Advertisements

Thursday, January 11, 2018

TUNATAKA ARUSHA YENYE MAAMUZI: HERRY JAMES

Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Taifa Ndg Herry James akisalimiana na baadhi ya viongozi wa UVCCM Mkoa wa Arusha mara baada ya kuwasili Mkoani Arusha kwa ziara ya kikazi ya siku mbili. Picha Na Mathias Canal

Na Mathias Canal, Arusha

Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Taifa Ndg Herry James amesifu ushirikiano wa wananchi Mkoani Arusha kwa kuunga mkono juhudi za serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt John Pombe Magufuli katika kusimamia rasilimali za Taifa.

Mwenyekiti huyo ambaye pia ni Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM ameeleza hayo Mara baada ya kuwasilia Mkoani Arusha leo 10 Januari 2018 katika ziara yake ya kikazi ya siku mbili ambapo pamoja na mambo mengine atashiriki kampeni za kumnadi Mgombea Ubunge wa CCM Jimbo la Longido katika uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika hivi karibuni.

Akizungumza na Vijana wa Chama Cha Mapinduzi waliozuru kumlaki katika Mtaa wa Tengeru, Wilaya ya Meru, Herry aliwasisitiza Vijana hao kuendeleza mahusiano mazuri kwa Chama na serikali ili kuwa na jamii yenye nidhamu, weledi na mtazamo chanya katika utendaji.

Alisema pia mahusiano mazuri ndio msingi wa ushindi wa ngazi mbalimbali ikiwemo uchaguzi mdogo wa udiwani uliomalizika hivi karibuni na CCM kuibuka kidedea kwa zaidi ya asilimia 97%.

Aidha, Herry amewafikishia vijana hao salamu za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Taifa kuwa amemuelekeza kushiriki kampeni za Uchaguzi mdogo ambapo pamoja na mambo mengine Rais Magufuli anatarajia matokeo ya ushindi wa kishindo katika chaguzi zote za marudio nchini.


Aliongeza kuwa katika kipindi kirefu Mkoa wa Arusha umekuwa na viongozi wasiokuwa na maamuzi lakini kupitia serikali ya awamu ya Tano viongozi wengi wamekuwa na maamuzi muhimu na mazuri kwa wakati sahihi huku akisifu uwajibikaji wa Kamishna wa CCM Mkoa wa Arusha ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa huo Mhe Mrisho Gambo.

Sambamba na hayo pia amewasihi Vijana wote nchini kusimamia kile wanachokiamini kwa maslahi ya wengi na kuwa na maamuzi yakinifu kwa wakati sahihi. 

MWISHO

No comments: