Advertisements

Friday, July 22, 2016

MHE. UMMY MWALIMU AAGIZA KUTENGWA FEDHA YA MFUKO WA MAENDELEO YA WANAWAKE

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (Mb.) akikagua shughuli za maendeleo za vikundi vya wanawake wajasiliamali wa Kata ya Magoweko Wilayani Gairo, Mkoa wa Morogoro.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (Mb.) akiendelea kukagua shughuli za maendeleo za vikundi vya wanawake wajasiliamali wa Kata ya Magoweko Wilayani Gairo, Mkoa wa Morogoro akiwa na Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Ahmed Shabiby (kulia).
. Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (Mb.) akiendelea akiangalia moja ya mashine ya kufyatua matofali wakati wa ziara yake ya kukagua shughuli za maendeleo za vikundi vya wanawake wajasiliamali wa Kata ya Magoweko Wilayani Gairo, Morogoro.Kulia ni Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Ahmed Shabiby (kulia).

Na. Mwandishi –Wetu –Gairo Morogoro.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (Mb.) leo amefanya ziara katika Wilaya ya Gairo, Mkoa wa Morogoro kwa kukagua shughuli za vikundi vya wanawake wajasiliamali wa Kata ya Magoweko.
Akihutubia wanawake na wananchi walio jitokeza katika maonyesho ya shughuli hizo, Mhe Ummy alieleza kuwa Serikali imejipanga katika kumuwezesha mwanamke kiuchumi.

Alisema, uwezeshaji huo utafanyika kupitia mifuko mbalimbali ya kuwawezesha wanawake, ikiwamo Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake (WDF) uliopo katika kila Halmashauri nchini na Benki ya Wanawake Tanzania.

Katika hadhara hiyo Mhe Ummy alimwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Gairo, Bibi Agness Martin Mkandya, kuhakikisha Halmashauri hiyo inatenga asilimia 5 ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake ili fedha hizo ziweze kutumika katika kukopesha wanawake wajasiliamali.

Aidha, aliwaeleza wananchi kuwa serikali itatekeleza ahadi yake ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-20 kwa kutenga kiasi cha shilingi milioni 50 kwa kila Kijiji kama Mfuko wa Mzunguko (Revolving Fund) kwa ajili ya kukopesha vikundi vya wajasiriamali kupitia Ushirika wa Kuweka na Kukopa (SACCOS) katika vijiji husika; hivyo wanawake nao wazichangamkie fedha hizo kwa kuanza kujiandaa kujiunga katika vikundi ili fursa hiyo isiwapite.

Katika kukabiliana na changamoto ya masoko kwa bidhaa zinazotengenezwa na wanawake, Mhe Ummy alisema, Ilani ya uchaguzi ya ccm pia inaelekeza Halmashauri zote kutenga asilimia 30 ya thamani ya manunuzi yake kwa ajili ya bidhaa zinazotengenezwa na vikundi vya vijana au wanawake. Aidha, mbunge wa Jimbo la Gairo, Mhe Ahmed Shabiby aliwaeleza wananchi kuwa wataandaa utaratibu wa kuwa na maonyesho rasmi ya kutangaza kazi za wanawake wajasiliamali wa Wilaya hiyo.
Baadhi ya Wanawake walioshiriki katika shughuli hiyo walieleza kuwa kupitia shughuli za vikundi wameweza kushiriki katika shughuli mbalimbali za kujiongezea kipato ikiwa ni pamoja na kuhamasisha vijana kujiunga na vikundi hivyo, wakilenga pia kuwaelimisha vijana kuacha matumizi ya madawa ya kulevya. Aidha, wanawake hao waliainisha moja ya changamoto kubwa inayo wakabili kuwa ni ukosefu wa mtaji wa kutosha kuendesha biashara zao.

Kupitia hadhara hiyo Mhe Ummy aliwataka wazazi kutilia mkazo elimu kwa watoto wa kike. Alieleza kuwa Wilaya ya Gairo inakabiliwa na tatizo kubwa la mimba na ndoa za utotoni, tatizo ambalo kwa kiasi kikubwa linafifisha jitihada za serikali katika kumpatia mtoto wa kike Elimu.

FULL SHANGWE

No comments: