Advertisements

Wednesday, February 28, 2018

BALOZI SEIF AHAIRISHA MKUTANO WA TISA WA BARAZA LA WAWAKILISHI ZANZIBAR

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiahirisha Mkutano wa Tisa wa Baraza la Tisa la Wawakilishi Zanzibar katika Majengo ya Baraza hilo yaliopo Chukwani Nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.
Baadhi ya Mawaziri wa SMZ na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wakifuatilia Hotuba ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alipotoa Hoja ya Kuahirisha Mkutano wa Tisa wa Baraza la Tisa la Wawakilishi Zanzibar .
Baadhi ya Manaibu Mawaziri wa SMZ na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wakimsikiliza Balozi Seif alipokuwa akisoma Hotuba ya Kuahirisha Mkutano wa Tisa wa Baraza la Tisa la Wawakilishi.
Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar M,h. Zubeir Ali Maulid akiongozwa na Askari wa Baraza hilo wakitoa nje ya Ukumbi baada kufungwa kwa Mkutano wa Tisa wa Baraza la Tisa la Wawakilishi huko Chukwani.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akibadilishana mawazo na Mwakilishi wa Jimbo la Dimani Dr. Mwinyihaji Makame Mwadini baada ya kufungwa kwa Mkutano wa Tisa wa Baraza la Tisa la Wawakilishi.


Picha na – OMPR – ZNZ.
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika mapambano yake dhidi ya vitendo vya udhalilishaji wa Kijinsia vilivyokithiri katika maeneo mbali mbali Nchini, kamwe haitamvumilia, kumuonea aibu, wala muhali Mtu yeyote wa cheo chochote na ngazi yeyote pindi atakapobainika kuhusika na vitendo hivyo.

Akitoa Hoja ya kuahirisha Mkutano wa Tisa wa Baraza la Tisa la Wawakilishi Zanzibar uliokuwa ukifanyika katika Majengo ya Baraza hilo Chukwani Nje kidogo ya Mji wa Zanzibar Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alionya na kutahadharisha wazi kwamba Viongozi na Wananchi wanapaswa kutambua kuwa Sheria ni Msumeno.

Balozi Seif alisema Serikali itaendelea kuchukuwa hatua kali za kisheria dhidi ya wote watakaobainika kushiriki katika kadhia hiyo ikiwemo wafanyaji na wale wote wanaoshiriki katika kuwalinda na kuwakingia kifua wahalifu wote wa masuala ya udhalilishaji wa kijinsia.

Alivinasihi vyombo vya ulinzi na usalama kupambana zaidi dhidi ya vitendo hivyo vinavyolitia aibu Taifa sambamba na kuharibu maisha ya Wananchi, huku Jamii ikipaswa kuendelea kutoa ushirikiano kwa vyombo hivyo katika Mkakati wa kukabiliana na tatizo hilo baya Kijamii na hata Kidini.

Balozi Seif alisema tabia ya baadhi ya Watu hasa Familia kuzimaliza kesi za Udhalilishaji Majumbani itakupunguza kasi ya Serikali kuwashughulikia wahalifu hao na kuwanasihi Wananchi wahusika kufika Mahakamani kwa kutoa ushahidi utakaotoa nguvu ya sheria kuchukuwa mkondo wake na haki kupatikana ili hatimae kuvimaliza vitendo hivyo katika Taifa hili.

Alieleza kwamba Baraza la Wawakilishi tayari limeshapitisha Sheria ya adhabu kwa wahusika wa vitendo vya udhalilishaji, ambapo imeweka bayana kuwa Mtuhumiwa ye yote wa kosa la udhalilishaji hatopaswa kupewa dhamana.

Balozi Seif alifahamisha kwamba Sheria hiyo sasa inangojea kuwekwa saini na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ili iwe Sheria ambapo Mheshimiwa Rais anatarajiwa kuifanya kazi hiyo muda sio mrefu kuanzia hivi sasa.

Akizungumzia suala la ulipaji umeme kwa Deni ya Shirika la Umeme Tanzania {TANESCO} kwa upande wa Zanzibar, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema Serikali ililiamuru Shirika la Umeme Zanzibar {ZECO}kulilipa deni hilo kwa Tanesco kwa kiwango cha Shilingi Bilioni Mbili kwa Mwezi.

Alisema malipo hayo yamepangwa kwenda sambamba na Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar pia kuagizwa kupunguza Deni hilo kwa kiwango cha Shilingi Bilioni Moja kwa Mwezi malipo ambayo yalianza utekelezaji wake.

Hata hivyo Balozi Seif alieleza kwamba utekelezaji huo ulikumbwa na changamoto zilizojitokeza kwa upande wa Shirika la Umeme Zanzibar {ZECO} kwa kutoendelea kulipa kwa ukamilifu kiwango kilichowekwa na Serikali na badala yake Shirika lililipa kwa Miezi Minne tu kuanzia Mwezi Juni, 2017 hadi Oktoba, 2017.

Alisema Miezi iliyofuata ZECO ililipa Deni hilo chini ya kiwango kilichoagizwa kutokana na ukusanyaji mdogo wa mapato yanayotokana na ankara za matumizi ya umeme kutoka kwa baadhi ya Taasisi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na zile za Muungano wa Tanzania zilizopo Zanzibar.

Balozi Seif alisema hali hiyo imepelekea Shirika la Umeme Zanzibar kutokuwa na mapato ya kutosha kulipa deni hilo kila Mwezi badala ya kukidhi mahitaji mengine ya msingi na ya lazima ya kuliendesha Shirika hilo.

Kuhusu suala la upatikanaji wa huduma za Maji safi ya salama Mjini na Vijijini, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alisema Serikali Kuu kwa kushirikiana na Washirika wa Maendeleo imejipanga kutekeleza miradi Minne mikubwa ya huduma hiyo Nchini.

Aliutaja ule Mradi wa Uimarishaji wa Miundombinu katika kubadilisha Mabomba yaliyochakaa wenye urefu wa Kilomita 68 katika Maeneo ya Bumbwisudi, Kinumoshi, Kianga, Welezo, Muembe Mchomeke, Amani pamoja na Kiponda Mji Mkongwe.

Alisema utekelezaji wa Mradi huu unaofadhiliwa na Mfuko wa Maendeleo ya Afrika wa Awamu ya 12 {ADF 12} unatarajiwa kugharimu jumla ya shilingi za Kitanzania Bilioni 48 hadi kukamilika kwake.

Balozi Seif aliutaja mradi mwengine wa Uimarishaji wa miundombinu ya Maji Mjini unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Japan (JICA) kwa gharama ya Shilingi Bilioni 225 za Kitanzania utahusisha ujenzi wa Matangi ya kuhifadhia Maji katika maeneo ya Welezo juu pamoja na Welezo Magharibi.

Alieleza Mradi huo utakwenda sambamba na ulazaji wa Mabomba yenye urefu wa Kilomita 120 katika Zoni ya Migombani pamoja na uwekaji wa huduma za Umeme katika maeneo husika.

Balozi Seif alisema upo mradi mpya wa uimarishaji miundombinu ya Maji Mjini utakaofadhiliwa na Serikali ya India kwa kwa gharama ya Shilingi Bilioni Mia 207 utakaohusisha ulazaji wa Mabomba katika maeneo ya Zoni ya Mfenesini, Kizimbani, Tunguu na Fumba.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alifahamisha kwamba Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China imekubali kufadhili mradi wa uchimbaji Visima 11 pamoja na ulazaji wa Mabomba ndani ya Mkoa Kaskazini Unguja na baadhi ya Wilaya ya Kati na Magharibi “A” unaotarajiwa kugharimu shilingi Bilioni 12 za Kitanzania.

Alisema ili miradi yote iendelee kudumu kwa kipindi kirefu katika utoaji wa huduma zake Wananchi watawajibika kuchangia gharama za uendeshaji wa huduma hiyo kwa wale watakaopata badala ya kubakia na dhana ya uchangiaji wa huduma ya Maji safi ni jukumu la Serikali pekee.

Mkutano wa Baraza la Wawakilishi ulipokea na kujadili Ripoti za Kamati za kudumu Saba za Baraza hilo ambapo pia Wajumbe wa Baraza hilo walijadili na kuipitisha Miswada Mitatu ya Sheria.

Miswada hiyo ni ule wa kufuta Sheria ya kusimamia mwenendo wa Biashara na kumlinda mtumiaji ya Zanzibar Nambari 2 ya Mwaka 1995 na kutunga Sheria Mpya ya Ushindani Halali wa Biashara na Kumlinda Mtumiaji, Kuweka Masharti Bora zaidi pamoja na Mambo Mengine yanayohusiana na hayo.

Mwengine ni Mswada wa Sheria ya kufuta Sheria ya Adhabu na kutunga Sheria Mpya ya Adhabu, Kuweka Masharti Bora zaidi pamoja na Mambo Mengine yanayohusiana na hayo.

Mswada wa Tatu ni ule wa Sheria ya kufuta Sgeria ya Mwenendo wa Jinai Nambari 7 ya Mwaka 2004 na kutunga Sheria Mpya ya Mwenendo wa Jinai na kujweka utaratibu Bora wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai na Usikilizaji wa Kesi za Jinai na Mambo Mengione yanayohusiana na hayo.

Baraza la Wawakilishi Zanzibar limeahirishwa hadi Jumatano ya Tarehe 9 Mwezi Mei Mwaka 2018.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

27/2/2018.

No comments: