Advertisements

Friday, January 12, 2018

KAMISHNA WA MAADILI AWATAKA VIONGOZI KUTOA USHIRIKIANO WAKITAKIWA KUWASILISHA BENK STATEMENT

Kamishna wa Maadili Jaji (Mst) Harold Nsekela amewataka viongozi wa umma kutoa ushirikiano kwa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi pindi watakapotakiwa kuwasilisha pamoja na nyaraka nyingine “bank statement zao” kama sehemu ya tamko la raslimali na madeni.
Akizungumza na waandishi wa habari jana (11/1/2018) ofisini kwake jijini Dar es Salaam, Kamishna Nsekela alisema Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Na 13 ya mwaka 1995 inampa mamlaka ya kumuagiza kiongozi kuwasilisha nyaraka za mali anazomiliki zikiwemo hati za mashamba, viwanja, kadi za magali na benk statement kama sehemu ya tamko la raslimali na madeni ya kiongozi.

“Nikiwaandikia barua viongozi kuwataka kuwasilisha benk statement na nyaraka nyingine za mali wanazomiliki watoe ushirikiano kwasababu ni matakwa ya kisheria,” alisema.

Kamishn Nsekela alieleza kuwa baada ya zoezi la kupokea tamko kukamilika tarehe 31 Desemba, 2017, zoezi linaloendelea kwa sasa ni kuchambua matamko hayo ili kuona ni viongozi wapi wataanza kuhakikiwa mali zao.

“Tukifikia wakati wa kuhakiki mali za viongozi baada ya uchambuzi wa matamko yao, watatakiwa kutoa ushirikiano. Tutataka wathibitishe mali hizo walizipataje?,” alisema na kuongeza kuwa viongozi hawatakiwi kuwa na hofu pindi wanapotakiwa kuhakikiwa mali zao kwasababu sheria ya maadili haiwazuii kumiliki mali, isipokuwa wathibitishe walivyozipata.


Kwa mujibu wa Kamhsina Nsekela, Sekretarieti ya Maadili haipokei tamko kuwatunzia viongozi bila kulifanyia kazi ndio maana, lazima zoezi la uhakiki lifanyike.

“Hatupokei matamko ya viongozi kuwatunzia, lazima tuthibitishe waliyoandika ndani vinginevyo hatuna sababu ya kuwepo,” alisema.

“Viongozi wa Umma lazima waelewe kuwa tukienda kuhakiki mali zao, lengo ni kutaka kuthibitisha mali walizonazo nan ni jukumu letu kufanya hivyo sio kuwatuhumu.”

No comments: