Advertisements

Thursday, July 21, 2016

NCCR WAMTIMUA MAKAMU MWENYEKITI WA CHAMA

 Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia (kulia), akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam, kuhusu maazimio mbalimbali yaliyopendekezwa katika kikao cha Halmshauri Kuu ya Taifa ya chama hicho cha kawaida  kilichoketi Julai 16 mwaka huu. Kushoto Katibu Mkuu wa chama hicho, Mosena Nyambabe.Picha na Dotto Mwaibale

Chama cha NCCR – Mageuzi kimemvua uanachama makamu mwenyekiti wake (Bara), Leticia Ghati (pichani) kikimtuhumu kujihusisha na migogoro ndani ya chama na tuhuma nyingine za kijinai. 

Mwenyekiti wa chama hicho, James Mbatia aliwaeleza waandishi wa habari jana kuwa uamuzi huo umepitishwa na Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho. 

Mbunge huyo wa Vunjo na mwenyekiti mwenza wa Ukawa, alisema makosa mengine aliyokutwa nayo Ghati ni pamoja na kukashifu na kutoa tuhuma dhidi ya kiongozi wa chama nje ya utaratibu na kuhujumu chama wakati wa uchaguzi. 

“Kwa makosa hayo ambayo Leticia Ghati aliyatenda wakati wa Uchaguzi Mkuu wa 2015 Halmashauri Kuu ya Taifa, inamsimamisha uongozi na kumvua uanachama,” alisema Mbatia. 
Mustakabali wa chama 
Akizungumzia mustakabali wa chama hicho katika Ukawa, Mbatia alisema Halmashauri Kuu ya chama hicho itaendelea kusimama imara kuhakikisha umoja huo unakuwa bora na taifa linapata Katiba kama yalivyokuwa malengo ya kuanzishwa kwake. 

“NCCR tutahakikisha Ukawa unaboreka na kusimama imara kwa ajili ya kupata Katiba, tumeazimia kuunga mkono jitihada za kuunganisha vyama vinavyounda umoja huu ili kufikia lengo la kuwa na chama  kimoja cha siasa chenye nguvu,” alisema Mbatia.

Mbatia pia alizungumzia hali ya kisiasa na kidemokrasia nchini na kusema chama chake kimebaini kuwa taifa linaongozwa kwa matamko ya Rais John Magufuli badala ya kufuata Katiba, sheria na kanuni.

Alisema demokrasia imeendelea kukiukwa huku uhuru wa kujieleza ukiendelea kudidimizwa na akatolea mfano mwenendo wa Bunge ambao alisema licha ya kuwa chombo cha kikatiba chenye mamlaka kamili ya kujiendesha, limeanza kuingiliwa katika uendeshaji wake kwa wabunge kunyimwa fursa ya kujadili kwa uwazi masuala ya Watanzania. 

Alisema NCCR inakemea matu- mizi ya nguvu za dola kupitia Jeshi la Polisi kuzuia mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa, kuwakamata na kuwaweka rumande viongozi wa kisiasa na kuwashtaki kwa makosa mbalimbali. 

“NCCR Mageuzi tunalaani tabia ya polisi kuwakamata na kuwahoji mara kwa mara viongozi wa kisiasa na kuwashtaki kwa makosa mbalimbali… vitendo hivi ni ukiukaji wa uhuru na haki za vyama vya siasa katika kufanya kazi zao,” alisema Mbatia.

No comments: