Advertisements

Thursday, June 30, 2016

MAJAMBAZI WATATU WALIOUA TANGA WAUAWA

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Leonard Paulo
POLISI mkoani Tanga imewaua watu watatu katika mapigano ya risasi wanaodaiwa kuhusika katika mauaji ya watu jijini humo wakiwamo watu wanane waliochinjwa katika Kitongoji cha Kibatini, Kata ya Mzizima.

Limewahakikishia wananchi kwamba eneo la Amboni yakiwemo Mapango ya Majimoto yanayodaiwa kutumiwa na wahalifu waliosababisha mauaji hasa ya wakazi wanane wa Kibatini lipo salama, baada ya watuhumiwa wengine watatu na silaha mbalimbali kukamatwa juzi.

Waliokamatwa ni Abdulkarim Singano, Seif Jumanne na Ramadhani Mohamed ambao baadaye walikufa kutokana na majeraha ya risasi wakati wa mapigano katika msitu wa Kibatini wakati askari wakijaribu kuwadhibiti, siku moja baada ya Abuu Seif anayedaiwa kuwa kiongozi wao kuuawa jijini Dar es Salaam.

Silaha zilizokamatwa ni bunduki mbili aina ya SMG, bastola moja, risasi 30, mapanga, majambia ambavyo vimepatikana kupitia msako ulioshirikisha kikosi kazi cha vyombo vya ulinzi na usalama vilivyohusisha askari kutoka majeshi yote.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Leonard Paulo alibainisha hayo wakati akitoa taarifa ofisini kwake jana kwamba, wahalifu hao walikamatwa Juni 28, mwaka huu wakati askari walipokuwa katika harakati za kuwakamata kwenye msitu wa Kibatini jirani na mapango ya Majimoto, Kata ya Mzizima jijini Tanga.

“Majambazi waliohusika kuua wananchi wanane pale Kibatini ndio tumewakamata lakini kwa bahati mbaya watatu kati yao wamekufa wakati wakidhibitiwa na askari,” alisema Kamanda Paulo. Alisisitiza wameyakagua yaliyokuwa maficho yao na kujiridhisha kuwa Amboni iko salama na imedhibitiwa.

Mapema wiki hii, Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, walitangaza kumuua Abuu Seif aliyeshiriki katika mauaji ya Tanga, baada ya kumpiga risasi alipokataa kujisalimisha baada ya kubainika kujificha katika nyumba moja jijini Dar es Salaam. Alifariki dunia akipelekwa hospitali.

HABARI LEO

No comments: