Advertisements

Friday, September 30, 2016

SAUDI ARABIA INAWASI WASI NA SHERIA MPYA ILIYOPITISHWA NA BUNGE LA MAREKANI

Saudi Arabia imesema hatua ya Bunge la Congress ambayo itawawezesha jamaa za waathiriwa wa shambulio la 9/11 kulishtaki taifa hilo ni suala linalozua "wasiwasi mkubwa".

Mnamo Jumatano, Bunge la Congress lilipinga kura ya turufu ya Rais Barack Obama dhidi ya mswada ambao unawawezesha jamaa za watu karibu 3,000 waliofariki kwenye shambulio hilo kufungulia mashtaka maafisa wa Saudi Arabia waliochangia shambulio hilo.

Rais Obama alitahadharisha kwamba hatua hiyo inatoa "mfano hatari".

Watu 15 kati ya 19 walioteka nyara ndege zilizotumiwa kutekeleza mashambulio hayo walikuwa raia wa Saudia, lakini ufalme huo umekana kuhusika kwa vyovyote vile.

Ikulu ya White House, pia ilionya kuwa hatua hiyo huenda ikahatarisha maisha ya wanajeshi wa Marekani, walioko mataifa ya nje ambao wataweza kushtakiwa katika nchi hizo.
Bunge la Marekani lapinga turufu ya Obama
Familia za wahanga kuishitaki Saudi Arabia

Hayo yakijiri, viongozi wa chama cha Republican katika Congress wamesema wanataka kutafakari upya sehria hiyo.

Kiongozi wa wengi katika bunge la Senete, Mitch Mc-Connell, amekiri kuwa wabunge walikuwa bado hawajaelewa madhara ambayo yanaweza kutokana na sheria hiyo.

"Kila mtu alielewa ni nani wangefaidi lakini hakuna aliyeangazia sana athari ambazo mswada huo ungesababisha kwenye uhusiano wetu na mataifa mengine," Bw McConnell amesema.

Msemaji wa ikulu ya White House Josh Earnest amesema huo ni mfano mzuri wa kisa cha mnunuzi kuanza kujutia ununuzi muda mfupi tu baada ya kununua.

Saudi Arabia, taifa la kifalme lenye utajiri mkubwa wa mafuta, ni mshirika mkuu wa Marekani Mashariki ya Kati.

Ufalme huo ulikuwa umepinga sana sheria hiyo ya Haki Dhidi ya Wafadhili wa Ugaidi (Jasta).

Taifa hilo hata hivyo halitasema ni hatua gani linaweza kuchukua lakini limetoa wito kwa Congress kubatilisha uamuzi wake.

Jamaa za waliouawa wakati wa shambulio la 9/11 wamefurahia kupita kwa mswada huo.

BBC

No comments: