Advertisements

Tuesday, August 15, 2017

Mke wa Mugabe akamatwa Afrika Kusini

Johannesburg, Afrika Kusini. Grace Mugabe, ambaye ni mke wa Rais Robert Mugabe aweza awe amewafanyia ubabe watu kadhaa nchini kwake lakini kitendo cha kumshambulia, kwa waya wa umeme, mrembo mwenye umri wa miaka 20 kimemweka matatani.
Mama Mugabe alikamatwa jana na alikuwa anatarajiwa kufikishwa mahakamani leo kwa kosa la kumshambulia mrembo huyo anayedaiwa kuwa ni mpenzi wa mtoto wake.
“Imeandikwa katika mitandao mingi ya kijamii kwamba mrembo wa Afrika Kusini mwenye umri wa miaka 20 inadaiwa alishambuliwa na mwanamke mmoja maarufu katika Hoteli ya Sandton mjini Johannesburg,” msemaji wa polisi Vish Naidoo alijibu vyombo vya habari kwa baruapepe. Mrembo huyo jana Jumatatu, “alileta malalamiko ya kushambuliwa kwa lengo baya la kudhuriwa mwili.”
Naidoo alikataa kutaja jina la mtuhumiwa kwa sababu alikuwa hajafikishwa mahakamani
Lakini Waziri wa Mambo ya Ndani, Fikile Mbalula amemtaja mwanamke huyo kuwa ni Grace Mugabe na kwamba alijisalimisha polisi.
"Anashikiliwa na polisi kwa sababu alitoa ushirikiano, na akajisalimisha yeye mwenyewe,” Waziri wa Mambo ya Ndani, Fikile Mbalula aliliambia jana shirika la habari la eNCA.
Fikile alisema Grace anatarajiwa kufikishwa kortini Jumanne
Waziri huyo alisema Grace lazima ajibu mashtaka dhidi yake maana yeye waziri hawezi kwenda Zimbabwe, akampiga mtu na akatarajia suala hilo litafunikwa chini ya zulia.
Chama tawala cha Zimbabwe, Zanu-PF kilisema kwa ujumbe wa Twitter kwamba Grace “alishambuliwa” lakini wanashukuru kwamba “ni mzima na yuko salama”. Hakukuwa na maelezo ya kina.
Zanu PF walituma ujumbe mwingine tena wakisema Mama Mugabe anaendelea vizuri baada ya kwenda Afrika Kusini kutibiwa kifundo cha mguu

Chanzo: Mwananchi

No comments: