Advertisements

Tuesday, December 26, 2017

Wanachama Wengine 1200 wa CHADEMA Watimkia CCM

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimezidi kumomonyoka baada ya wanachama wao zaidi 1,200, wakiwemo viongozi wakuu wa Wilaya ya Ngorongoro, kuhamia Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Miongoni mwa viongozi waliohama ni pamoja na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema wa Wilaya Ngorongoro, Samweli Ole Nakumbale, aliyekuwa mgombea ubunge wa jimbo hilo mwaka 2015, Elias Ngorisa na aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Vijana (BAVITA) Wilaya ya Ngorongoro, Wiliam ole Telele.

Wakizungumza baada ya kuomba kurudi CCM na kupokewa wakati wa uzinduzi wa kampeni za CCM za ubunge katika Jimbo la Longido juzi, walisema kuwa ubinafsi ndani ya Chadema umekithiri na vyeo katika chama hicho hutolewa kwa kuangalia sura na ukabila.

“Nilikuwa kada wa CCM nikachukuliwa na mafuriko ya mwaka 2015 nimekaa huko hakuna kipya ni usanii mtupu. Chama hakina hata ofisi ya wilaya kwenye baadhi ya mikoa lakini baada ya kulinganisha nikaona kweli nimepotea njia,” alisema Nakumbale.

Naye Ngorisa alisema mwanaume mwenye busara, ni yule anayejitafakari na kujitathimini katika maamuzi yake. “Nimekaa nimetafakari kwa kina, nikaona kweli kuna mahali nilikosea na ndiyo maana nikaamua kurudi CCM, kwa kuwa ilani yake inatekelezeka kwa vitendo na wananchi wanafurahia utendaji wa Rais John Magufuli”.

Alisema kibaya zaidi amekuwa akiandikwa vibaya kila siku kwenye mitandao ya kijamii kwa mambo ya uongo na uzushi yasiyokuwa na tija, hali ambayo imemfanya arudi CCM. 

“Nimetuhumiwa sana kwenye mitandao nikiitwa msaliti wakati si kweli, lakini sasa kutokana na tuhuma zao ambazo hazikuwa na mashiko nimeamua kurudi CCM.

“Nimekuwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro kwa miaka 10 kupitia CCM na ukweli kuna mahali tulikosea baadhi ya viongozi, tulikuwa na maslahi binafsi badala ya kuhangaika na kero za wananchi, lakini Mungu ametupa Rais mzalendo aliyejitoa sadaka kwa ajili ya kupambana na mafisadi na kusimamia rasilimali za nchi,” alisema.

Kwa upande wake, mfanyabiashara maarufu katika Wilaya ya Longido ambaye pia ni Laigwanani wa mila ya jamii ya Kimasai, Eliya Malari alisema wazee wa mila walilala kwake siku 10 wakimuomba arudi CCM, na baada ya kutafakari utendaji wa Rais Magufuli, alikubali ombi la wazee hao na kuamua kurudi CCM na wafuasi wake

No comments: