Tuesday, June 7, 2016

JELA MIAKA 30 KWA KUFANYA NGONO NA BINTI WA KUMZAA

Mkazi wa Njiapanda ya Himo wilayani hapa, Daniel Mshana (41), amehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatikana na kosa la kufanya ngono na binti yake wa kumzaa.
Suala hilo liligunduliwa na walimu katika shule aliyokuwa akisoma mtoto huyo mwenye umri wa miaka tisa, baada kumuona siyo mchangamfu na ufaulu wake darasani kuanza kuporomoka.
Kwa mujibu wa ushahidi uliotolewa mahakamani, baada ya mtoto huyo kuonyesha hali hiyo, mwalimu wa darasa alimhoji na ndipo alipoeleza mkasa mzima na suala hilo kufikishwa polisi.
Mshtakiwa alikuwa akiishi nammtoto wake huyo baada ya kutengana na mkewe ambaye aliondoka na watoto wawili wadogo na kumwacha binti huyo na baba yake.
Hukumu hiyo ilitolewa Ijumaa iliyopita na Hakimu Mkazi wa Mkoa Kilimanjaro, Anthony Ngowi aliyesema kitendo alichokifanya mshtakiwa ni kibaya kisichopaswa kufumbiwa macho na jamii.
Awali, Wakili wa Serikali Kanda ya Moshi, Ignas Mwinuka alidai mahakamani hapo kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo kwa tarehe tofauti kati ya Oktoba na Novemba 23, 2015.
Alidai kosa alilolitenda mzazi huyo ni kinyume cha kifungu cha 158 cha kanuni za adhabu.
Kifungu hicho kinasema mwanamume yeyote anayefanya mapenzi na mjukuu au mtoto wake, dada au mama yake anatenda kosa la kufanya mapenzi na maharimu (incest by male).
Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Ngowi alisema ushahidi wa mashahidi sita akiwamo mtoto mwenyewe, daktari na walimu umeithibitishia Mahakama kuwa Mshana alitenda kosa hilo.
Kabla ya hukumu hiyo, Wakili Mwinuka aliiomba Mahakama kutoa adhabu kali kwa vile vitendo vya aina hiyo vinaanza kuongezeka nchini.

No comments: