Advertisements

Thursday, June 29, 2017

WADAU WA ELIMU NA CHAMA CHA WALIMU WAKUTANA KUJADILI KUHUSU KODI NA UBORA WA ELIMU NCHINI TANZANIA ELIMU

Mwakilishi kutoka Mtandao wa Kodi Tanzania (TTJC), Grace Masalakulangwa akiwasilisha ripoti ya utafiti ya One Billion Question iliyotafitiwa na shirika la ISCEJIE katika Mkutano uliowakutanisha wadau wa Elimu na Wenyeviti wa Chama cha Walimu ngazi ya mikoa ya Tanzania Bara  iliyofanyika jijini  Dar es Salaam. 
Afisa Mradi wa Elimu kutoka TENMET, Alistidia Kamugisha akifungua mkutano na kuwaelezea malengo ya mkutano huo wa siku mbili kwa wadau wa elimu na Chama cha Walimu Tanzania uliofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Blue Pearl jijini Dar es Salaam.
 Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TENMET), Cathleen Sekwao akitoa mada kuhusu umuhimu wa ukusanyaji wa rasilimali za ndani na kuwekeza katika kuboresha sekta ya elimu hususani kwa mtoto wa kike na maslahi ya walimu katika mkutano uliowakutanisha wanachama wa chama cha walimu Tanzania (CWT/TTU).
Meneja Mradi wa Elimu kutoka shirika la ActionAid Tanzania Ndugu Karoli Kadeghe akiwasilisha changamoto zinazoikabili elimu msingi hapa nchini ikiwa ni pamoja na upungufu wa vyumba vya madarasa, upungufu wa walimu kwenye mkutano uliowakutanisha wadau wa elimu pamoja baadhi ya viongozi wa Chama cha Walimu ngazi ya mikoa ya Tanzania Bara  iliyofanyika jijini  Dar es Salaam. 
  Baadhi ya wadau wa elimu nchini Tanzania wakichangia mada kwenye mkutano uliowakutanisha ili kujadili kodi na ubora wa elimu hapa nchini Tanzania  kwenye mkutano uliofanyika jijini Dar 

Shirika la ActionAid-Tanzania, Mtandao wa Elimu Tanzania, Shirika la Maendeleo ya Elimu Singida-MEDO na Mtandao wa Asasi za Kiraia-KINGONET  kwa pamoja wanatekeleza mradi wa uhamasishaji utoaji elimu bora kupitia rasilmali zetu wenyewe ( PROMOTING QUALITY EDUCATION THROUGH PROGRESSIVE DOMESTIC RESOURCE MOBILIZATION) unaotekelezwa huko Kilwa na Singida Vijijini kwa ngazi ya wilaya kwa kufanya kazi na kamati za shule na klabu za haki za watoto shuleni. Kitaifa MRADI Huo unalenga kufanya  utetezi wa mabadiliko ya kisera na sheria  hasa suala la ulipaji kodi, ukusanyaji kodi kwa haki (tax Justice), uzibaji wa mianya ya uvujaji wa kodi  ili makusanyo yaongezeke na yagharimie huduma bora kwa wananchi wa Tanzania hususani kuboresha utoaji wa Elimu bora Nchini.

Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania Bi. Cathleen Sekwao akifungua mkutano huo aligusia pia kuhusu “utoaji wa huduma za jamii hapa nchini unakabiliwa na ufinyu wa fedha, wote tu mashahidi kuwa hadi kufikia mwezi Machi, 2017 serikali ilikuwa imetoa asilimia 34 tu ya bajeti yote ya 2016/2017. Jambo hili lina madhara makubwa katika utoaji wa huduma za jamii hasa elimu msingi yenye ubora  hasakwa mtoto wa kike”.
Aliongelea pia serikali kushindwa kutoa asilimia mia moja ya fedha za kutekeleza bajeti ya 2016/2017 tafiti zinaonyesha kuwa Tanzania inapoteza fedha nyingi kupitia misamaha ya kodi.

Meneja Mradi wa Elimu kutoka shirika la ActionAid Tanzania Ndugu Karoli Kadeghe aliwasilisha changamoto zinazoikabili elimu msingi hapa nchini ikiwa ni pamoja na: Upungufu wa vyumba vya madarasa, Upungufu wa ofisi za walimu, Upungufu wa vyoo vya wanafunzi,Uwiano usiokubalika kitaratibu wa mwalimu na wanafunzi, Shule nyingine kukosa kabisa walimu wa kike.

 Upungufu wa nyumba za walimu, fedha za ruzuku zisizotosheleza, utegemezi wa bajeti ya nchi za nje unaoathiri pia bajeti ya elimu na kusababisha Serikali kushindwa kugharimia kiufanisi utoaji wa elimu, mgawanyo wa ruzuku usiozingatia mahitaji halisi ya wenye uhitaji maalumu, jinsia na mahitaji ya kijiografia na pia shule changa na zile ambazo ni kongwe, Kuwa na mipango ya kibaguzi-Shule inayofanya vizuri ndiyo inapewa fedha(payment for results- P4R) kutoka mpango wa BRN bila kujali mizania ya usawa wa mazingira kati ya shule na shule, Kukosekana kwa mafunzo kazini kwa walimu, Kutopandishwa madaraja walimu, Kutolipwa kwa wakati stahiki za walimu wanaohamishwa/kustaafu mfano pesa ya usafiri.

Mratibu wa Inter Faith Standing Committee Bi. Grace Masalakulangwa aliwasilisha kuhusu Utafiti wa Ripoti ya “1 Billion Question” iliyojikita kubaini upotevu wa kodi katika sekta ya madini au uziduaji katika wilaya za Kilwa, Tarime na Geita. Utafiti huo umebaini serikali inapoteza takribani dola bilioni 1.83 sawa na Tsh trilioni 4.09 kwa mwaka kupitia misamaha ya kodi, uhamishaji wa fedha nje ya nchi bila kufuata utaratibu, kushindwa kutoza kodi sekta isiyo rasmi na aina nyingine za ukwepaji kodi.

Washiriki mbalimbali wakichangia katika mkutano huo, walishauri serikali kuboresha ukusanyaji wa kodi na utengaji wa bajeti katika sekta ya maendeleo hususani sekta ya elimu. Baadhi ya washiriki walichangia pia kukosekana kwa ufanisi na maendeleo yenye tija katika sekta ya Elimu kutokana na usimamizi mbovu wa elimu, serikali kushindwa kuwekeza katika elimu, kuwepo kwa wizara mbili zinazosimamia elimu na muda mwingine kuingiliana kwa majukumu pamoja na kutozingatiwa katika maslahi ya walimu.  

No comments: