Advertisements

Saturday, December 30, 2017

NIDA YATAJA MIKOA INAYOFANYA VIZURI ZOEZI LA USAJILI VITAMBULISHO VYA TAIFA

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Dkt Mwigulu L.Nchemba akiwa ameongozana na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Mhe. Christina Mndeme na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa Ndugu Andrew W. Massawe wakiwasili kwenye viwanja vya Lisaboni –Songea kushiriki sherehe za uzinduzi wa zoezi la Usajili Vitambulisho vya Taifa mkoa wa Ruvuma.
Mhe.Dkt Mwigulu L.Nchemba akikagua baadhi ya Vitambulisho 3470 ambavyo watagawiwa wananchi wa Kata ya Songea ambao Usajili wao umekamilika kufuatia zoezi la Usajili Vitambulisho kuwa kufanyika katika Kata za karibu kabla ya kuanza Usajili wa Umma. Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Mhe. Christina Mndeme na Katikati ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Nida Ndugu Andrew W. Massawe.
Mhe Waziri akimkabidhi Kitambulisho chake mmoja wa wananchi wa Kata ya Songea Bwana Hassan Ally Shomari wakati wa zoezi la ugawaji Vitambulisho kwenye sherehe za uzinduzi wa zoezi la Usajili kwa mkoa wa Ruvuma. Jumla ya Vitambulisho 3470 viligawanywa kwa wanachi wakati wa sherehe hizo.
kikundi cha burudani za asili maarufu kama wana Lizombe wakitumbuiza wakati wa sherehe za uzinduzi wa zoezi la Usajili kwa mkoa wa Ruvuma.
Viongozi wakiongozwa na Mhe. Mhe.Dkt Mwigulu L.Nchemba, Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Mhe. Christina Mndeme na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA Ndugu Andrew W. Massawe wakicheza ngoma ya kabila la Wangoni maarufu kama Lizombe kwenye uzinduzi wa zoezi la Usajili Vitambulisho vya Taifa kwa wanachi kwa Mkoa wa Ruvuma.
Baadhi ya wananchi wakiwa kwenye foleni ya kupokea vitambulisho vyao kwenye uwanja wa Lisaboni wakati wa sherehe za uzinduzi wa zoezi la usajili Vitambulisho vya Taifa mkoani Ruvuma. 

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) Ndg Andrew W. Massawe ameitaja mikoa ya Mara, Arusha, Iringa, Geita, Lindi, Simiyu, Mbeya na Songwe kuwa mikoa inayoongoza katika zoezi la kuwasajili wananchi kupata Vitambulisho vya Taifa; huku mikoa mingine ikiwa nyuma kiusajili kulinganisha na malengo waliyowekewa.

Akizungumza katika sherehe za uzinduzi wa zoezi la usajili kwa mkoa wa Ruvuma lilofanyika katika viwanja vya Lisaboni-Songea, Ndugu Massawe amemuomba Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Mwigulu Nchemba kusaidia kuweka msukumo kwa viongozi na wananchi kwenye mikoa ambayo haifanyi vizuri ili iongeze kasi ya usajili kwa lengo la kukamilisha usajili kwenye mikoa yao kwa muda uliopangwa.

Akihutubia wananchi wa Ruvuma waliofurika kwenye viwanja vya Lisaboni vilivyopo nje kidogo ya mji wa Songea, Waziri wa Mambo wa Ndani ya Nchi Mhe.Dkt Mwigulu Lameck Nchemba amewasisitizia wananchi kujitokeza kwa wingi kusajiliwa kwani kuwa na kitambulisho cha Taifa siyo suala la hiyari ni wajibu kwa kila Mtanzania mwenye sifa kuwa nacho.

“ Mhe. Rais wetu ametoa hela za kuwasajili, zoezi ni bure bado kujisajiliwa kwenda kupigwa picha na kuchuliwa alama za vidole ikushinde?” aliuliza Waziri huyo mwenye dhamana kubwa katika kusimamia utekelezaji wa zoezi hilo.

Aidha amewataka viongozi wa Mikoa na wote wenye dhamana katika kusimamia zoezi hili kuhakikisha wanashirikiana kwa karibu na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa katika kuhakikisha wananchi wenye sifa wanasajiliwa na kamwe pasiwepo wageni watakaojipenyeza kusajiliwa Vitambulisho vya Taifa kama raia. 

“Kwakuwa NIDA inatoa vitambulisho vya aina tatu, cha Raia, Mgeni na Mkimbizi basi niwaombe wageni badala ya kufanya udanganyifu wajisajili kwa hadhi yao kwani siyo dhamira ya Serikali kumfukuza yeyote lakini kuwatambua Raia wake kama ilivyo kwa nchi nyingine duniani” alisema

Naye Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Mhe. Christina Mndeme amemhakikishia Mhe. Waziri mkoa wake uko tayari kusimamia na kuhakikisha wananchi wote wenye sifa wanasajiliwa na kupata Vitambulisho ndani ya muda uliopangwa na kwamba kamwe hata mvumilia mtu yeyote ambaye atakuwa kikwazo katika utekelezaji wa zoezi hilo kwa wananchi; akiwakemea wanasiasa kuingiza siasa kwenye zoezi la Usajili wananchi vitambulisho vya Taifa.

Mkoa wa Ruvuma wenye Wilaya 5 unakisiwa utawasajili zaidi ya wananchi 900,000 katika zoezi lililopangwa kumalizika ndani ya miezi mitatu. Tayari NIDA imekamilisha usambazaji wa vifaa na kutoa mafunzo kwa maafisa ambao watatumika kuwasajili wananchi wa Ruvuma na viunga vyake.

Mikoa mingine inayoendelea na Usajili kwa sasa ni Iringa, Mbeya, Njombe, Singida, Manyara, Arusha, Kilimanjaro, Mwanza, Shinyanga, Geita, Simiyu, Mara, Songwe, Lindi na Mtwara.

No comments: