Advertisements

Monday, July 11, 2016

WAUGUZI WAWILI WASIMAMISHWA KAZI BAADA YA MAMA KUJIFUNGUA KWENYE KORIDO

Siku chache baada ya vyombo vya habari kuripoti mjamzito kujifungulia kwenye korido ya Kituo cha Afya Lyabukande, Shinyanga kwa kukosa huduma, uongozi wa Halmashauri ya Shinyanga umewasimamisha kazi watumishi wawili wa kituo hicho kwa tuhuma za uzembe.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Kiomoni Kibamba ambaye kwa sasa ameteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, jana aliwataja waliosimamishwa kuwa ni pamoja na muuguzi msaidizi wa kituo hicho, Zulfa Mussa na mhudumu katika maabara, Peter Mazengo.

Kibamba alisema wamewasimamisha kazi na kufunguliwa mashtaka ya kukiuka maadili ya utumishi huku wakipewa siku 14 kujibu kwa utaratibu wa ajira ya utumishi.

“Baada ya hapo tunasubiri baraza la madiwani ndilo litatoa uamuzi juu yao.”

Alisema wakati tukio hilo linatokea, watumishi hao walikuwa zamu na kushindwa kumsaidia mjamzito huyo na kitendo hicho kilibainika kuwa cha makusudi na uzembe wa wazi.

“Awamu hii ya tano ni awamu nyepesi kwa kufanya kazi sababu imenyooka na iko wazi. Mtu anayeona hawezi kwenda na kasi atupishe ili wabaki wanaoweza kutekeleza majukumu yao kwa kufuata kanuni, taratibu na sheria za nchi na nilishasema mara kwa mara suala hili,” alisema Kibamba.

Kamati iliyoteuliwa kuchunguza jambo hilo, ikiongozwa na Mganga Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Dk Athuman Pembe ilibaini kuwa baada ya mjamzito huyo kujifungua kwenye korido, watumishi ambao hawakuwapo bali walipata taarifa na kufika kumhudumia mtoto ambaye ana afya nzuri na baada ya muda aliruhusiwa kurudi nyumbani.

Ilivyotokea
Tukio la mjamzito huo, Margareth Charles (22), mkazi wa Kijiji cha Kizungungu lilitokea Julai 2 baada ya kuelezwa na mtaalamu wa maabara kuwa hakuna huduma waende sehemu nyingine, lakini mama huyo alishindwa kutokana na uchungu.

Mtendaji wa Kata ya Lyabukande, Julius Lugende alisema wananchi wamekuwa wakikilalamikia kituo hicho kwa muda mrefu na ilifikia wakati waliandamana kuwakataa watumishi waliopo kutokana na wajawazito kunyanyasika na kujifungua bila usaidizi.

No comments: