Advertisements

Tuesday, July 25, 2017

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Akutana Na Madaktari kutoka Diaspora - HEAD, INC

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  Balozi Seif Ali Iddi alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaelewa na kutambua  umuhimu wa Taasisi zinazojumuisha Watanzania walioko nje ya Nchi zenye utararibu wa kuchangia maendeleo ya Uchumi na Kijamii kupitia misaada na huduma mbali mbali. Alisema umuhimu huo umepelekea Serikali kuunda Idara ya Uratibu ya Wazanzibar  wanaoishi nje ya Nchi  na Ushirikiano wa Kimataifa ili kuzipa nguvu Taasisi hizo ikilenga zaidi  ile ya Diaspora.

Balozi Seif Ali Iddi alieleza hayo wakati akizungumza na  Timu ya Madaktari, Wataalamu wa Sekta ya Afya pamoja na Wauguzi kutoka Nchini Marekani wanaounda Timu ya Diaspora ambao wapo Zanzibar  kutoa huduma  mbali mbali za Afya bure katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja katika kipindi cha siku Tano kilichoanzia  Jumatatu. Alisema azma ya Timu hiyo  ya Madaktari ya kusogeza huduma za Kijamii  kwa Wananchi wa rika zote Visiwani Zanzibar  imeleta faraja  kubwa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliyojipanga kuimarisha huduma za Afya katika kila masafa yasiyopungua Kilomita Tano. “ Sera ya Afya Zanzibar ni kuwa na Vituo vya Afya kila baada ya kilomita Tano ili kuwaondoshea shiha ya kupata huduima hiyo Wananchi hasa Vijijini”. Alifafanua  Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.

Balozi Seif  aliihakikishia Tumu hiyo ya Madaktari kutoka Marekani chini ya Mwamvuli wa Diaspora kwamba Serikali Kuu itaendelea kushirikiana nao katika kuona malengo waliyojipangia yanafanikiwa kwa kiwango kikubwa. Hata hivyo Balozi Seif aliwaasa wananchama wa Jumuiya hiyo ya Diaspora  wale wenye asili ya Zanzibar na Tanzania kwa ujumla kukunjua zaidi mikono yao katika kusaidia Jamii yao ili faida ya uwepo wao nje ya Nchi uweze kuleta tija. Alisema ni vyema masuala hayo yakaenda sambamba kwa Wanachama hao kuangalia hatma ya maisha yao ya baadae wakielewa kwamba Nyumbani kutabakia muhimu kwao katika maisha yao ya baadae. Mapema Kiongozi wa Timu ya Madaktari hao Kutoka Nchini Marekani  wa Diaspora mwenye asili ya Tanzania Mtaalamu wa Maabara Asha Nyang’anyi alisema Timu yake imejipanga kutoka Huduma za Afya Zanzibar kwa Wananchi wa rika zote.
Bibi Asha alisema uwepo wao Nchini utatoa fursa kwa watu mbali mbali kuchunguzwa afya zao hasa katika maradhi ya Ngozi, Shindikizo la Damu. Kisukari pamoja na afya ya akina Mama. 

Alisema uwamuzi wao huo umekuja baada ya washirika wa Taasisi hiyo kutoka Nchi mbali mbali Duniani hasa zile za Bara la Afrika wanaoishi Nchini Marekani kujikusanya pamoja wakilenga kusaidia Jamii ya Nchi zitakazohitaji huduma za Kijamii ambazo ziko ndani ya uwezo wao.

Timu hiyo ya Madaktari, Wataalamu wa Sekta ya Afya pamoja na Wauguzi kutoka Nchini Marekani wanaounda Timu ya Diaspora wana asili ya Mataifa ya Nigeria, Cameroun, Lesotho, Norway, Canada na wengi wao ni Watanzania.


Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Picha na – OMPR – ZNZ.
Balozi Seif  aliyepo kati kati waliokaa vitini akiwa katika Picha ya pamoja na Timu ya Madaktari na Wauguzi kutoka Nchini Marekani kupitia Taasisi ya Diaspora waliopo Zanzibar kutoa huduma za Afya.

 Kiongozi wa Timu ya Madaktari na Wauguzi kutoka Nchini Marekani kupitia Taasisi ya Diaspora Bibi Asha Nyang’anyi Kulia akimkabidhi Balozi Seif  baadhi ya Vifaa na Dawa zitakazotumika wakati wanapotoa huduma za Afya. 

BaloZi Seif  Kushoto akibadilishana mawazo na Mkuu wa Kitengo cha Mahesabu cha Taasisi ya Head, inc  ilichounda Timu ya Madaktari na Wauguzi kutoka Nchini Marekani kupitia  Diaspora Bwana Iddi Sandaly.   


 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akisalimiana na Baadhi ya Timu ya Madaktari na Wauguzi kutoka Nchini Marekani kupitia Taasisi ya Diaspora ambao wapo Zanzibar kutoa huduma za Afya bure kwa muda wa siku Tano.







No comments: