Advertisements

Monday, September 25, 2017

Kituo cha Usuluhishi CRC chazinduwa iPad kupokea taarifa za ukatili

Mwenyekiti wa Kituo cha CRC, Saida Mukhi (kushoto) akizinduwa 'iPad' maalum kwa ajili ya upokeaji taarifa za matukio ya vitendo vya ukatili wa kijinsia kwenye wilaya mbili za Mkoa wa Dar es Salaam, yaani Kinondoni (Kata za Makumbusho na Kawe) na Ubungo (Kata ya Saranga). Kulia ni Mratibu wa Kituo cha Usuluhishi cha CRC, Bi. Gladness Munuo. 
Mwenyekiti wa Kituo cha CRC, Saida Mukhi (kushoto) akionesha 'iPad' maalum kwa ajili ya upokeaji taarifa za matukio ya vitendo vya ukatili wa kijinsia mara baada ya kuizinduwa.

Mratibu wa Kituo cha Usuluhishi cha CRC, Bi. Gladness Munuo (kulia) akizungumza katika hafla hiyo. Kushoto ni Mwenyekiti wa Kituo cha CRC, Saida Mukhi.[/caption]   VITENDO vya ukatili wa kijinsia vinavyoshamiri kila uchao maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam, huenda vikapungua endapo kampeni madhubuti iliyoanzishwa na Kituo cha Usuluhishi wa masuala ya kijamii na kijinsia (CRC) kwa ufadhili wa Shirika la Legal Service Facilities (LSF) itafanikiwa kama ilivyopangwa. Ili kurahisisha ufikishaji taarifa za matukio ya vitendo vya ukatili wa kijinsia kwenye wilaya mbili za mkoa wa Dar es Salaam, yaani Kinondoni (Kata za Makumbusho na Kawe) na Ubungo (Kata ya Saranga), CRC imezinduwa 'iPad' maalum kwa ajili ya upokeaji taarifa za matukio hayo kutoka kwa wadau wake maeneo hayo. Akizinduwa kifaa hicho, Mwenyekiti wa CRC, Saida Mukhi kwenye semina ya wadau wa mradi huo wakiwemo wasaidizi wa sheria, maofisa ustawi wa jamii, wanasheria na Dawati la Jinsia, maofisa watendaji wa mitaa kutoka wilaya hizo aliwataka kuhakikisha wanashirikiana katika kuibua matukio hayo, kuyakemea huku kila mmoja akiwajibika eneo lake ili kutokomeza matukio hayo. Kwa upande wake, Mratibu wa Kituo cha Usuluhishi cha CRC, Bi. Gladness Munuo awali kabla ya uzinduzi huo aliwataka wadau kukitumia kifaa hicho kitakachokuwa kikipokea taarifa za matukio ya vitendo vya unyanyasaji na kuyafanyia kazi jambo ambalo likifanywa kwa ufasaha litapunguza vitendo hivyo hasa katika maeneo ya mradi. Akifafanua juu ya mradi huo Ofisa Mradi wa Kituo cha Usuluhishi wa masuala ya kijamii na kijinsia, CRC, Suzan Charles aliongeza kuwa mradi huo utasaidia utoaji wa huduma za msaada wa kisheria na ushauri nasihi kwa wahanga wa vitendo vya ukatili wa kijinsia kwenye wilaya mbili za mkoa wa Dar es Salaam. Alisema lengo la mradi huo unaofadhiliwa na shirika la Legal Service Facilities (LSF) ni kuhimarisha zaidi upatikanaji wa msaada wa kisheria na ushauri nasihi kwa wahanga wa ukatili wa kijinsia. Aliongeza kuwa mradi huo utajikita zaidi katika utoaji wa msaada wa kisheria na ushauri nasihi kwa waathirika na kuhakikisha mfumo wa upatikanaji wa haki unafanya kazi vizuri.    
Ofisa Mradi wa Kituo cha Usuluhishi wa masuala ya kijamii na kijinsia, CRC, Suzan Charles akizungumza na washiriki wa warsha hiyo (hawapo pichani). 
Ofisa Mradi wa Kituo cha Usuluhishi wa masuala ya kijamii na kijinsia, CRC, Suzan Charles (aliyesimama mbele) akizungumza na washiriki wa warsha kwa wadau wa utoaji wa huduma za msaada wa kisheria na ushauri nasihi kwa wahanga wa vitendo vya ukatili wa kijinsia kwenye wilaya mbili za mkoa wa Dar es Salaam.
Sehemu ya washiriki wa warsha kwa wadau wa utoaji wa huduma za msaada wa kisheria na ushauri nasihi kwa wahanga wa vitendo vya ukatili wa kijinsia kwenye wilaya mbili za mkoa wa Dar es Salaam, Kinondoni (Kata za Makumbusho na Kawe) na Ubungo (Kata ya Saranga) wakiwa kwenye semina.

No comments: