Advertisements

Tuesday, August 16, 2016

WANAFUNZI WA SHULE YA MSINGI YA MASANZA WASOMEA JUANI.

Na, Shushu Joel, BUSEGA

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Msingi Masanza katika Kijiji cha Mitindu Kata ya Kiloleli, Wilaya ya Busega, Mkoani Simiyu, wanalazimika kusomea kwenye mti kutokana na upungufu wa madarasa. 


Aidha upungufu huo wa madarasa unawalazimu wanafunzi wengine kusomea juani katika madarasa mawili ambayo hayajapauliwa licha kufikia hatua hiyo miaka miwili iliyopita. 

Shule hiyo ilianzishwa tangu mwaka 2006 lakini mpaka sasa haina hata nyumba moja ya walimu. 

Mwalimu mkuu wa shule hiyo Vedasto Chibuga amesema kutokana na uwepo wa changamoto hizo kunapelekea idadi kubwa ya wanafunzi kusomea kwenye darasa la vyumba viwili ambalo halijaezekwa, huku wengine wakisomea chini miti.


Chibuga aliongeza kuwa wanaosomea kwenye darasa hilo ni wanafunzi wa awali,darasa la sita na darasa la tatu, lakini ikifika majira ya saa tano asubuhi hulazimika kusitisha vipindi kutokana na jua kali na kwenda kuwachanganya na wananfunzi madarasa mengine. 


“Sera ya elimu inasema kuwa kila chumba wasome wanafunzi 45 lakini hapa kwangu mkondo mmoja wanasoma wanafunzi wasiopungua 100 kutokana na changamoto hizo za uhaba wa vyumba vya madara”. 

Aidha Chibuka alisema kuwa serikali ndio ya kulaumiwa kwani wananchi wao walitimiza wajibu wao wa kuchangishana kwa ajili ya ujenzi wa boma hilo tangu mwaka 2013. 

Kwa muji mwalimu mkuu huyo, hali inawafanya walimu kukata tamaa hali inayopelekea wanafunzi kutofanya vizuri kwenye matokeo ya mitihani ya kitaifa kutokana na mazingira magumu ya kufundishia.


Mmoja wa wazazi wa wanafunzi katika shule hiyo, Mikwanga Yona, alisema kuwa ni aibu kwa serikali kushindwa kupaua jengo hilo lililojengwa kwa nguvu za wananchi, na kwamba hali hiyo inaweza kufanya wananchi kukata tamaa kuchangia maendeleo katika maeneo yao kwa kukatishwa tamaa na serikali kwa kushindwa kuunga mkono jitihada zao. 


Ofisa Elimu Kata ya Kiloleli John Mayunga amethibitisha kuwepo kwa hali hiyo, na kwamba jambo hilo wamelifikisha katika kikao cha maendeleo ya kata ambacho mwenyekiti wake huwa diwani wa kata husika, na kuongeza kuwa pengine serikali inalifanyia hivyo kwa kuwa walishaliwasilisha katika ngazi ya halmashauri.

1 comment:

Anonymous said...

Then inaletwa sera ya kinamama fyatueni watoto kwa wingi nitawasomesha bure. Wasomee juani wakirudi nyumbani watakula karatasi!!