Advertisements

Thursday, May 11, 2017

Maalim Seif ‘amchongea’ Lipumba kwa Gwajima


Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad ameutua mgogoro wa chama che kwa Askofu Mkuu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima huku kiongozi huyo wa kidini akitangaza kuwa atamlipua Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba Jumapili ijayo.

Akizungumza Dar es Salaam jana wakati alipomtembelea Askofu Gwajima, Maalim Seif alibainisha kwamba amemweleza kiongozi huyo mambo mbalimbali ikiwemo suala la mgogoro ndani ya CUF, aliodai umesababishwa na Lipumba.

Alisema kuwa ameamua kwenda kwa Askofu Gwajima kumweleza hayo kwa sababu ni rafiki yake na hawajaonana siku nyingi lakini pia kiongozi huyo alikuwa haelewi mgogoro wa CUF umesababishwa na nani.

"Nimemweleza Askofu Gwajima mambo mengi hususani mgogoro wa CUF hivyo ataamua mwenyewe nini afanye kutokana na niliyomweleza,"alisema.

Aliongeza kuwa mbali na kwenda kwa Gwajima  pia ameshazungumza na viongozi wengine wa dini husuani ya Kiislamu.

Kwa upande wake, Askofu Gwajima alisema kuwa ameshafahamu chanzo cha mgogoro huo kwa kuwa Maalim ni rafiki yake wa siku nyingi lakini Lipumba hana urafiki naye.



"Mimi huyu ni rafiki yangu kwa hiyo nilitaka kujua Professa Lipumba anafanya nini kuvuruga CUF, hivyo nilitaka kujua Lipumba amepatwa na nini mpaka amevuruga chama chako na kiukweli mimi nilikuwa siufahamu vizuri huu mgogoro ila saizi Seif ameniambia kwa hiyo na mimi nataka nitafakari alichoniambia rafiki yangu ni ‘digest’ baada ya hapo nitajua nafanya nini” alisema Gwajima

Alipoulizwa kama watu watarajie chochote kutokea kuhusu CUF, Maalim Seif na Lipumba kwenye ibada Jumapili ijayo, Gwajima alijibu: “Kumbe mnajua, subirini Jumapili ifike nitamlipua na tutajua amekula maharage ya wapi.”

No comments: