Advertisements

Saturday, June 25, 2016

MGAHAWA WA KIPEKEE WA PWEZA WAZINDULIWA JIJINI DAR

Muonekano wa Pweza Cafe kwa nje.

Mgahawa huu waleta mapishi mapya ya makange ya pweza, kamba (prawns) na ngisi.
Samaki aina ya pweza amekuwa maarufu sana hapa nchini Tanzania, kutokana na ladha yake tamu na faida zake kiafya. Kutokana na umaarufu huo vijana wa kitanzania wameamua kuwa wabunifu zaidi na kuanzisha mgahawa wa kisasa maalum kwa ajili ya mapishi ya pweza, kamba (prawns) na ngisi unaoitwa Pweza Cafe.


Akiongea na mwanidishi wetu, mmoja wa wamiliki wa mgahawa huo bwana Alfred Kiwuyo alisema, "Sisi wenyewe ni wapenzi wa supu na nyama ya pweza, kamba (prawns) na ngisi lakini mazingira ya awali ya kuuza vyakula hivi kwenye vituo vya daladala na makutano ya barabara kadhaa hapa jijini yalikuwa yanatukatisha tamaa hasa ukizingatia usafi na mapishi yenyewe haukuwa wa kuridhisha sana. Sasa tukajiuliza swali je, haiwezekani kuwa na sehemu ya kisasa zaidi ya kuuza pweza, ngisi na kamba (prawns) na kukawa na mapishi zaidi ya haya. Ndipo tukaamua kuanzisha mgahawa huu ambapo tunapika mpaka makange ya pweza, prawns (kamba) na ngisi."
Vivyo hivyo akiongea na mwandishi wetu mmoja wa wateja waliofika kwenye mgahawa huo wa kipekee nchini alisema, "Mimi nimekula makange ya pweza na ni mara yangu ya kwanza na nimeyapenda kwa kweli, ni matamu. Kwa mara ya kwanza nilivyosikia makange ya pweza nilishtuka kwanza nikasema lazima niyaonje kwa kuwa tumezoea kula makange ya kuku,ng'ombe, na mbuzi lakini sijawahi kuonja makange ya pweza."

Watafiti wa masuala ya kiafya wanasema, gramu 100 za nyama ya pweza ina madini na vitamini za kutosha kwa mahitaji ya mwili wa binadamu kwa siku. Kwa mfano kiwango hiki cha nyama ya pweza kinampatia mwanadamu mahitaji yake ya siku ya madini ya chuma, seleniamu na vitamini B-12. Madini haya na Vitamini hizi ni muhimu katika kuusaidia mwili kupambana na magonjwa,kutengeneza seli hai nyekundu za damu na kuhakikisha ubongo unafanya kazi yake vizuri.

Makange ya Prawns yakiwa tayari kwa ajili ya mteja Pweza Cafe.

Kuanzishwa kwa Pweza Cafe iliyopo nyuma ya jengo la tume ya taifa ya Sayansi na teknolojia, Kijitonyama ni mfano wa kuigwa kwa vijana wabunifu na wenye ndoto za kuwa wajasiriamali nchini hivyo basi ni muhimu kwa vijana wengine kuangalia ni biashara zipi zinaweza kuboreshwa katika jamii yetu na kutengeneza ajira kwa vijana wengine zaidi.

Unaweza kufuatilia zaidi kuhusu mgahawa huu kwa kutembelea tovuti yao: https://www.instagram.com/pwezacafe/

Rosti ya prawns inayopatikana Pweza Cafe.

No comments: