Advertisements

Saturday, August 19, 2017

MAKAMU WA RAIS AHUDHURIA UFUNGUZI RASMI WA MKUTANO WA 37 WA SADC KATIKA UKUMBI WA O.R TAMBO, MJINI PRETORIA AFRIKA KUSINI

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan leo tarehe 19 Agosti 2017, amehudhuria  ufunguzi rasmi wa Mkutano wa 37 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika – SADC mjini Pretoria Afrika Kusini akimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.
John Pombe Magufuli.

Mhe. Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan ametoa taarifa fupi kuhusu majukumu ya SADC Organ kwa kipindi cha Agosti 2016 - Agosti 2017 kwa niaba ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa SADC Organ anayemaliza muda wake.

Makamu wa Rais amewasilisha kwa Wakuu wa Nchi na Serikali taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya SADC Organ kwa kipindi cha Agosti 2016 hadi Agosti 2017 kwa niaba ya Mwenyekiti wa SADC Organ anayemaliza muda wake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli.
Taarifa hiyo inaelezea hali ya kisiasa, kiulinzi na kiusalama katika Kanda katika kipindi tajwa hususan katika Nchi za DRC, Madagascar na Lesotho.


Aidha taarifa hiyo pia imetoa mapendekezo ya namna ya kutatua changamoto zinazoendelea kuikabili Kanda katika maeneo ya siasa, ulinzi na usalama.

Taarifa hiyo pia imeelezea hali ya demokrasia na chaguzi zilizofanyika kwa kipindi cha 2016/2017 kwa nchi wanachama.

Katika Mkutano huu Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan amekabidhi Uenyekiti wa Asasi ya SADC ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama kwa Angola, baada ya Tanzania kukamilisha kipindi cha Uongozi wake chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

Mkutano huu wa SADC uliofunguliwa rasmi leo na Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini ambaye ni Mwenyeji wa Mkutano wa 37 wa SADC, ulitanguliwa na mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Troika Mbili uliofanyika tarehe 18 Agosti, 2017

Mkutano wa Troika Mbili umefanyika kwa kuzingatia mapendekezo ya Mkutano wa Mawaziri wa Kamati ya Asasi ya Ushirikiano wa Siasa,Ulinzi na Usalama (SADC MCO) uliofanyika Dar es Salaam tarehe 20 na 21 Julai, 2017 ambapo Mawaziri waliona ipo haja ya kuitisha Double Troika pembezoni mwa Mkutano huu wa 37 ili kujadili pamoja na mambo mengine, hali ya ulinzi na usalama.

Troika Mbili inahusisha nchi wanachama sita ambao kwa sasa ni Swaziland, Tanzania, Afrika Kusini, Angola, Botswana na Msumbiji.

Serikali ya Afrika Kusini ambayo ni mwenyeji wa Mkutano huu wa 37 wa SADC na Mwenyekiti imependekeza kuwa kaulimbiu ya Mkutano wa 37 iwe ni Kushirikiana na Sekta Binafsi katika kuendeleza Viwanda na Kuongeza Thamani ya Bidhaa.

Akizungumza mara baada ya kukabidhiwa Uenyekiti wa SADC kutoka kwa Mfalme Mswati III, Rais wa Afrika Kusini Mhe. Jacob Zuma amesisitiza nchi wananchama kutekeleza kwa vitendo Kauli Mbiu ya Mkutano wa 37 wa SADC juu ya kushirikiana na Sekta Binafsi katika kuendeleza Viwanda na Kuongeza Thamani ya Bidhaa kuwa ndio njia pekee ya nchi za Jumuiya hiyo kupiga hatua kimaendeleo.

Rais Zuma amesisitiza nchi za Afrika kufanyakazi kwa bidii na kuhakikisha rasilimali za nchi  zinatumika kwa faida ya maendeleo yay a kweli.

Wakuu wa Nchi na Serikali wamepokea taarifa ya utekelezaji wa Mkakati wa Maendeleo ya Viwanda wa SADC 2015 - 2063 ambao ulipitishwa katika Mkutano wa Dharura uliofanyika tarehe 29 Aprili, 2015 mjini Harare, Zimbawe.

Mkakati huu unalenga kuzifanya nchi za SADC kuwa na uchumi wa viwanda na kushiriki zaidi katika  mnyororo wa thamani kikanda na kimataifa  na hivyo kuongeza kasi ya maendeleo kwa wananchi wake.

Mkutano wa 37 wa Wakuu wa Nchi na Serikali (SADC) utahitimishwa hapo kesho Jumapili tarehe 20 Agosti 2017, kwa kutolewa Tamko (Communique) litakaloelezea yaliyojiri katika Kikao cha Wakuu wa Nchi na Serikali.

No comments: