Advertisements

Thursday, January 18, 2018

WAZIRI MKUU AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA DARAJA MTO MARA

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akihutubia mkutano wa hadhara katika kijiji cha Nyamongo wilayani Tarime Januari 18, 2018. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa daraja la mto Mara linalounganisha wilaya za Tarime na Serengeti akiwa katika ziara ya mkoa wa Mara Januari 18, 2018. 
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akikata utepe kuweka jiwe la msingi la daraja la mto Mara linalounganisha wilaya za Serengeti na Tarime Januari 18, 2018. Wengine kutoka kushoto ni Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Josephat Kandege , Mwenyekiti wa CCM wa mkoa wa Mara, Samweli Kiboyi, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Adam Malima na Mkuu wa wilaya ya Serengeti, Nurdin Babu. 
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimwagilia mti alioupanda baada ya kuweka jiwe la musing la ujenzi wa daraja la mto Mara linalounganisha wilaya za Tarime na Serengeti akiwa katika ziara ya mkoa wa Mara, Januari 18, 2018.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizunguma na wananchi wa Kijiji cha Nyamwaga wilayani Tarime akiwa katika ziara ya mkoa wa Mara , Januari 18, 2018. Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa mradi wa Daraja la Mto Mara katika barabara ya Tarime-Mugumu unaogharimu sh. bilioni 6.803.

Ameweka jiwe hilo la msingi leo (Alhamisi, Januari 18, 2018) baada ya kuwasili wilayani Serengeti kwa ziara ya kikazi akitokea wilayani Tarime mkoani Mara.

Mkataba wa ujenzi wa daraja hilo ulitiwa saini Februari 23, 2017 na kazi ilianza rasmi Machi 2, 2017 na linatarajiwa kukamilika Machi, 2018.

Amesema lengo la Serikali ni kuziunganisha wilaya hizo kwa barabara ya lami na wameanza na ujenzi daraja hilo.

Waziri Mkuu amesema kuwa daraja hilo litakuwa na barabara za maungio zenye urefu wa mita 900 kila upande na upana wa mita 6.5 na mabega ya mita 1.5 kila upande.

Kukamilika kwa daraja hilo kutafungua fursa za kibiashara na kiuchumi kati ya wilaya hizo za Tarime na Serengeti  pamoja na nchi jirani ya Kenya.

Awali, Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mhandisi Mlima Ngaile alisema daraja hilo linajengwa na makapuni mawili ya kizalendo.

Alisema daraja hilo lina urefu wa mita 94 na upana wa mita 9.9, ambapo sehemu ya kupita magari ni mita 7.5 na watembea kwa miguu mita 1.175 kwa kila upande.

Mhandisi huyo alisema kwa muda mrefu mawasiliano ya wakazi wa Tarime na Serengeti pamoja na Kenya kibiashara na kiuchumi yamekua ya shida kwa kutokuwa na daraja imara.

“Daraja la chuma na mbao lililopo kwa sasa halina uwezo wa kupitisha magari makubwa yanayobeba mazao ya biashara kwa sababu uwezo wake ni kubeba tani 10 tu.”

Alisema kukamilika kwa daraja hilo lenye uwezo wa kubeba tani 56 litakuwa ni suluhu ya matatizo hayo na litaongeza kasi ya utoaji wa huduma za maendeleo kwa jamii inayozunguka wilaya za Tarime na Serengeti.


IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU
ALHAMISI, JANUARI 18, 2018.

No comments: