Advertisements

Thursday, July 14, 2016

WANA MBWEWE WAKABIDHIWA ZAHANATI YA MAMA NA MTOTO

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Dk Beatrice Byarugaba akikata utepe kuzindua zahanati ya mama na mtoto. Kulia kwake ni mbunge viti maalum mkoa wa Pwani, Subira Mgalu na Mkurugenzi wa Taasisi ya THPS, Dk. Redempta Mbatia. Zahanati hiyo imejengwa kwa Ufadhili wa Taasisi ya Afya ya Marekani kwa kushirikiana na THPS, Taasisi ya Utafiti ya Ifakara na vyuo vikuu vya Columbia na Havard.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Dk Beatrice Byarugaba akizungumza na wananchi wa kijiji cha Mbwewe mkoa wa Pwani wakati wa sherehe za kukabidhiwa zahanati ya mama na mtoto. Kushoto ni Mkurugenzi wa Taasisi ya THPS, Dk. Redempta Mbatia waliojenga zahanati hiyo na anayefuata ni mbunge viti maalum mkoa wa Pwani, Subira Mgalu.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Dk. Beatrice Byarugaba akipima uzito katika sherehe za kukabidhiwa zahanati ya mama na mtoto iliyopo Mbwewe mkoa wa Pwani. Zahanati hiyo ilikabidhiwa na Taasisi ya THPS.


     Na Mwandishi Wetu

WAKAZI wa Mbwewe mkoani Pwani, sasa watakuwa na huduma za uhakika za uzazi baada ya taasisi ya THPS kukabidhi zahanati iliyojengwa kwa ushirikiano na washirika wengine.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi kituo hicho, Mkurugenzi Mkuu wa THPS, Dk. Redempta Mbatia, alisema kuwa kituo hicho kimejengwa kwa gharama ya Sh milioni 70 ambapo ilitokana na mpango wa utafiti wa uboreshaji wa huduma za mama na watoto wa miaka mitano.

“Mradi huu umeanza mwaka 2012, ambapo ulifanyika utafiti wa kuangalia kama njia zilizotumika kupunguza maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi kama zinaweza kutumika pia kusaidia kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wakati wa kujifungua,” alisema.

Dk. Mbatia alisema mradi huo ulilenga kutoa mafunzo kwa watoa huduma za afya wanofanya kazi katika wadi za kujifungulia, kuboresha wadi za wazazi katika zahanati ikiwa ni kuhakikisha vifaa vyote vinapatikana pamoja na kufanya usimamizi shirikishi na timu za afya za halmashauri husika.

“Mpaka sasa watoa huduma 95 kutoka zahanati 12 walipewa mafunzo ya siku 10, maboresho yalifanyika katika zahanati 12 kuzingatia viwango vya Shirika la Afya Duniani (WHO). Maboresho haya yamechangia kuongezeka kwa wagonjwa wanaokuja kliniki kutokana na mazingira rafiki yalivyoboreshwa,” alisema.

Akipokea kituo hicho, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhandisi Evarist Ndikilo, aliyewakilishwa na Mganga Mkuu wa Mkoa, Dk. Beatrice Byarugaba, aliwataka wananchi kukitunza kituo hicho kwani kitakuwa mkombozi kwa wakazi wa eneo hilo.

“Mkoa wa Pwani ulikuwa ukipoteza akina mama 100 katika kila akina mama waliokuwa wakijifungua. Nawaomba wahudumu muwahudumie wagonjwa kwa upendo, hii itachangia wagonjwa kuja hospitali badala ya kuamua kujifungulia nyumbani,” alisema.

Mradi huo umeendeshwa kwa ushirikiano na Taasisi ya Utafiti ya Ifakara, Vyuo vikuu vya Columbia na Havard vya Marekeni kwa ufadhili wa Taasisi ya Afya ya Marekani.

No comments: