waamuzi hao wasichezee kichapo kutoka kwa wachezaji na mashabiki waliokuwa wakiishangilia Mtibwa Sugar.
Mohamed Kichuya alipachika mpira wavuni kuiandikia Mtibwa bao la pili lakini mshika kibendera (line one) aliinua juu kibendera chake kuashiria mchezaji huyo alikuwa ameotea kabla ya kufunga goli hilo. Baada ya goli hilo kukataliwa, wachezaji wa Mtibwa walimfuata mshika kibendera huyo na kumzonga lakini baadaye walikubali kuendelea na mchezo.

Dakika chache baadaye mwamuzi wa kati akamaliza mchezo na hapo ndipo likazuka ‘timbwili’ kama siyo ‘mbilinge’ kwani wachezaji wa Mtibwa Sugar walimfuata mwamuzi na kuanza kumtia ‘kashkash’ kwanini alikataa goli lao ambalo lingewapa ushindi. Lakini si wachezaji tu, benchi la ufundi pia uzalendo uliwashinda nao wakaanza kuwaandama waamuzi wa mchezo huo.

Jeshi la polisi kuona mzozo umekuwa mkubwa na waamuzi hao wameshawekwa kati, ikabidi waingilie kwenda kunusuru usalama wao. Hata hivyo mashabiki nao walikuwa wamepagawa wakirusha maneno makali kwa waamuzi hao kitu ambacho kilizidi kuwaweka waamuzi hao kwenye wakati mgumu.

Mamia ya mashabiki waliokuwepo uwanjani kushuhudia pambano hilo walikuwa wakiwaimbia Mtibwa Sugar na kuwashangilia wakati wakitoka uwanjani baada ya mechi kumalizika.

No comments: