Advertisements

Sunday, July 10, 2016

VIONGOZI WATATU WA BARAZA LA VIJANA LA CHADEMA (BAVICHA) WATIWA MBARONI MKOANI DODOMA

JESHI la Polisi mkoani Dodoma linawashikilia viongozi watatu wa Baraza la Vijana la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Bavicha) Taifa, kwa uchochezi na kuikashifu serikali.

Pia viongozi hao wanadaiwa kuvaa fulana zenye maandishi demokrasia imenyongwa, huku nyingine zikiandikwa dikteta uchwara.

Wanaoshikiliwa ni pamoja na Mwenyekiti wa Bavicha- Taifa, Patrobas Katambi, Katibu wa Bavicha-Taifa, Julius Mwita na Mwenyekiti wa Bavicha mkoani Mbeya, George Tito.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa alisema watuhumiwa hao watashikiliwa mpaka Jumatatu watakapofikishwa mahakamani.

“Hawatadhaminiwa mpaka Jumatatu, watakapofikishwa mahakamani,” alisema.

Kamanda Mambosasa alisema kitendo cha viongozi hao kuvaa fulana inayosema demokrasia imenyongwa, inamaanisha serikali inanyonga demokrasia, jambo ambalo ni la uchochezi.

Akizungumza na waandishi wa habari kuelezea tukio hilo Mjumbe wa Baraza Kuu la Chadema-Taifa, Joseph Kasambala alidai walikuwa katika ziara katika baadhi ya mikoa, wakianzia mkoani Mara katika Kijiji cha Mwitongo, Mwanza kabla hawajafika Dodoma juzi saa 8:00 mchana.

Alisema jana walikusudia kukutana na vyombo vya habari mjini Dodoma kuelezea hatua iliyofikiwa katika mpango wao wa Bavicha – Taifa kushirikiana na Jeshi la Polisi mkoani Dodoma, kuzuia wanachama wa CCM kufanya Mkutano Mkuu wa Taifa, Julai 23 mwaka huu.

Alidai wakiwa katika baa ya Cape Town, usiku aliwaacha wenzake na kwenda kukutana na jamaa yake mwingine na baadaye alipata taarifa za wenzake kukamatwa na polisi.

Kwa mujibu wa madai ya Kasambala, kilichomsikitisha ni kukataliwa kuonana nao alipofika kwenye kituo kikuu cha polisi jana asubuhi ambapo alitakiwa kwanza akaonane na viongozi wa Polisi wa wilaya na mkoa (OCD, RPC).

Kasambala alidai taarifa alizopatiwa kwenye kituo hicho cha polisi, zilieleza kuwa kosa wanalotuhumiwa kufanya ni kukashifu serikali, kwa kuvaa fulana yenye maandishi ‘Dikteta Uchwara’, tuhuma alizodai kuwa si za kweli.

Alionesha fulana aliyokuwa amevaa, yenye rangi nyeusi na maandiko meupe yanayosema, ‘Mwl. Nyerere: Demokrasia inanyongwa’ upande wa mbele ikiwa na maandishi ‘haki na amani’.

Alidai kuwa ziara yao inajumuisha viongozi sita wa Bavicha, akiwemo yeye, watatu waliokamatwa ambao ni Katibu Mwenezi wa Bavicha – Taifa, Edward Simbeye na Katibu wa Bavichamkoani Temeke, Hilda Newton.

Kasambala alidai kuwa baada ya kikao hicho, wangerejea Dar es Salaam, ili kukamilisha mikakati hiyo akisema ingawa wanafahamu kuwa hawana mamlaka ya kuzuia mkutano huo wa CCM, lakini wanao wajibu wa kushirikiana na polisi kama raia wema, kuhakikisha maagizo ya serikali yanazingatiwa.

Hivi karibuni, viongozi wa BAVICHA wakiwa jijini Dar es Salaam, walitangaza msimamo wao wa kuzuia mkutano huo kwa kutumia wanachama wake wapatao 4,000.

Makamu Mwenyekiti wa Bavicha, Patrick ole Sosopi, alidai kuwa vijana hao watatoka sehemu mbalimbali ili kuzuia mkutano huo wa CCM ili kusaidia Jeshi la Polisi kutekeleza amri yake ya kuzuia mikutano ya kisiasa hadi 2020.

CHANZO: HABARI LEO

No comments: