Advertisements

Thursday, July 21, 2016

KINANA ATOA NENO IWAPO JPM ATAMUHITAJI

Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana.
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana ametoa neno endapo Rais John Magufuli atamhitaji kuendelea na wadhifa huo, huku akibainisha kuwa amekutana na changamoto nyingi katika nafasi hiyo kiasi kwamba wakati mwingine alikata tamaa.

Mwanasiasa huyo maarufu ndani ya CCM na nchini, anatarajiwa kuhitimisha uongozi wake wiki hii wakati Mwenyekiti mpya wa CCM Taifa, Rais John Magufuli atakapokabidhiwa uenyekiti huo na kuunda Sekretarieti yake mpya ambayo haijulikani kama itaongozwa tena na Kanali huyo wa zamani wa Jeshi.

Akizungumza jana na waandishi wa habari baada ya kukagua Ukumbi wa Mkutano Maalumu wa CCM utakaofanyika keshokutwa Jumamosi, Kinana ambaye amekuwa katika nafasi hiyo kwa miaka mitatu na nusu, alisema aliombwa katika nafasi hiyo baada ya kuwa aliamua kustaafu, lakini akakumbana na changamoto mbalimbali.

CCM kuwa mbali na wananchi Alisema kuna wakati aliona kama vile chama kiliacha kwenda kwa wananchi na kwamba hakikuwa karibu sana nao.

“Ninyi ni mashahidi, ikabidi kubuni utaratibu mzuri wa kwenda kwa wananchi ili chama kiwe karibu na wananchi, kiwasikilize na kuwa sauti ya wananchi kifuatilie matatizo yao kisimamie utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi,” alisema Kinana na kuongeza kuwa katika kufanya hivyo amekuwa akiwasiliana na Rais na Waziri Mkuu kwa ajili ya matatizo kutatuliwa.

“Changamoto ya pili ya kuimarisha umoja na mshikamano ndani ya chama, hapo nyuma kulikuwa na misukosuko kidogo ya umoja na mshikamano, kushutumiana na kulaumiana,” alisema na kuongeza kuwa kazi nyingine aliyofanya ni kuimarisha umoja ndani ya chama, kushirikiana na viongozi wenzake kuhakikisha chama kinajitahidi kwa kadri ya uwezo wake kurejea katika misingi yake ya awali katika maeneo ya uadilifu, uwajibikaji na utendaji kazi kwa ufanisi.

Azuiwa ziarani

Kinana alisema amekwenda wilaya zote, majimbo, mikoa na nusu ya kata za nchi na amesafiri zaidi ya kilometa 192,000, kufanya mikutano zaidi ya 3,700 ya aina mbalimbali ya ndani na nje na haikuwa kazi rahisi “Changamoto nilizokutana nazo ambazo lazima nikiri ni pale nilipotaka wakati mwingine kufanya ziara kwenye maeneo fulani fulani niliambiwa ni hatarishi siwezi kwenda kwa hiyo ilibidi nibishane na viongozi na watendaji wakuu wa serikali…nikasema hapana nimeamua kwenda lazima niende,” alisema Kinana.

Katibu huyo akitoa mfano alisema kuna wakati aliamua kutoka kwa boti kutoka Nyamisati wilayani Rufiji kwenda Mafia, viongozi wa Mkoa wa Pwani walifikiri si njia salama ya kusafiri na kumpelekea ujumbe asisafiri kwa boti, bali asafiri kwa ndege, lakini alisema hapana ataondoka kwa boti.

“Walichofanya wakakaa kikao cha Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa na wakaniandikia barua rasmi kwamba tunakushauri usisafiri kwa boti safiri kwa ndege kwa maana nyingine walikuwa wanajivua lawama kwa yatakayotokea, lakini vile vile kunitisha kidogo kwamba si salama zaidi nikawasisitiza hapana,” alieleza Kinana.

Ashitakiwa kwa JK

“Baadaye Rais mstaafu Kikwete alikuwa Msoga, viongozi wa Mkoa wa Pwani wakaenda kumwambia tumezungumza na Katibu Mkuu wako naona hasikii tumemuandikia barua ya kumuomba asisafiri na boti hasikii, Rais akaandika meseji ndefu sana…nikamjibu rais nakuheshimu mamlaka yako ni makubwa si vizuri nikakukatalia, lakini niruhusu nikukatalie kwa sababu hata wananchi wanaosafiri kwenye boti hii wanahatarisha maisha yao, ni vizuri na mimi nikahatarisha maisha yangu hata kidogo… akaniambia nimekuelewa endelea,” alibainisha.

Alisema zipo changamoto nyingi sana nyingine, kwa mfano Mbambabay kwenda Kyela, mkuu wa mkoa akamuambia boti haifai kusafiri akasema mara haiwezi kusafiri imeharibika.

“Nikazungumza na Mwakyembe akapeleka mafundi wakatengeneza, safari haikuwa rahisi, lakini changamoto zilikuwa nyingi sana, kwingine Lupingu kule ni gari moja tu ndio inayoshuka chini hakuna kupishana magari nikaambiwa nisiende nikasema nina kwenda,” alisema na kuongeza kuwa kulikuwa na ubishi mwingi wakati mwingine alionekana mtu mmoja kidogo ambaye hasikilizi ushauri sana.

Pia nyingine zinazotokana na changamoto za wananchi kutolipwa mazao yao kwa wakati, mbolea kutofika kwa wakati, halmashauri kutopata fedha za maendeleo kwa wakati, watumishi wa umma wanaohamishwa kwenda vijijini hawaendi vijijini kwenda kuwahudumia wananchi, tatizo kubwa la migogoro kati ya wakulima na wafugaji kati ya wananchi na hifadhi za taifa.

“Ndio maana mnaniona siku hizi nimenyamaza kwa sababu yale yote niliyokuwa nikiyaombea yanafanyika, umangimeza haupo watu wachape kazi wawahudumie wananchi, uadilifu unapigwa vita, rushwa inapigwa vita, uwajibikaji na uadilifu unahimizwa, utendaji kazi unatakiwa na hayo yasipofanyika mtu anaondolewa mara moja,” alifafanua Kinana ambaye kuanzia mwaka 2014 hadi mwanzoni mwa mwaka jana alitembea kote nchini akikisafisha chama chake na kuibana serikali.

Kurejea kwake CCM

“Yalitokea mazingira ambayo niliombwa na viongozi wastaafu na viongozi wa chama kuniomba niwe mtendaji mkuu wa chama chetu. Si nafasi ambayo niliipenda, bali niliitwa na nikakalishwa wakanisihi na mimi nikakubali sababu ni wito na kwa kuwa ni watu ninaowaheshimu na wana dhamana kubwa kwenye nchi yetu, nikakubali kufanya kazi hiyo,” alisema Kinana akizungumzia jinsi alivyoteuliwa kushika nafasi hiyo.

Alisema amekuwepo katika uongozi ndani ya chama kwa muda mrefu (miaka 25) ndani ya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Taifa, na alihisi ni wakati muafaka wa kung’atuka.

“Mwanasiasa mzuri ni yule anayejua wakati wa kuingia na wakati wa kutoka. Ni wakati mzuri wa kung’atuka kuachia waingie wenye umri wa kati na umri wa vijana kuachia waongoze chama na kuwaamini,” alieleza.

Alisema moja ya mambo ambayo walikubaliana wakati ule akajitahidi kukiimarisha chama, kusimamia na kumsaidia mwenyekiti kusimamia mchakato wa kuwapata wagombea kwenye nafasi zote za Urais, Ubunge na Udiwani. Pia alijitahidi kuendesha shughuli za kampeni na uchaguzi na utakamalizika.

“Uchaguzi umekwisha niruhusiwe kupumzika, na wote waliafiki na kukubali sasa muda umefika kwa hiyo nimewakumbusha yale tuliyokubaliana muda wake umefika sasa wengine wakaniuliza hivi ndivyo tulivyokubaliana nikawaambia wazee hamjawa wazee kiasi cha kusahau ndio haya tuliyokubaliana,” alieleza.

Akiombwa na JPM

Alipoulizwa kama akiombwa na Rais Magufuli aendelee kwa Katibu Mkuu, Kinana alisema, “Niseme hajasema, hatujazungumza hilo, likitokea tutaangalia, tutakaa naye kikao kama akiniomba, tutakuwa na kikao na mazungumzo muda utakapofika kama nilivyokuwa na mazungumzo na kikao kama kwa wale walioniomba mwaka 2012.”

Waliokisaliti chama

Akizungumzia walioisaliti CCM katika Uchaguzi Mkuu mwaka jana, mtendaji huyo wa CCM alisema msaliti yeyote adhabu yake ni mbaya sana, hata kwenye chama cha siasa.

“Kwenye CCM wapo watu walioyumba, kulikuwa na wimbi kubwa mwaka jana, watu waliyumba hivi kidogo wakakaa mguu upande huku hawapo na kule hawapo, wako ambao sio tu waliyumba, bali walikiuka maadili na hawakushiriki kwenye shughuli za kampeni,” alisema.

Pia alisema wapo ambao hawakushiriki, hawakusaidia na wakasaidia upinzani na kila mtu atakuwa na adhabu yake kulingana na makosa yake.

“Kama mmekuwa mkifuatilia kuna waliochukuliwa hatua ngazi za wilaya na mikoa. Kwa mfano, Shinyanga 123 walichukuliwa hatua. Wapo wanaotakiwa kuchukuliwa hatua kwenye ngazi za juu, sasa jambo moja mtu yeyote kabla ya kuchukuliwa hatua lazima aelezwe mashtaka yake, apewe fursa ya kusikilizwa, kwa hiyo hawa wote watasomewa mashtaka, watasikiliza na kupewa adhabu kwa kadri itakavyostahili, lakini hatua zitachukuliwa mara baada ya Mkutano Mkuu kumalizika,” alieleza.

HABARI LEO

No comments: