Advertisements

Sunday, May 28, 2017

Ikulu yaijibu Acacia kuhusu mchanga wa madini

Uamuzi wa Serikali kuhusu suala la usafirishaji wa mchanga wa madini, utategemea ripoti ya kamati ya pili iliyoundwa na Rais John Magufuli kuchunguza suala hilo.

Hayo yamebainishwa jana na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais (Ikulu), Gerson Msigwa ikiwa ni siku moja baada ya kampuni ya Acacia kuitaka Serikali kuunda kamati huru kuchunguza kiasi cha madini kwenye makontena yake 277 yaliyozuiwa bandarini.

Wiki iliyopita, Rais Magufuli alikabidhiwa ripoti na kamati ya kwanza iliyoongozwa na Profesa Abdulkarim Mruma ambayo ilibaini kuwa makontena hayo yana tani 7.8 za dhahabu.

Pia, Acacia wanadai hawakupewa ripoti ya kamati hiyo licha ya kutoa ushirikiano wakati wa uchunguzi.


“Sijui chochote kuhusu hao Acacia kuomba iundwe kamati huru, lakini tunasubiri ripoti ya kamati ya pili iliyoundwa kuchunguza sakata hili wampelekee ripoti Rais,” alisema Msigwa.


Kamati ya awali iliyokuwa ikiongozwa na Prof. Mruma ambayo ilikabidhi ripoti yake Mei 24 mwaka huu ilionyesha kuwa kiwango cha madini yaliyomo kwenye makinikia hayo ni zaidi ya yale ambayo hujazwa kwenye makabrasha.


Mbali na kuonekana kiasi kuzidi, lakini kamati hiyo ilibaini pia kuna madini makakati (strategic metals) ambayo yamo kwenye makinikia hayo lakini hayakuwa yakitajwa na kampuni zinazosafirisha mchanga nje jambo lililosababisha serikali kupata hasara ya mabilioni.

Kwa upande wao Acacia, walipinga ripoti hiyo na kusema wao hutangaza kila kitu kwa mujibu wa sheria na kulipa tozo zote stahiki hivyo kuomba iundwe kamati huru kuchunguza upya kiasi cha madini kwenye mchanga huo.

No comments: