Advertisements

Tuesday, October 24, 2017

WAZIRI MKUCHIKA ATANGAZA KIAMA KWA WATUMISHI WALA RUSHWA

Serikali imesema mtumishi anayefanya kazi katika Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (Mkurabita) akibainika kushiriki vitendo vya rushwa atachukuliwa hatua mara moja.

Mkurabita ilianzishwa kwa lengo la kumsaidia anayemiliki ardhi kimila atambulike kisheria na apewe hati itakayomwezesha kupata mkopo ili aendeleze biashara.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), Kapteni mstaafu George Mkuchika alitoa onyo hilo alipotembelea taasisi hiyo. Alisema asingependa kusikia kuna mwananchi anatafuta hati au wanataka eneo lake lipimwe lakini mtumishi wa Mkurabita anamweleza kuwa ili kazi yako iende haraka lazima ‘waonane’ jambo ambalo si sawa.

“Naomba muelewe, anayepambana na rushwa ni Rais mwenyewe kwa sababu Takukuru (Taasisi ya Kuzuia na Kupambana Rushwa) ipo chini yake. Pia, Mkurabita ipo chini ya Ofisi ya Rais Ikulu. 

“Maana yake Waziri wa Mkurabita ni Rais John Magufuli, mimi namsaidia kwa hiyo mnapofanya kazi hapa mjue mkuu wa nchi ndiyo mwenye wizara,” alisema Kapteni Mkuchika ambaye pia ni Mbunge wa Newala Mjini (CCM).

Mratibu wa Mkurabita, Seraphia Mgembe alisema licha ya mafanikio walionayo kuna changamoto ya kutopata fedha za kutosha ili kujiendesha. Alisema mwaka 2009 Mkurabita iliomba Sh43 bilioni kwa ajili kufanya shughuli zake kulingana na mpango kazi wao, lakini fedha walizopata hadi sasa ni asilimia 55 sawa na Sh23 bilioni.

No comments: