Advertisements

Monday, July 11, 2016

MTOTO WA MIAKA MINNE AUAWA, ATUPWA KISIMANI JIJINI DAR

Mtoto wa kike, Rahila Salim Ali (4) amekutwa amekufa huku mwili wake ukiwa umening’inizwa kisimani na vidole vya mikono vikiwa vimekatwa na mashavu kuchubuliwa.

Tukio hilo limetokea jana asubuhi, katika eneo Njiapanda, Mbagala, Temeke baada ya mtoto huyo kutoweka nyumbani siku nne zilizopita.

Akizungumzia tukio hilo, mama mzazi wa mtoto huyo, Raziah Ramadhani alisema binti yake alitoweka nyumbani saa tano asubuhi, wakati wakiwa pamoja wakitazama televisheni.

“Alitoka nje kama anaenda kucheza na wote hatukuwa na wasiwasi. Baada ya saa moja tulishtuka baada ya kutomuona, hivyo ikabidi tuanze kumtafuta,” alisema.

Alisema walitoa taarifa polisi na kwenye baadhi ya vyombo vya habari bila mafanikio hadi jana mwili wake ulipokutwa umening’inizwa kwenye kisima cha nyumba ya jirani yao.

“Nilipofika nilishangaa kuona nguo zake ni kavu na ana majeraha,”alisema.

Alisema kisima hicho kina tundu dogo ambalo huenda wauaji walijitahidi kuusukumiza mwili huo ili ionekane kama amefia humo ikashindikana.

Alisema mpaka juzi mchana, kilikuwa kikitumika na kuwa huenda mwili huo ulining’inizwa usiku wa kuamkia jana.

Baadhi ya majirani waliliomba jeshi la polisi kufanya uchunguzi wa kina na kuwachukulia hatua watu ambao wamekuwa wakijihusisha na vitendo vya ukatili dhidi ya watoto.

Kamanda wa Polisi Temeke, Andrew Satta alisema wanaendelea na uchunguzi: “Taarifa zilizopo ni kwamba amekufa maji lakini kwa hayo mazingira mengine tunaendelea kufanya uchunguzi zaidi.”

Chanzo: Mwananchi

No comments: